Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Namna Mukristo Anaweza Kufanya Ndoa Yake Ikuwe ya Muzuri

Namna Mukristo Anaweza Kufanya Ndoa Yake Ikuwe ya Muzuri

‘Kila mutu mumoja-mumoja kati yenu na amupende hivyo muke [bibi] wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; . . . muke anapaswa kumuheshimu sana mume [bwana] wake.’WAEFESO 5:33.

NYIMBO: 87, 3

1. Kwa kawaida ndoa inaanza na furaha, lakini bibi na bwana wanajua kama wanaweza kupatwa na nini? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

WAKATI bwana-arusi anamuona bibi-arusi wake mwenye sura ya muzuri siku ya ndoa yao, wote wawili wanafurahi sana. Wakati wa uchumba, upendo wao uliendelea kuongezeka sana na walipenda kuoana. Kwa hiyo, waliahidi kama kila mumoja atabakia muaminifu kwa mwenzake. Kisha siku ya ndoa yao, wakati wanaanza kuishi pamoja, watakuwa na lazima ya kufanya mabadiliko ili waendelee kuwa na umoja. Yehova, mwenye alianzisha ndoa, anataka bibi na bwana wakuwe na ndoa ya muzuri na yenye furaha. Kwa hiyo, amewapatia mashauri yenye hekima katika Neno lake, Biblia. (Methali 18:22) Hata hivyo, Biblia inatuonyesha kama watu wenye hawakamilike wenye wanaoana watakuwa na magumu, ao ‘ziki katika mwili wao.’ (1 Wakorintho 7:28) Namna gani bibi na bwana wanaweza kupunguza magumu hayo? Na namna gani Wakristo wanaweza kufanya ndoa yao ikuwe ya muzuri?

2. Ni aina gani za upendo bibi na bwana wanapaswa kuonyeshana?

2 Biblia inasema kama upendo ni sifa ya maana. Lakini kuko aina mbalimbali za upendo zenye bibi na bwana wanapaswa kuonyeshana katika ndoa. Kwa mufano, wanapaswa kuonyeshana upendo wenye upole na kuonyeshana mapenzi. Na kama wako na watoto, upendo kati ya watu wa familia ni jambo la maana hata zaidi. Lakini upendo wenye kuongozwa na kanuni ndio unafanya ndoa ikuwe ya muzuri kabisa. Mutume Paulo alieleza upendo huo wakati aliandika hivi: ‘Kila mutu mumoja-mumoja kati yenu na amupende hivyo muke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, muke anapaswa kumuheshimu sana mume wake.’—Waefeso 5:33.

BIBI NA BWANA WAKO NA MADARAKA GANI?

3. Bibi na bwana wanapaswa kupendana kwa kiasi gani?

3 Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Enyi waume, muendelee kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.’ (Waefeso 5:25) Leo, Wakristo wanaiga mufano wa Yesu kwa kupendana kama vile Yesu alipenda wanafunzi wake. (Soma Yohana 13:34, 35; 15:12, 13.) Bwana na bibi Wakristo wanapaswa kupendana sana, na upendo huo unafanya kila mumoja wao akuwe tayari kufa kwa ajili ya mwengine. Lakini wakati magumu mazito yanatokea katika ndoa, wengine wanaweza kufikiri kama upendo wao hauko wenye nguvu sana. Ni nini inaweza kuwasaidia? Ni upendo wenye kuongozwa na kanuni, wenye ‘unahimili mambo yote, unaamini mambo yote, unatumaini mambo yote, unavumilia mambo yote.’ Upendo kama huo ‘haushindwe kamwe [hata kidogo].’ (1 Wakorintho 13:7, 8) Bibi na bwana wanapaswa kukumbuka kama walifanya naziri ao kiapo. Waliahidi kupendana na kubakia waaminifu kwa mumoja na mwengine. Kukumbuka jambo hilo kutawachochea waendelee kutafuta musaada wa Yehova na kutumika pamoja ili kumaliza magumu yao.

4, 5. (a) Kwa sababu bwana ndiye kichwa cha familia, ana daraka gani? (b) Namna gani bibi anapaswa kuona ukichwa wa bwana yake? (c) Bibi na bwana fulani walipaswa kufanya mabadiliko gani?

4 Mutume Paulo alizungumuzia madaraka ya bibi na bwana wakati alisema hivi: ‘Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha muke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko.’ (Waefeso 5:22, 23) Haiko kusema kama bwana ni wa maana zaidi kuliko bibi yake. Yehova alizungumuzia daraka la maana sana la bibi wakati alisema hivi: ‘Si vema [haiko muzuri] huyo mwanaume aendelee kuwa peke yake. Nitamufanyia musaidizi, akuwe kikamilisho chake.’ (Mwanzo 2:18) Bibi anapaswa kusaidia bwana yake atimize muzuri daraka lake la kichwa cha familia. Bwana anapaswa kuiga mufano wenye upendo wa Yesu, “kichwa cha kutaniko.” Ikiwa bwana anafanya hivyo, bibi yake atajisikia salama na haitakuwa vigumu kwake kuheshimia na kutegemeza bwana yake.

“Tumekaribiana sana kwa kufanya mambo katika njia yenye kumufurahisha Yehova”

5 Cathy, mwenye ameolewa na Fred, anasema hivi: “Wakati nilikuwa sijaolewa, nilikuwa na uhuru, na nilikuwa ninajihangaikia mimi mwenyewe. Ndoa ilibadilisha maisha yangu kwa sababu nilijifunza kumutegemea bwana yangu. Haikukuwa vyepesi sikuzote, lakini tumekaribiana sana kwa kufanya mambo katika njia yenye kumufurahisha Yehova.” [1] (Soma maelezo kwenye mwisho wa habari hii.) Fred anasema hivi: “Kukamata maamuzi haikukuwa vyepesi kwangu hata kidogo. Katika ndoa, kufikiria mawazo ya watu wawili kunafanya ikuwe vigumu zaidi. Lakini wakati ninatafuta muongozo wa Yehova katika sala na wakati ninasikiliza kabisa mawazo ya bibi yangu, inakuwa vyepesi sana kila siku. Ninaona kama tunaungana mukono kabisa!”

6. Wakati magumu yanatokea katika ndoa, namna gani upendo unaweza kuwa “kifungo kikamilifu cha muungano”?

6 Ndoa inaweza kuwa na nguvu ikiwa bibi na bwana ‘wanaendelea kuvumiliana na kusameheana kwa hiari [kwa kupenda].’ Kwa sababu bibi na bwana hawakamilike, wote wawili wanaweza kufanya makosa. Wakati hilo linatokea, wanaweza kujifunza jambo fulani kupitia makosa yao, wanaweza kujifunza kusameheana, na kuonyeshana upendo wenye kuongozwa na kanuni za Biblia. Upendo huo ni “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:13, 14) Bibi na bwana wanaweza kuonyeshana upendo wa namna hiyo ikiwa wako wavumilivu na wapole na wanaepuka ‘kuweka hesabu ya ubaya.’ (1 Wakorintho 13:4, 5) Wakati hawaelewane, bibi na bwana wanapaswa kujikaza kumaliza haraka kabisa magumu yao mbele usiku uingie. (Waefeso 4:26, 27) Inaomba kuwa munyenyekevu na kuwa na ujasiri ili kusema “unisamehe kwa sababu nimekukwaza,” lakini kufanya hivyo kunasaidia kumaliza magumu na kunafanya bibi na bwana wakaribiane zaidi.

KUTENDEANA KWA UPOLE NI JAMBO LA LAZIMA SANA

7, 8. (a) Biblia inatoa shauri gani juu ya kitendo cha ndoa kati ya bibi na bwana? (b) Sababu gani bibi na bwana wanapaswa kutendeana kwa upole kupitia maneno na matendo?

7 Biblia inatoa mashauri ya muzuri yenye yanaweza kusaidia bibi na bwana wakuwe na mawazo ya muzuri juu ya kitendo cha ndoa. (Soma 1 Wakorintho 7:3-5.) Ni jambo la lazima bibi na bwana wafikirie kila mumoja mahitaji ya mwenzake na namna anajisikia. Ikiwa bwana hamutendee bibi yake kwa upole kupitia maneno na matendo, inaweza kuwa vigumu kwa bibi huyo kufurahia kitendo cha ndoa. Bwana wanapaswa kutendea bibi zao “kulingana na ujuzi.” (1 Petro 3:7) Bibi ao bwana hapaswe hata kidogo kukaza ao kuomba mwenzake wafanye kitendo cha ndoa, lakini wanapaswa kujua kama ni jambo la kawaida katika ndoa. Mara nyingi, mwanaume anaweza kuwa tayari zaidi kuliko mwanamuke. Lakini ni muzuri wafanye hivyo wakati wote wawili wako tayari.

8 Biblia haitoe sheria zenye kuwa wazi juu ya mipaka na namna mbalimbali za mapenzi zenye bibi na bwana wanapaswa kuonyeshana. Lakini inazungumuzia mapenzi hayo. (Wimbo wa Sulemani 1:2; 2:6) Bibi na bwana Wakristo wanapaswa kutendeana kwa upole kupitia maneno na matendo.

9. Sababu gani ni mubaya kuchezea kimapenzi mutu mwenye haiko bibi ao bwana yetu?

9 Ikiwa tunapenda sana Mungu na jirani yetu, hatutaacha mutu yeyote ao jambo lolote liharibishe ndoa yetu. Watu fulani wamefanya ndoa yao ikuwe na magumu ao iharibike kwa sababu wamekuwa watumwa wa pornografia. Tunapaswa kuepuka kila kitu chenye kinaweza kutuchochea tuangalie pornografia, na mambo mengine yenye kuamusha tamaa mbaya ya ngono. Tunapaswa kuepuka hata kitu chochote chenye kufanya ionekane kama vile tunachezea kimapenzi ao kutongoza mutu fulani mwenye haiko bibi ao bwana yetu. Kwa sababu kufanya hivyo ni kukosa upendo. Tunapaswa kukumbuka kama Mungu anajua mawazo na matendo yetu yote. Kukumbuka jambo hilo kutatusaidia tutafute kabisa kupendeza Mungu na kubakia washikamanifu kwa bibi ao bwana yetu.—Soma Mathayo 5:27, 28; Waebrania 4:13.

WAKATI MAGUMU YANATOKEA KATIKA NDOA

10, 11. (a) Ndoa nyingi zinapatwa na nini leo? (b) Biblia inasema nini juu ya kuachana? (c) Ni nini inaweza kusaidia bibi na bwana wasiachane haraka?

10 Wakati bibi na bwana fulani wanashindwa kumaliza magumu mazito, wanaweza kuamua kuachana ao kuvunja ndoa yao. Katika inchi fulani, zaidi ya nusu ya ndoa zenye kufanywa zinavunjika. Kwa kweli, kuvunja ndoa hakutokee mara nyingi katika kutaniko la Kikristo. Lakini, Wakristo wengi zaidi wanaendelea kupata magumu mazito katika ndoa zao.

11 Biblia inatoa maagizo haya: ‘Muke hapaswe kuondoka kwa mume wake. Lakini kwa kweli akiondoka, na akae museja [bila kuolewa] kama sivyo apatane tena na mume wake; na mume hapaswe kumuacha muke wake.’ (1 Wakorintho 7:10, 11) Bibi na bwana fulani wanaweza kuamua kuachana kwa sababu wanaona kama magumu yao ni mazito sana. Lakini, Yesu alionyesha kama kuachana haiko jambo la muchezo wakati alirudilia maneno yenye Mungu alikuwa amesema tangu mwanzo juu ya ndoa. Kisha Yesu aliongeza hivi: ‘Kile ambacho Mungu ameunganisha mutu yeyote asikitenganishe [asikiachanishe].’ (Mathayo 19:3-6; Mwanzo 2:24) Kwa hiyo, Yehova anapenda bibi na bwana wasiachane. (1 Wakorintho 7:39) Sisi wote tunapaswa kukumbuka kama tutatoa hesabu kwa Yehova kwa ajili ya matendo yetu. Jambo hilo linaweza kutusaidia tumalize magumu haraka mbele yakuwe mazito zaidi.

Bibi na bwana Wakristo wanamaliza magumu yao kwa sababu wanamuacha Mungu awaongoze

12. Ni nini inaweza kufanya bibi ao bwana afikirie kuachana na mwenzake?

12 Sababu gani bibi na bwana fulani wanapata magumu mazito katika ndoa yao? Wamoja hawapate mambo yenye waliwazia kupata katika ndoa, kwa hiyo wanavunjika moyo ao wanakasirika. Mara nyingi, namna watu walikomaa ao namna wanajisikia katika moyo wao inaleta magumu mbalimbali. Pia, bibi ao bwana anaweza kupata magumu na watu wa familia ya mwenzake ao wanaweza kukosa kuelewana juu ya namna ya kutumia feza ao namna ya kukomalisha watoto. Lakini, ni jambo lenye kufurahisha kuona kama bibi na bwana wengi Wakristo wanamaliza magumu yao kwa sababu wanamuacha Mungu awaongoze.

13. Ni sababu gani zenye kufaa zenye zinaweza kufanya bibi na bwana waachane?

13 Kunaweza kuwa sababu zenye kufaa za kufanya bibi na bwana waachane. Hali ngumu kama vile kukataa kimakusudi kutimiza mahitaji ya watu wa familia, kutendewa mubaya sana kimwili, ao kutia kabisa hali ya kiroho ya Mukristo katika hatari zimefanya bibi ao bwana fulani waamue kuachana. Wakati bibi na bwana wanapata magumu mazito, wanapaswa kuomba musaada kwa wazee wa kutaniko. Wanaume hao wako na uzoefu mwingi na wanaweza kusaidia bibi na bwana watumie mashauri ya Biblia katika maisha yao. Na wakati bibi na bwana wanamuomba Yehova roho yake takatifu, inaweza kuwasaidia watumie kanuni za Biblia na kuonyesha sifa za Kikristo. (Wagalatia 5:22, 23) [2]—Soma maelezo kwenye mwisho wa habari hii.

14. Biblia inatoa shauri gani kwa Wakristo wenye wameoa ao kuoelewa na watu wenye hawako Mashahidi?

14 Biblia inaonyesha kama kuko sababu zenye kufaa zenye kufanya bibi na bwana wasiachane hata kama mumoja kati yao haiko mutumishi wa Yehova. (Soma 1 Wakorintho 7:12-14.) Bibi ao bwana mwenye haiko Shahidi ‘anatakaswa’ kwa sababu ameoa ao kuolewa na mutumishi wa Mungu. Mungu anaona watoto wao wadogo kuwa “watakatifu” na kwa hiyo, anawalinda. Mutume Paulo alitia moyo bibi na bwana Wakristo kwa kusema hivi: ‘Kwa maana, wewe muke, unajuaje kama utamuokoa mume wako? Ao, wewe mume, unajuaje kama utamuokoa muke wako?’ (1 Wakorintho 7:16) Kuko mifano mingi ya muzuri ya Wakristo wenye wamesaidia bwana ao bibi zao wakuwe watumishi wa Yehova.

15, 16. (a) Biblia inatoa shauri gani kwa bibi Wakristo wenye kuwa na bwana wenye hawako Mashahidi? (b) Mukristo atafanya nini ikiwa bibi ao bwana yake mwenye haiko Shahidi anaamua ‘kuondoka’?

15 Mutume Petro alishauria bibi Wakristo wajitiishe kwa bwana zao, “ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili [mwenendo muzuri] pamoja na heshima kubwa.” Kuliko kuzungumuzia kila wakati mambo yenye anaamini, bibi anaweza kusaidia zaidi bwana yake akubali kweli ikiwa anaonyesha ‘roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya samani kubwa [maana sana] machoni pa Mungu.’—1 Petro 3:1-4.

16 Biblia inasema nini ikiwa bibi ao bwana mwenye haiko Shahidi wa Yehova anaamua kuachana na mwenzake? Inasema hivi: “Yule asiyeamini akiondoka, acha aondoke; ndugu ao dada hayumo [haiko] katika utumwa chini ya hali za namna hiyo, lakini Mungu amewaita ninyi kwenye amani.” (1 Wakorintho 7:15) Hata kama kuachana kunaweza kusaidia mutu akuwe na amani kwa kiasi fulani, Biblia hairuhusu Mukristo mwenye ameachana na bibi ao bwana yake aoe ao kuolewa tena. Lakini Mukristo hapaswe kulazimisha bibi ao bwana yake abakie. Kisha wakati fulani, bibi ao bwana mwenye haiko Shahidi anaweza kuamua kurudia katika ndoa yake. Na wakati unaokuja, bibi ao bwana mwenye haiko Shahidi anaweza hata kuwa mutumishi wa Yehova.

WAKRISTO WANAPASWA KUTIA NINI PA NAFASI YA KWANZA KATIKA NDOA YAO?

Wakati tunatia ibada yetu kwa Yehova pa nafasi ya kwanza, tunaweza kuwa na furaha zaidi katika ndoa yetu (Picha hii inapatana na fungu la 17)

17. Bibi na bwana Wakristo wanapaswa kutia nini pa nafasi ya kwanza katika ndoa yao?

17 Kwa sababu tunaishi kwenye mwisho wa “siku za mwisho,” tuko katika ‘nyakati za hatari zilizo ngumu kushugulika nazo.’ (2 Timotheo 3:1-5) Ndiyo sababu, tuko na lazima ya kuwa na urafiki wenye nguvu pamoja na Yehova ili kupata ulinzi. Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Wakati uliobaki umepunguka. Tangu sasa wale walio na wake na wakuwe kana kwamba hawana, . . . na wale wanaoutumia ulimwengu wakuwe kama wale wasioutumia kwa ukamili.’ (1 Wakorintho 7:29-31) Paulo hakupenda kusema kama watu wenye kuoana hawapaswe kuhangaikiana. Lakini, kwa sababu tunaishi katika siku za mwisho, tunapaswa kutia ibada yetu kwa Yehova pa nafasi ya kwanza.—Mathayo 6:33.

18. Sababu gani inawezekana Wakristo wakuwe na ndoa ya muzuri na yenye furaha?

18 Katika siku hizi za mwisho, ndoa nyingi zinaendelea kuharibika. Inawezekana kuwa na ndoa ya muzuri na yenye furaha? Ndiyo, ikiwa tunabakia karibu na Yehova na watu wake, ikiwa tunatumia kanuni za Biblia, na kutii mwongozo wa roho takatifu ya Yehova. Ikiwa tunafanya hivyo, tunaheshimia, “kile ambacho Mungu ameunganisha.”—Marko 10:9.

^ [1] (fungu la 5) Majina yamebadilishwa.

^ [2] (fungu la 13) Soma nyongeza, “Mambo Ambayo Biblia Inafundisha Kuhusu Kuvunja Ndoa na Kutengana,” katika kitabu Mubaki “Katika Upendo wa Mungu,” ukurasa wa 219-221.