Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

2 Mungu Hajali—Je, Ni Kweli?

2 Mungu Hajali—Je, Ni Kweli?

2 Mungu Hajali​—Je, Ni Kweli?

Jambo ambalo huenda umesikia: “Ikiwa kwa kweli Mungu anawajali wanadamu, basi anapaswa kuondoa uovu na mateso ulimwenguni. Na hata kama anawajali wanadamu kwa ujumla, hanijali mimi binafsi.”

Biblia inafundisha nini?: Yehova Mungu hasababishi uovu wala kuteseka. (Yakobo 1:13) Ingawa anaweza kuondoa mambo hayo wakati wowote, anaruhusu watu wapotovu waendelee kuishi ili asuluhishe masuala ambayo yalizushwa mwanzoni mwa historia ya mwanadamu kuhusu uaminifu na utawala. Mwishowe, atachukua hatua ili kuwasaidia wanadamu na kuondoa matatizo yote yanayosababishwa na wale wanaokataa utawala wake.—Mwanzo 3:1-6; Isaya 65:17. *

Ingawa Mungu anawajali wanadamu kwa ujumla, anampenda sana kila mmoja wetu. Andiko la Mathayo 10:29-31 linaonyesha kwamba anaona mambo mengi madogo-madogo kutuhusu ambayo hata sisi wenyewe hatuyajui: “Je, shomoro wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiogope: Ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.”

Jinsi kujua ukweli kunavyokusaidia: Kwa kawaida sisi huwaepuka watu ambao ni wakali au wasiojali. Si ajabu kwamba uwongo kuwa Mungu hajali huwafanya watu wengi wasitake kumjua hata kidogo au wasali kwake tu wakati wanaposhindwa kutatua matatizo yao. Ukijua kwamba Yehova Mungu anakujali kikweli, utataka kujifunza mengi zaidi kumhusu na kusitawisha urafiki pamoja naye.

Kwa mfano, huenda ulisali kwa Mungu lakini ukawa na shaka kama anakusikiliza au kama atakujibu. Biblia inatuhakikishia kwamba nyakati zote “msikiaji wa sala” huwasikiliza wote wanaozungumza naye kwa unyofu.—Zaburi 65:2.

Mungu anataka ‘umtupie mahangaiko yako yote, kwa sababu yeye anakujali.’ (1 Petro 5:7) Tunaweza kumtegemea nyakati za taabu kubwa kwa sababu Neno lake linasema: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zaburi 34:18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kwa habari zaidi kuhusu sababu zinazofanya Mungu aruhusu wanadamu wateseke, ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

[Blabu katika ukurasa wa 5]

Ikiwa Mungu hajali, kwa nini anatuambia tusali kwake?