Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Nilijifunza Kujiheshimu na Kuwaheshimu Wanawake

Nilijifunza Kujiheshimu na Kuwaheshimu Wanawake
  • ALIZALIWA: 1960

  • NCHI: UFARANSA

  • HISTORIA: ALIKUWA MRAIBU WA DAWA ZA KULEVYA NA HAKUWAHESHIMU WANAWAKE

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa Mulhouse, kaskazini-mashariki mwa Ufaransa, katika eneo la watu maskini lililojulikana kwa sababu ya vurugu. Ninakumbuka nikiwa mtoto niliona familia mbalimbali katika eneo hilo zikigombana sana. Katika familia yetu wanawake walidharauliwa sana na mara nyingi walikatazwa kushauriana na wanaume. Nilifundishwa kwamba jukumu la mwanamke ni kupika na kutunza wanaume na watoto.

Maisha ya utotoni hayakuwa rahisi. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, baba yangu alikufa kwa sababu ya kunywa pombe kupita kiasi. Miaka mitano baadaye, kaka yangu mkubwa alijinyonga. Mwaka huohuo, nilishuhudia mauaji yaliyosababishwa na ugomvi wa familia na jambo hilo lilinishtua sana. Ndugu zangu walinifundisha jinsi ya kutumia visu na bunduki ili kujilinda. Nikiwa kijana aliyechanganyikiwa, nilianza kunywa pombe na kuchora mwili wangu.

Nilipofikia umri wa miaka 16 nilikunywa bia chupa 10 hadi 15 kwa siku na baada ya muda mfupi nikaanza kutumia dawa za kulevya. Niliuza vyuma chakavu na kujihusisha na wizi ili nipate pesa za matumizi. Nilipofikia umri wa miaka 17 tayari nilikuwa nimetumikia kifungo gerezani. Kwa ujumla, nilihukumiwa mara 18 kutokana na wizi wa kutumia nguvu.

Nilipofikia umri wa miaka 20 hivi, tabia yangu ilikuwa mbaya hata zaidi. Nilikuwa nikivuta misokoto ishirini ya bangi kwa siku na kutumia heroini pamoja na aina nyingine za dawa za kulevya. Mara nyingi, nilikuwa karibu kufa kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya kupita kiasi. Nilipoanza kuuza dawa za kulevya, mara zote nilibeba visu na bunduki ili kujilinda. Siku moja nilijaribu kumpiga risasi mwanaume fulani, hata hivyo, kwa tukio zuri risasi hiyo iligonga kifuniko cha mkanda wake wa kiunoni! Nilipokuwa na umri wa miaka 24, mama yangu alikufa, na jambo hilo lilinikasirisha sana. Watu wengi waliniogopa sana hivi kwamba walipokutana nami njiani walibadili njia. Kwa sababu ya kuwa mgomvi, mara nyingi nilipelekwa kituo cha polisi au hospitali kutibu majeraha.

Nilifunga ndoa nilipokuwa na umri wa miaka 28. Sikumheshimu mke wangu hata kidogo. Nilimtukana na kumpiga. Hatukushirikiana katika jambo lolote. Nilihisi kwamba ilitosha tu kumpa vito vingi nilivyoiba. Siku moja, jambo fulani lisilotarajiwa lilitokea. Mke wangu alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Baada ya kujifunza mara ya kwanza, aliacha kuvuta sigara, alikataa kupokea pesa za wizi na alinirudishia vito nilivyompa. Nilikasirika sana. Nilimkataza kujifunza Biblia na mara nyingine nilimpulizia moshi wa sigara usoni. Isitoshe, nilimdhihaki mbele ya majirani.

Siku moja, kwa sababu ya kulewa kupita kiasi niliichoma moto nyumba yetu. Mke wangu aliniokoa mimi na binti yetu aliyekuwa na umri wa miaka mitano. Pombe ilipoisha mwilini, dhamiri yangu iliniuma sana. Nilihisi kwamba Mungu hangeweza kamwe kunisamehe. Nilikumbuka wakati mmoja ambapo kasisi alisema kwamba waovu watakwenda motoni. Hata daktari wangu wa magonjwa ya akili aliniambia hivi: “Huu ndio mwisho wako! Hauwezi kurekebishwa.”

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Baada ya tukio hilo la moto, tulihamia kwa wazazi wa mke wangu. Mashahidi walipomtembelea mke wangu, niliwauliza hivi, “Mungu anaweza kunisamehe dhambi zangu zote?” Walinionyesha katika Biblia andiko la 1 Wakorintho 6:9-11. Mistari hiyo inataja matendo yanayomchukiza Mungu, kisha inaongezea hivi: “Wengine wenu mlikuwa hivyo.” Maneno hayo yalinihakikishia kwamba ninaweza kubadilika. Kisha Mashahidi walinihakikishia kwamba Mungu ananipenda kwa kunionyesha andiko la 1 Yohana 4:8. Nilichochewa sana hivi kwamba niliwaomba Mashahidi wanifundishe Biblia mara mbili kwa juma, pia nilianza kuhudhuria mikutano yao ya Kikristo. Nilisali kwa Yehova kwa ukawaida.

Mwezi huohuo, niliamua kuacha kutumia dawa za kulevya na pombe. Muda mfupi baadaye, nilianza kupambana na mabadiliko mwilini mwangu. Nilikuwa nikiota ndoto za kutisha, kichwa kiliniuma, misuli ilikakamaa pamoja na hali nyingine zinazompata mtu anayeacha kutumia dawa za kulevya. Hata hivyo, wakati huo pia nilihisi kwamba Yehova alikuwa pamoja nami na alikuwa akiniimarisha. Nilihisi kama mtume Paulo. Kuhusiana na msaada aliopewa na Mungu, Paulo aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:13) Baada ya muda, niliweza kuacha kuvuta sigara.—2 Wakorintho 7:1.

Mbali na kunisaidia maishani, Biblia imeboresha maisha ya familia yetu. Mtazamo wangu kuelekea mke wangu umebadilika. Nilianza kumheshimu hata zaidi na kumwambia maneno kama vile “tafadhali” na “asante.” Isitoshe, nilianza kuwa baba mzuri kwa binti yetu. Baada ya kujifunza Biblia kwa mwaka mmoja, niliiga mfano wa mke wangu kwa kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Nina uhakika kwamba kanuni za Biblia zimeokoa uhai wangu. Hata washiriki wa familia yangu wasio Mashahidi husema kwamba huenda ningekufa kwa sababu ya kutumia dawa za kulevya au ningeuawa.

Maisha ya familia yangu yamebadilishwa kabisa na mafundisho ya Biblia yanayotaja majukumu yangu nikiwa mume na baba. (Waefeso 5:25; 6:4) Tulianza kufanya mambo pamoja tukiwa familia. Sasa, badala ya kumwachia mke wangu kazi zote za jikoni ninafurahia kumsaidia ili atimize vizuri jukumu lake akiwa mhubiri wa wakati wote. Naye hufurahia kunisaidia ili nitimize vizuri mgawo wangu nikiwa mzee wa kutaniko.

Nimejionea rehema na upendo wa Yehova Mungu maishani mwangu. Nina hamu kubwa ya kuzungumza kuhusu sifa za Mungu ninapokutana na watu wanaoonekana kwamba hawawezi kubadilika kwa kuwa mwanzoni watu wengi waliniona hivyo. Ninajua kwamba Biblia ina nguvu za kumsaidia mtu yeyote kuwa na maisha bora na yenye kusudi. Biblia imenisaidia kujiheshimu, kuwapenda na kuwaheshimu watu wote, wanaume kwa wanawake.