Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ataacha Umpate”

“Ataacha Umpate”

Mkaribie Mungu

“Ataacha Umpate”

1 MAMBO YA NYAKATI 28:9

JE, UNAMJUA Mungu? Kujibu swali hilo si rahisi kama inavyoonekana. Kwa kweli, kumjua Mungu kunamaanisha kufahamu kikamili mapenzi yake na njia zake. Hivyo, tunasitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye ambao unakuwa na uvutano mkubwa katika maisha yetu yote. Je, inawezekana kweli kuwa na uhusiano kama huo? Ikiwa ndivyo, tunaweza kuusitawisha jinsi gani? Tunaweza kupata majibu katika shauri la Mfalme Daudi kwa mwana wake Sulemani, linalopatikana kwenye 1 Mambo ya Nyakati 28:9.

Fikiria hali ilivyo. Daudi ametawala Israeli kwa miaka 40 hivi, na taifa limesitawi sana chini ya utawala wake. Sulemani, ambaye karibuni atarithi utawala huo, ni kijana tu. (1 Mambo ya Nyakati 29:1) Anapokaribia kufa, Daudi anampa mwana wake shauri gani?

Akikumbuka mambo mengi aliyokuwa amejionea katika kumtumikia Mungu, Daudi anaanza kwa kusema hivi: “Sulemani mwanangu, mjue Mungu wa baba yako.” Bila shaka, Daudi anamaanisha mengi zaidi ya kujua mambo fulani tu kumhusu Mungu. Tayari Sulemani ni mwabudu wa Yehova, Mungu wa Daudi. Sehemu fulani ya Maandiko ya Kiebrania tayari imeandikwa, na bila shaka Sulemani anajua yale ambayo maandiko hayo matakatifu yanasema kumhusu Mungu. Msomi mmoja anasema kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “-jua” linaweza kumaanisha “kujua kwa undani kabisa.” Ndiyo, Daudi anataka mwana wake asitawishe kitu ambacho yeye mwenyewe anakithamini sana—uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.

Uhusiano huo wa karibu unapaswa kuwa na uvutano mkubwa katika mtazamo na maisha ya Sulemani. Daudi anamhimiza mwana wake hivi: “Mtumikie [Mungu] kwa moyo kamili na kwa nafsi yenye shangwe.” * Ona kwamba anamwagiza amtumikie Mungu baada ya kumhimiza amjue. Kwa kweli, kumjua Mungu kunatusukuma tumtumikie. Lakini Mungu hatumikiwi kwa moyo nusunusu wala kwa moyo wa unafiki. (Zaburi 12:2; 119:113) Daudi anamsihi mwana wake amtumikie Mungu kwa moyo wote na kwa kupenda.

Kwa nini Daudi anamhimiza mwana wake amwabudu Mungu kwa nia na mtazamo unaofaa? Daudi anaeleza: “Kwa maana Yehova anaichunguza mioyo yote, naye anatambua kila mwelekeo wa fikira.” Sulemani hapaswi kumtumikia Mungu ili tu ampendeze baba yake, Daudi. Mungu anawatafuta watu ambao wanataka kumtumikia kwa moyo wa kupenda.

Je, Sulemani atafuata mfano wa baba yake na kumkaribia Mungu? Uamuzi ni wake. Daudi anamwambia hivi mwana wake: “Ukimtafuta, ataacha umpate; lakini ukimwacha, atakutupa mbali milele.” Ili kuwa mwabudu mwenye uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, lazima Sulemani ajitahidi sana kumjua. *

Shauri la Daudi lililo kama la baba linatuhakikishia kwamba Yehova anataka tuwe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Hata hivyo, ili tusitawishe uhusiano huo, tunahitaji ‘kumtafuta,’ huku tukiyachunguza Maandiko kwa bidii tukiwa na lengo la kumjua kwa undani. Ujuzi wetu kumhusu unapaswa kutusukuma tumtumikie kwa moyo wote na kwa kupenda. Yehova anatamani—na anastahili—kutumikiwa kwa njia hiyo na waabudu wake.—Mathayo 22:37.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika Biblia fulani mstari huo umetafsiriwa hivi: “Mtumikie kwa moyo wote na kwa nia ya kupenda.”

^ fu. 6 Inasikitisha kwamba ingawa Sulemani alianza kumtumikia Mungu kwa moyo kamili, hakuendelea kuwa mwaminifu.—1 Wafalme 11:4.