Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

ENDELEA KUKESHA!

Mfumuko wa Bei Ulimwenguni—Biblia Inasema Nini?

Mfumuko wa Bei Ulimwenguni—Biblia Inasema Nini?

 Msimamizi wa Benki ya Dunia alitoa onyo hili katika ripoti ya Juni 2022: “Uchumi wa ulimwengu uko hatarini tena. Mfumuko wa bei umetokea upesi sana na wakati uleule kiasi cha pesa ambacho watu wanacho kwa ajili ya matumizi kimepungua.”

 Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) linasema kwamba “bei ya mafuta na ya chakula imeongezeka upesi na kuwaathiri zaidi watu katika nchi maskini.”

 Biblia inatusaidia kuelewa kwa nini kuna hali ngumu za kiuchumi, jinsi tunavyoweza kukabiliana nazo, na tumaini lililopo la kupata suluhisho la kudumu.

Kuongezeka kwa bei katika “siku za mwisho”

  •   Biblia inafafanua wakati tumoishi kuwa “siku za mwisho.”​—2 Timotheo 3:1.

  •   Yesu alisema kwamba “mambo yenye kuogopesha,” au matukio yenye kutisha, yangetokea katika siku hizi. (Luka 21:11) Mfumuko wa bei unatokeza hofu. Watu wana wasiwasi kuhusu wakati wao ujao na ikiwa wataweza kuandalia familia yao.

  •   Kitabu cha Ufunuo kilitabiri kwamba bei ya chakula ingeongezeka katika kipindi hiki. “Nikasikia kitu kilichosikika kama sauti. . . . Ilisema, ‘Bei ya kibaba cha ngano au vibaba vitatu vya shayiri itakuwa mshahara wa siku moja.’”​—Ufunuo 6:6, Easy-to-Read Version.

 Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu “siku za mwisho” na unabii wa kitabu cha Ufunuo, ona video yenye kichwa Ulimwengu Umebadilika Tangu Mwaka wa 1914 na usome makala yenye kichwa “Wapanda Farasi Wanne​—Jinsi Wanavyokuhusu.”

Suluhisho la matatizo yote ya kiuchumi

  •   “Watajenga nyumba na kuishi ndani yake, nao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake, wala hawatapanda na watu wengine wale.”​—Isaya 65:21, 22.

  •   “Kutakuwa na nafaka nyingi duniani; itafurika juu ya milima.”​—Zaburi 72:16.

  •   “‘Kwa sababu wale wanaoteswa wanakandamizwa, kwa sababu ya kilio cha uchungu cha maskini, nitainuka na kutenda,’ asema Yehova.”​—Zaburi 12:5. a

 Hivi karibuni Mungu atakomesha hali zisizofaa za kiuchumi, si tu katika nchi moja bali ulimwenguni pote. Ili kuona jinsi atakavyofanya hivyo, soma makala yenye kichwa “Je, Inawezekana Kuwa na Mfumo wa Kiuchumi Wenye Usawa?

 Lakini hata leo, Biblia inaweza kukusaidia kukabiliana na bei zinazoongezeka. Katika njia gani? Ina ushauri unaofaa wa jinsi ya kutumia pesa kwa hekima. (Methali 23:4, 5; Mhubiri 7:12) Ili ujifunze mengi zaidi, soma makala yenye kichwa “Linda Mapato Yako” na “Jinsi ya Kuishi Ukiwa na Pesa Kidogo.”

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.​—Zaburi 83:18.