Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tunapaswa Kuwa Watu wa Namna Gani?

Tunapaswa Kuwa Watu wa Namna Gani?

‘Munapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu!’​—2 PET. 3:11.

1, 2. ‘Tunapaswa kuwa watu wa namna gani’ ili tukubaliwe na Mungu?

 NI KAWAIDA kuhangaikia namna watu wengine wanavyofikiri juu yetu. Hata hivyo, sisi Wakristo tunapaswa kuhangaikia hata zaidi namna Yehova anavyotuona kwa sababu yeye ndiye mutu mukubwa zaidi katika ulimwengu wote muzima, na yeye ndiye “chemchemi ya uzima.”​—Zab. 36:9.

2 ‘Tunapaswa kuwa watu wa namna gani’ kulingana na maoni ya Yehova? Mutume Petro anapokazia jambo hilo, anatutia moyo tuwe na “matendo matakatifu na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (Soma 2 Petro 3:11.) Ili tukubaliwe na Mungu, “matendo ya mwenendo” wetu yanapaswa kuwa matakatifu, ni kusema, safi​—kiadili, kiakili, na kiroho. Zaidi ya hilo, tunahitaji kufanya “vitendo vya ujitoaji​-kimungu” kwa kumuogopa Mungu na kuwa washikaminifu kwake. Kwa hiyo, ili kukubaliwa na Mungu ni vizuri kuwa na mwenendo muzuri lakini pia ni lazima kuchunguza namna tulivyo kwa ndani. Kwa kuwa Yehova ni ‘muchunguzaji wa moyo,’ anajua ikiwa sisi ni watakatifu katika mwenendo wetu na ikiwa tumejitoa kwake kwa moyo wetu wote ao hapana.​—1 Nya. 29:17.

3. Kuhusu uhusiano wetu pamoja na Mungu, ni maulizo gani ambayo tunapaswa kujiuliza?

3 Shetani Ibilisi hafurahie jitihada tunazofanya ili kukubaliwa na Mungu. Kwa hiyo, anafanya yote anayoweza ili tuvunje uhusiano wetu pamoja na Yehova. Shetani anatumia uongo na ujanja ili kutudanganya na kututenganisha na Mungu tunayemuabudu. (Yoh. 8:44; 2 Kor. 11:13-15) Kwa hiyo, ni jambo la hekima tujiulize hivi: ‘Namna gani Shetani anawadanganya watu? Ninaweza kufanya nini ili nilinde uhusiano wangu pamoja na Yehova?’

NAMNA GANI SHETANI ANAWADANGANYA WATU?

4. Shetani anavizia nini ili kujaribu kuvunja uhusiano wetu pamoja na Mungu, na sababu gani?

4 Mutume Yakobo aliandika hivi: ‘Kila mutu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa zambi; nayo zambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.’ (Yak. 1:14, 15) Ili kujaribu kuvunja uhusiano wetu pamoja na Mungu, Shetani anavizia chanzo cha tamaa zetu, ni kusema, moyo wetu.

5, 6. (a) Shetani anatumia njia gani ili kutudanganya? (b) Shetani anatumia vishawishi gani ili kujaribu kupotosha tamaa za moyo wetu, na amekuwa na ufundi gani katika kutumia vishawishi hivyo?

5 Shetani anatumia njia gani ili kudanganya moyo wetu? Biblia inasema hivi: ‘Ulimwengu muzima unakaa katika nguvu za yule muovu.’ (1 Yoh. 5:19) Silaha za Shetani zinatia ndani “vitu vilivyo katika ulimwengu.” (Soma 1 Yohana 2:15, 16.) Kwa miaka mingi, Shetani ametumia kwa ujanja vitu vinavyotuzunguka. Kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu huu, tunapaswa kujiepusha na matendo yake ya ujanja.​—Yoh. 17:15.

6 Shetani anatumia njia ambazo zinaweza kupotosha tamaa za moyo wetu. Mutume Yohana anataja njia tatu anazotumia ili kutushawishi: (1) “tamaa ya mwili,”(2) “tamaa ya macho,” na (3) ‘mutu kujionyesha mali yake maishani.’ Shetani alitumia vishawishi hivyo ili kumujaribu Yesu katika jangwa. Kwa kuwa ametumia mitego hiyo kwa miaka mingi, Shetani anaitumia kwa ufundi mwingi leo, na anatumia vishawishi hivyo kulingana na muelekeo wa kila mutu. Mbele ya kuchunguza njia tunazoweza kutumia ili kujilinda, acheni tuone namna Ibilisi alivyotumia vishawishi fulani ili kumudanganya Eva lakini alishindwa kumudanganya Mwana wa Mungu kwa kutumia vishawishi hivyo.

“TAMAA YA MWILI”

“Tamaa ya mwili” ilimuangusha Eva (Ona fungu la 7)

7. Namna gani Shetani alitumia “tamaa ya mwili” ili kumushawishiEva?

7 Ili kuendelea kuishi, wanadamu wanahitaji chakula. Muumbaji wetu alifanya mipango ili dunia itoe chakula kwa wingi. Shetani anaweza kutumia tamaa yetu ya kula ili kutupotosha tusifanye mapenzi ya Mungu. Tuone namna alivyofanya hivyo alipomudanganya Eva. (Soma Mwanzo 3:1-6.) Shetani alimuambia kwamba angeweza kula matunda ya ‘muti wa ujuzi wa mema na mabaya’ bila kufa, alimuambia Eva kwamba siku tu angekula matunda ya muti huo, angekuwa kama Mungu. (Mwa. 2:9) Ni kama vile Ibilisi alisema kwamba si lazima Eva amutii Mungu ili aendelee kuishi. Huo ulikuwa uongo mutupu kabisa! Shetani alipoingiza wazo hilo katika akili yake, Eva alikuwa na maamuzi mawili: Kukataa wazo hilo, ao kuendelea kulifikiria ili kukomalisha tamaa ya kula tunda hilo. Ijapokuwa aliruhusiwa kula matunda ya miti mingine yote ya shamba, Eva aliamua kusikiliza mambo ambayo Shetani alisema kuhusu muti uliokuwa katikati ya bustani, na ‘alianza kuchukua kati ya matunda yake akala.’ Kwa hiyo, Shetani alianzisha ndani mwake tamaa ya kula kitu ambacho Muumbaji wake alimukataza.

Yesu hakurusu kitu chochote kimukengeushe akili (Ona fungu la 8)

8. Namna gani Shetani alijaribu kumushawishi Yesu kwa kutumia “tamaa ya mwili,” na sababu gani kishawishi hicho hakikufanikiwa?

8 Shetani alitumia ufundi huo huo alipojaribu kumushawishi Yesu katika jangwa. Kisha Yesu kufanya siku 40 muchana na usiku bila kula, Shetani alimujaribu kwa kuchochea tamaa yake kwa ajili ya chakula. Shetani alimuambia hivi: ‘Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, liambie jiwe hili liwe mukate.’ (Lu. 4:1-3) Yesu alikuwa na maamuzi mawili: Kutumia uwezo wake wa kufanya miujiza ili apate chakula, ao kutotumia uwezo huo. Yesu alijua kwamba hapaswe kutumia uwezo huo kwa ajili ya faida zake mwenyewe. Hata ikiwa alikuwa na njaa, jambo alilotia pa nafasi ya kwanza lilikuwa kuendelea kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova kuliko kutosheleza tamaa ya chakula. Yesu alimujibu Shetani hivi: “Imeandikwa, ‘Mwanadamu ataishi, si kwa mukate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’”​—Mt. 4:4.

“TAMAA YA MACHO”

9. Maneno “tamaa ya macho” yanaonyesha nini, na namna gani Shetani alitumia tamaa hiyo alipomudanganya Eva?

9 Yohana alitaja kishawishi kingine, ni kusema, “tamaa ya macho.” Maneno hayo yanaonyesha kwamba mutu anaweza kuanza kutamani kitu fulani kwa kukitazama tu. Alipozungumuza na Eva, Shetani alichochea tamaa hiyo, kwa kusema hivi: “Macho yenu yatafunguliwa.” Eva alipoendelea kutazama tunda hilo lililokatazwa, tunda hilo lilianza kumuvutia. Eva aliona kwamba muti huo “ulikuwa kitu cha kutamanika kwa macho.”

10. Ni katika njia gani Shetani alitumia “tamaa ya macho” ili kumushawishi Yesu, na Yesu alitenda namna gani?

10 Tuseme nini kuhusu Yesu? Shetani “alimuonyesha [Yesu] mara moja falme zote za dunia inayokaliwa; naye alimwambia: ‘Hakika nitakupa mamlaka yote hii na utukufu wake.’” (Lu. 4:5, 6) Yesu hangeona mara moja falme zote hizo kwa macho yake ya kibinadamu, lakini inawezekana Shetani alifikiri kwamba utukufu wa falme hizo, alizomuonyesha katika maono, ungemuvutia Yesu. Bila kusikia haya, Shetani alimuambia hivi: “Ukifanya tendo la ibada mbele yangu, yote itakuwa yako.” (Lu. 4:7) Yesu hakutaka hata kidogo kumupendeza Shetani. Alimujibu mara moja hivi: “Imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumuabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumutolea utumishi mutakatifu.’”​—Lu. 4:8.

‘MUTU KUJIONYESHA MALI YAKE MAISHANI’

11. Namna gani Shetani alimushawishi Eva?

11 Alipotaja vitu vilivyo katika ulimwengu, Yohana alizungumuzia ‘mutu kujionyesha mali yake maishani.’ Wakati Adamu na Eva walikuwa peke yao duniani, hawangeweza kabisa ‘kuonyesha mali yao maishani’ mbele ya watu wengine. Lakini walionyesha kiburi. Shetani alipomushawishi Eva, alidai kwamba Mungu alimuficha Eva kitu fulani kizuri sana. Alimuambia kwamba siku ileile atakapokula matunda ya ‘muti wa ujuzi wa mema na mabaya,’ ‘atakuwa kama Mungu, akijua mema na mbaya.’ (Mwa. 2:17; 3:5) Shetani alionyesha kwamba Eva angepata uhuru, hangeongozwa tena na Yehova. Inaonekana kwamba kiburi ndicho kilimuchochea kuamini uongo huo. Alikula tunda lililokatazwa, akiamini kwamba kwa kweli hatakufa. Alijidanganya kabisa!

12. Shetani alitumia njia gani nyingine ili kumushawishi Yesu, na Yesu alitenda namna gani?

12 Tofauti na Eva, Yesu alituachia mufano muzuri sana wa unyenyekevu! Shetani alijaribu kumushawishi katika njia nyingine, lakini Yesu alitupilia mbali wazo lolote la kufanya jambo la kushangaza ambalo lingemujaribu Mungu. Hilo lingekuwa tendo la kiburi! Lakini jibu la Yesu lilikuwa wazi na la moja kwa moja: “Imesemwa, ‘Usimujaribu Yehova Mungu wako.’”​—Soma Luka 4:9-12.

NAMNA GANI TUNAWEZA KULINDA UHUSIANO WETU PAMOJA NA YEHOVA?

13, 14. Eleza namna Shetani anavyotumia vishawishi fulani leo.

13 Leo, Shetani anatumia vishawishi hivyo hivyo alivyotumia ili kujaribu Eva na Yesu. Ili kuchochea “tamaa ya mwili,” Ibilisi anatumia ulimwengu wake ili kuchochea watu waendelee kufanya mambo machafu na kula na kunywa kupita kiasi. Kupitia ponografia, inayopatikana zaidi sana kwenye Internete, Shetani anaweza kuwanasa wale wasiokuwa waangalifu na kuchochea “tamaa ya macho.” Pia, Shetani anatumia ufuatiaji wa vitu vya kimwili, kupenda mamlaka na sifa ili kuwashawishi wale walio na kiburi na wale wanaotaka ‘kujionyesha mali yao maishani’!

Ni kanuni gani za Maandiko ambazo unapaswa kukumbuka unapokuwa katika hali hizi? (Ona fungu la 13 na 14)

14 “Vitu vilivyo katika ulimwengu” vinaweza kufananishwa na chambo ambacho muvuaji wa samaki anatumia. Vitu vilivyo katika ulimwengu vinavutia, lakini kila kimoja kimefungwa kwenye ndoano. Shetani anatumia mambo ambayo watu wanaweza kuona kuwa mahitaji ya kawaida ya kila siku ili kuwafanya watende mambo yanayopingana na sheria za Mungu. Hata hivyo, kusudi la vishawishi hivyo vyenye ujanja ni kuamusha tamaa zetu na kupotosha moyo wetu. Kwa kweli vishawishi hivyo vinatufanya tuamini kwamba kuhangaikia mahitaji yetu wenyewe na kutafuta maisha ya raha ni jambo la maana sana kuliko kufanya mapenzi ya Mungu. Je, tutaacha tushindwe na vishawishi hivyo?

15. Namna gani tunaweza kumuiga Yesu katika kupinga vishawishi vya Shetani?

15 Eva alianguka katika vishawishi vya Shetani, lakini Yesu alishinda vishawishi hivyo. Kila wakati, Yesu alijibu kulingana na Maandiko kwa kusema hivi: “Imeandikwa” ao, “Imesemwa.” Ikiwa sisi ni wanafunzi wa Biblia wenye bidii, tutaelewa vizuri Maandiko, tutakumbuka maandiko yanayoweza kutusaidia tuendelee kuchukua maamuzi mazuri tunapopambana na kishawishi. (Zab. 1:1, 2) Kukumbuka mifano inayopatikana katika Maandiko ya watu waaminifu waliokuwa washikamanifu kwa Mungu, kunaweza kutusaidia tuwaige. (Rom. 15:4) Kumuogopa Yehova, kupenda mambo ambayo anapenda na kuchukia mambo ambayo anachukia, kutatulinda.​—Zab. 97:10.

16, 17. “Nguvu za kufikiri” zinaweza kutusaidia namna gani?

16 Mutume Paulo anatutia moyo tutumie “nguvu zetu za kufikiri” ili tuwe watu wanaoongozwa na mawazo ya Mungu, wala si mawazo ya ulimwengu. (Rom. 12:1, 2) Alipokazia uhitaji wa kulinda vizuri mawazo yetu, Paulo alisema hivi: ‘Kwa maana sisi tunapindua mawazo na kila jambo lililo juu sana ambalo limeinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu; nasi tunaiteka kila fikira ili kuifanya imutii Kristo.’ (2 Kor. 10:5) Mawazo yetu yanaweza kutuchochea kutenda mambo mazuri ao mabaya, kwa hiyo ni lazima “kuendelea kufikiria” mambo yenye kujenga.​—Flp. 4:8.

17 Hatuwezi kutazamia kuwa watakatifu ikiwa tunaendelea kujaza katika akili na moyo wetu mawazo na tamaa mbaya. Tunapaswa kumupenda Yehova na “moyo safi.” (1 Tim. 1:5) Lakini moyo ni mudanganyifu, na pengine “vitu vilivyo katika ulimwengu” vinaweza kuanza kutuvutia sana bila sisi kujua. (Yer. 17:9) Kwa hiyo, tunapaswa ‘kuendelea kujijaribu kama tuko katika imani, kuendelea kusibitisha sisi wenyewe jinsi tulivyo’ kwa kujichunguza kikweli kupitia mambo tunayojifunza katika Biblia.​—2 Kor. 13:5.

18, 19. Sababu gani tunapaswa kuazimia kuwa watu wa namna ambayo Yehova anataka tuwe?

18 Jambo lingine linaloweza kutusaidia kupinga “vitu vilivyo katika ulimwengu” ni kuendelea kuweka katika akili maneno haya ya mutume Yohana: “Ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yoh. 2:17) Ulimwengu wa Shetani unaonekana kuwa hauwezi kuwa na mwisho. Lakini, siku moja ulimwengu huo utafikia mwisho wake. Kila kitu ambacho ulimwengu wa Shetani unaweza kututolea hakiwezi kudumu. Kukumbuka jambo hilo kutatusaidia tusidanganywe na vishawishi vya Ibilisi.

19 Mutume Petro anatutia moyo tuwe watu wenye kukubaliwa na Mungu ‘tunapongojea na kuweka akilini kuwapo kwa siku ya Yehova, kupitia hiyo mbingu zikiwa zimewaka moto zitayeyushwa na vitu vya musingi vikiwa moto sana vitayeyuka!’ (2 Pet. 3:12) Siku hiyo itafika hivi karibuni, na Yehova ataharibu sehemu zote za ulimwengu wa Shetani. Mupaka wakati huo, Shetani ataendelea kutumia “vitu vilivyo katika ulimwengu” ili kutujaribu, kama vile alivyojaribu Eva na Yesu. Tusiwe hata kidogo kama Eva na tusitafute kutosheleza tamaa zetu wenyewe. Kufanya hivyo kungekuwa sawa na kumuona Shetani kuwa mungu wetu. Tunahitaji kuwa kama Yesu na kupinga vishawishi hivyo, hata ikiwa vinaonekana kuwa vyenye kupendeza na kuvutia sana. Acheni kila mumoja wetu aazimie kuwa mutu wa namna ambayo Yehova anataka tuwe.