Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dini Zote Ni Nzuri?

Je, Dini Zote Ni Nzuri?

Je, Dini Zote Ni Nzuri?

TUNAISHI katika ulimwengu ambao umejaa dini tofauti-tofauti. Uchunguzi mmoja wa hivi karibuni ulionyesha kwamba ulimwenguni pote kuna dini 19 kubwa na dini ndogo-ndogo 10,000 hivi. Kuwapo kwa dini nyingi hivyo, kunawapa watu uhuru mwingi wa kuchagua dini kuliko wakati mwingine wowote. Hivyo basi, je, unaweza kujiunga na dini yoyote ile bila kujali?

Watu fulani wanasema kwamba dini mbalimbali ni kama njia tofauti zinazoelekea juu ya mlima. Watu hao hawajali sana kuhusu njia wanayochagua, kwa kuwa njia zote zinaelekea mahali palepale. Wanasema kwamba kuna Mungu mmoja tu Mweza-Yote, kwa hiyo, lazima dini zote ziwe zinawaongoza watu kwake.

Je, Njia Zote Zinaongoza kwa Mungu?

Yesu Kristo, mmoja wa walimu wa dini wanaoheshimiwa sana katika historia, alisema nini kuhusu jambo hilo? “Ingieni kwa kupitia mlango mwembamba,” akawaambia wanafunzi wake. Kwa nini? “Kwa maana njia inayoongoza kwenye maangamizi ni pana, na mlango wa kuingilia humo ni mpana; waendao njia hiyo ni wengi. Lakini njia inayoongoza kwenye uhai ni nyembamba, na mlango wa kuingilia humo ni mwembamba; ni watu wachache tu wanaoweza kuigundua njia hiyo.”—Mathayo 7:13, 14, Biblia Habari Njema.

Je, kwa kweli Yesu alikuwa akisema kwamba dini fulani zinaongoza kwenye “maangamizi”? Au je, alikuwa akifundisha kwamba ni watu tu wasiomwamini Mungu ndio walio kwenye ile njia pana, lakini wale wanaomwamini Mungu, bila kujali wao ni wa dini gani, wako kwenye njia nyembamba inayoongoza kwenye uhai?

Mara tu baada ya kutaja kwamba kuna njia mbili peke yake, Yesu alisema hivi: “Jihadharini na manabii wa uongo. Wao huja kwenu wakionekana kama kondoo kwa nje, lakini kwa ndani ni mbwa mwitu wakali.” (Mathayo 7:15, BHN) Baadaye alisema: “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.” (Mathayo 7:21, Union Version) Ikiwa mtu anaitwa nabii au anadai kwamba Yesu ni “Bwana” wake, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba yeye ni mtu wa dini, yeye si mtu asiyemwamini Mungu. Basi, ni wazi kuwa Yesu alikuwa akionya kwamba kuna dini ambazo si nzuri na kwamba kuna viongozi wa kidini ambao hatupaswi kuwaamini.

Je, Tunaweza Kuitambua Ile Njia Nyembamba?

Kwa kuwa si njia zote zinazoongoza kwa Mungu, unaweza kupata jinsi gani ile njia nyembamba inayoongoza kwenye uzima kati ya maelfu ya dini zilizopo? Hebu fikiria mfano huu: Wazia kwamba umepotea katika jiji kubwa. Unaamua kuomba msaada. Mtu mmoja anakwambia kwa uhakika uende upande wa mashariki. Mwingine anakuhimiza uende upande wa magharibi. Naye mwingine anapendekeza kwamba uchague upande wowote unaoona kuwa ni sawa kwako. Mwishowe, msafiri fulani anatoa ramani inayotegemeka na kukuonyesha njia inayofaa. Kisha anakupa ramani hiyo ili uitumie unapoendelea na safari. Je, si kweli kwamba utakuwa na uhakika zaidi wa kufika mahali unapokwenda?

Vivyo hivyo, inapohusu kuchagua dini inayofaa, tunahitaji ramani ya kiroho inayotegemeka. Je, kuna ramani kama hiyo? Ndiyo, ipo. Ramani hiyo ni Biblia, nayo inasema hivi: “Maandiko yote Matakatifu yameandikwa kwa uongozi wa Mungu, na yanafaa katika kufundishia ukweli, kuonya, kusahihisha makosa, na kuwaongoza watu waishi maisha adili.”—2 Timotheo 3:16, BHN.

Inaelekea kwamba unaweza kupata tafsiri ya Biblia katika lugha yako ambayo unaweza kutumia kama ramani ya kiroho. Wachapishaji wa gazeti hili, Mashahidi wa Yehova, wanachapisha tafsiri ya Biblia inayotegemeka ambayo inaitwa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Hata hivyo, ikiwa wewe si Shahidi wa Yehova, huenda utapenda kutumia tafsiri nyingine unapochunguza jinsi unavyoweza kuitambua dini nzuri na dini mbaya. Hivyo basi, habari zinazofuata zinataja tafsiri mbalimbali za Biblia ambazo zinaheshimiwa sana na dini nyingine.

Unaposoma habari hizo, linganisha mambo unayojua na yale ambayo Biblia inasema. Kumbuka maneno ya Yesu kuhusu jinsi tunavyoweza kutofautisha dini nzuri na dini mbaya. Alisema hivi: “Mti mzuri huzaa matunda mazuri, na mti mbaya huzaa matunda mabaya. Mti mzuri hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mbaya hauwezi kuzaa matunda mazuri.” (Mathayo 7:17, 18, BHN) Basi, chunguza matunda matatu tu kati ya matunda mazuri ambayo Biblia inasema yangeutambulisha ule “mti mzuri.”

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Biblia ni kama ramani inayotegemeka inayoweza kumsaidia mtu kupata dini inayofaa