Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MATUKIO MUHIMU YA MWAKA ULIOPITA

Ripoti ya Mambo ya Kisheria

Ripoti ya Mambo ya Kisheria

Mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo: “Wakumbukeni wale walio katika vifungo vya gereza kana kwamba ninyi mmefungwa pamoja nao.” (Ebr. 13:3) Tukiwa waabudu wa Yehova, tunaendelea kuwakumbuka ndugu na dada zetu waaminifu na kusali kwa ajili ya “wale wote walio katika cheo cha juu; ili tuendelee kuishi maisha shwari na matulivu pamoja na ujitoaji-kimungu kamili na kuchukua mambo kwa uzito.”1 Tim. 2:1, 2, Efe. 6:18.

Vifuatavyo ni baadhi ya visa ambavyo Mashahidi wa Yehova wamekabiliana navyo mwaka uliopita:

Ndugu zetu nchini Urusi wanaendelea “bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema” licha ya jitihada za Kanisa Othodoksi la Urusi na baadhi ya maofisa wa serikali kuzuia kazi yetu. (Mdo. 5:42) Wenye mamlaka nchini Urusi wanatumia vibaya sheria isiyo wazi kuhusu watu wenye msimamo mkali wa kidini ili kuzuia machapisho yetu na kuwanyanyasa ndugu zetu. Sheria hiyo ilitungwa hasa ili kukabiliana na ugaidi. Matokeo ni kwamba Mahakama za Urusi zimesema kwamba machapisho yetu 70 hivi yana maneno yanayochochea watu kuwa na msimamo mkali, na serikali imeyaongeza kwenye orodha ya taifa ya machapisho yaliyopigwa marufuku kwa sababu ya msimamo mkali. Wakidai kwamba machapisho hayo ni hatari, baadhi ya maofisa wa serikali wanavamia Majumba ya Ufalme na nyumba za ndugu zetu ili kutafuta machapisho hayo. Polisi wanawakamata, wanawapiga picha, na kisha kuwachukua alama za vidole Mashahidi wengi kwa sababu ya kushiriki katika utumishi wa shambani. Mara nyingi wao hujaribu kuwatisha ndugu zetu wanapowazuia kwenye kituo cha polisi.

 Kuanzia Mei 2013, ndugu na dada 16 jijini Taganrog walishtakiwa kwa kosa la kupanga, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Hii ni mara ya kwanza tangu kuanguka kwa Muungano wa Sovieti kwa Mashahidi kushtakiwa kwa sababu ya kushiriki katika mambo yanayohusiana na imani yao. Wenye mamlaka katika maeneo mengine ya Urusi wanajaribu kuzishinikiza mahakama zitangaze machapisho yetu kuwa yenye “msimamo mkali,” na kuwashtaki ndugu zetu kwa kosa la kuchochea chuki ya kidini.

Hali ya ndugu na dada zetu nchini Eritrea haijabadilika. Kufikia Julai 2013, Mashahidi 52 walikuwa gerezani, kutia ndani ndugu nane wenye umri wa miaka 70 hivi na dada sita. Ndugu watatu, Paulos Eyassu, Isaac Mogos, na Negede Teklemariam, wamefungwa gerezani tangu Septemba 24, 1994, kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi.

Zaidi ya nusu ya waliofungwa wako katika gereza la Meiter, lililoko jangwani kaskazini ya mji mkuu, Asmara. Kuanzia Oktoba 2011 hadi Agosti 2012, wenye mamlaka waliwaadhibu ndugu zetu 25 kwa kuwaweka kwenye jengo la mabati lililokuwa limefukiwa nusu ardhini. Wakati wa majira ya joto, askari wanawatoa nje wafungwa wakati wa mchana ili wasiumizwe na joto. Hata hivyo, hawapati chakula na maji ya kutosha, jambo linalofanya afya yao izorote sana. Inasikitisha kwamba Ndugu Yohannes Haile, mwenye umri wa miaka 68 alikufa Agosti 2012 kwa sababu ya mateso hayo, na Ndugu Misghina Gebretinsae pia alikufa mwaka wa 2011 kwa sababu hiyohiyo.