Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 BIBLIA INABADILI MAISHA

“Walitaja Nijithibitishie Ukweli”

“Walitaja Nijithibitishie Ukweli”
  • MWAKA WA KUZALIWA: 1982
  • NCHI: JAMHURI YA DOMINIKA
  • HISTORIA: ALILELEWA KATIKA KANISA LA MORMON

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa huko Santo Domingo, Jamhuri ya Dominika, nikiwa mtoto wa mwisho kati ya watoto wanne. Wazazi wangu walikuwa na elimu na walitaka watoto wao pia waishi katika mazingira mazuri ya kijamii. Miaka minne kabla sijazaliwa wazazi wangu walikutana na wamishonari wa Kanisa la Mormon. Walipendezwa na jinsi vijana hao walivyokuwa nadhifu, baada ya muda mfupi wazazi wangu waliamua kwamba familia yetu ingekuwa kati ya familia za kwanza kwenye kisiwa hicho kujiunga na Kanisa la Church of Jesus Christ of Latter-day Saints, au Kanisa la Mormon.

Nilipoendelea kukua, nilifurahia kushirikiana na marafiki kanisani na niliheshimu maoni ya kanisa la Mormon kuhusu maisha ya familia na viwango vya maadili. Nilijivunia kuwa Mmormoni na nikajiwekea mradi wa kuwa mmishonari.

Nilipokuwa na umri wa miaka 18, familia yetu ilihamia Marekani ili niendelee na masomo ya chuo. Mwaka mmoja hivi baadaye, tulitembelewa na mjomba na shangazi yangu, ambao ni Mashahidi wa Yehova, walioishi Florida. Walitualika kuhudhuria kusanyiko la Biblia pamoja nao. Nilifurahi kuona kwamba kila mtu alifungua Biblia na kuandika mambo makuu. Hivyo, nikaomba kalamu na karatasi nami pia nikaanza kuandika.

Baada ya kusanyiko hilo, shangazi na mjomba walisema kwa vile nilitaka kuwa mmishonari, wangenisaidia kujifunza Biblia. Niliona wazo hilo lilikuwa zuri kwa sababu wakati huo nilifahamu zaidi Kitabu cha Wamormoni kuliko Biblia.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Tulipokuwa tukizungumzia Biblia kwa simu, sikuzote shangazi na mjomba walinitia moyo nilinganishe imani yangu na mafundisho ya Biblia. Walitaka nijithibitishie ukweli.

Kulikuwa na mambo mengi kuhusu imani ya Wamormoni ambayo nilikubali, lakini kwa kweli sikuwa na hakika  jinsi mafundisho hayo yalivyohusiana na Maandiko. Shangazi alinitumia gazeti Amkeni! la Novemba 8, 1995, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ambalo lilikuwa na makala kadhaa kuhusu imani ya Wamormoni. Nilishangaa kuona kwamba sikujua mafundisho mengi ya Wamormoni. Hilo lilinichochea kuchunguza zaidi kupitia Tovuti rasmi ya Wamormoni ili kuhakikisha ukweli wa mambo yaliyosemwa na Amkeni! Yalikuwa ya kweli, na niliamini zaidi mambo hayo nilipotembelea jumba la makumbusho la Kanisa la Mormon huko Utah.

Sikuzote niliamini kwamba Kitabu cha Wamormoni kinapatana na Biblia. Lakini nilipoanza kusoma Biblia kwa makini, nilitambua tofauti kati ya mafundisho ya Wamormoni na Biblia. Kwa mfano, kwenye Ezekieli 18:4, Biblia inasema kwamba nafsi hufa. Hata hivyo, Kitabu cha Wamormoni, kwenye Alma 42:9, kinasema: “Nafsi haiwezi kamwe kufa.”

Kwa kuongezea tofauti za kimafundisho, nilisumbuliwa pia na mawazo ya kizalendo yaliyofundishwa na Wamormoni. Kwa mfano, Wamormoni hufundishwa kwamba bustani ya Edeni ilikuwa huko Jackson County, Missouri, Marekani. Na manabii wa kanisa hilo husema kwamba “Ufalme wa Mungu utakapotawala, bendera ya Marekani itapepea bila dosari kwenye mlingoti wa uhuru na haki sawa.”

Nilijiuliza jinsi ambavyo nchi nilikozaliwa, au nchi nyinginezo, zingefaidika. Nilianza kuzungumzia jambo hilo jioni moja nilipopigiwa simu na kijana fulani Mmormoni aliyekuwa akizoezwa kuwa mmishonari. Nilimuuliza waziwazi ikiwa angekuwa tayari kupigana dhidi ya Wamormoni wenzake ikiwa nchi yake ingepigana na nchi yao. Nilishangaa alipokubali! Nilifanya utafiti zaidi kuhusu mafundisho na imani yangu na pia nikajadiliana na viongozi wakuu wa Kanisa la Mormon. Niliambiwa kwamba majibu ya maswali yangu yalihusisha mafumbo ambayo siku moja yangetatuliwa kadiri nuru ilivyozidi kuongezeka.

Nikiwa nimekatishwa tamaa na ufafanuzi wao, nilijichunguza kwa undani zaidi na sababu zangu za kutaka kuwa mmishonari Mmormoni. Nilitambua kwamba nilitamani kuwa mmishonari kwa sababu tu nilitaka kuwasaidia watu. Nilivutiwa pia na cheo ambacho ningepata kwa kuwa mmishonari. Lakini sikujua mengi sana kumhusu Mungu. Ingawa nilikuwa nimesoma Biblia mara nyingi, kwa kweli sikuithamini. Sikujua kamwe kusudi la Mungu kuelekea dunia na wanadamu.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Kupitia kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, kati ya mambo mengine, nilijifunza jina la Mungu, kinachotupata tunapokufa, na daraka la Yesu katika kutimiza kusudi la Mungu. Mwishowe nilianza kuielewa Biblia, na nikafurahia kuwaeleza wengine kuhusu kweli nilizokuwa nikijifunza. Sikuzote niliamini kwamba Mungu yuko, lakini sasa ningeweza kuzungumza naye katika sala akiwa Rafiki yangu wa karibu zaidi. Nilibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova tarehe 12 Julai 2004, na miezi sita baadaye nikawa mhudumu wa Kikristo wa wakati wote.

Kwa miaka mitano, nilifanya kazi kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Nilifurahia sana kusaidia kuchapisha Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia ambayo huwasaidia mamilioni ya watu ulimwenguni kote, na ninaendelea kufurahia kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Mungu.