Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maji Yanayobubujika Ili Kutokeza Uzima wa Milele

Maji Yanayobubujika Ili Kutokeza Uzima wa Milele

Maji Yanayobubujika Ili Kutokeza Uzima wa Milele

“Yule atakayekunywa maji ambayo nitampa hatapatwa na kiu hata kidogo, lakini maji ambayo nitampa yatakuwa chemchemi ya maji ndani yake, inayobubujika ili kutokeza uzima wa milele.”—YOHANA 4:14.

“KWA ghafula, nyuma ya mwezi, . . . kito cha bluu kinachong’aa kinatokea, tufe la bluu lililofunikwa kwa ushungi mweupe, linainuka polepole kama lulu ndogo katika giza zito lisiloeleweka.”—Mwanaanga, Edgar Mitchell, akieleza jinsi dunia inavyoonekana kutoka angani.

Ni nini kinachoipa sayari yetu rangi hiyo maridadi ambayo ilimsukuma mwanaanga huyo kuifafanua kishairi? Ni maji yanayofunika karibu robo tatu za dunia. Kwa kweli, maji hayafanyi tu sayari yetu iwe maridadi bali pia yanasaidia kuendeleza uhai wa viumbe. Kwa hakika, maji yanafanyiza asilimia 65 hivi ya mwili wa mwanadamu. Hivyo, kitabu kimoja (Encyclopædia Britannica) kinasema hivi kuhusu maji: “Ni muhimu kwa uhai, yanahusika katika karibu kila utendaji katika mimea na wanyama.”

Kwa sababu ya mfumo bora wa kusafisha maji, kiasi cha maji duniani hakihitaji kuongezwa. “Karibu kila tone la maji tunalotumia hurudi baharini,” chaeleza kitabu kimoja (The World Book Encyclopedia). “Matone hayo yakiisha kufika baharini yanavukizwa na jua. Kisha yanaanguka tena duniani yakiwa mvua. Maji yanatumiwa na kutumiwa tena na tena. Hayaishi.” Miaka 3,000 hivi iliyopita, mzunguko huo wa ajabu ulifafanuliwa katika Biblia: “Mito yote ya wakati wa majira ya baridi kali inaenda baharini, hata hivyo bahari haijai. Mahali inapoenda mito hiyo ya majira ya baridi kali, hapo ndipo inarudi ili iende tena.” Mzunguko wa maji ni uumbaji wa ajabu kama nini!—Mhubiri 1:7.

Tunapofikiria umuhimu wa maji kwa uhai na mfumo wa ajabu wa kuandaa maji, hatupaswi kushangaa kugundua kwamba maji yanatajwa zaidi ya mara 700 katika Biblia. Mara nyingi Biblia inatumia uwezo mbalimbali wa pekee wa maji kuonyesha jinsi Biblia inavyoweza kusafisha na kuendeleza hali yetu ya kiroho.—Isaya 58:11; Yohana 4:14.

Uwezo wa Biblia wa Kusafisha

Waisraeli walijulikana kuwa watu safi sana kimwili kwa sababu kwa ukawaida walioga na kujisafisha kwa maji. Kulikuwa na desturi ya kuosha miguu kwa maji mtu alipokuwa akiingia ndani ya nyumba kwa ajili ya mlo. (Luka 7:44) Zaidi ya kusafisha miili na vitu vyao, Waisraeli walitumia maji kwa ajili ya usafi wa kisherehe. Makuhani waliotumika katika maskani au hema la mkutano walipaswa kuoga na kuosha mavazi yao mara nyingi. (Kutoka 30:18-21) Baadaye, katika hekalu huko Yerusalemu, Sulemani alitengeneza “bahari ya kuyeyushwa” ya shaba ambayo kwa kawaida ilikuwa na zaidi ya lita 44,000 za maji, kiasi cha maji ya kutosha kutimiza matakwa yote ya usafi ya Sheria ya Mungu. (2 Mambo ya Nyakati 4:2, 6) Matumizi hayo ya maji yanawahusu Wakristo jinsi gani leo?

Mtume Paulo alieleza kwamba Yesu alikuwa amelisafisha kutaniko la Kikristo na “kuliosha kwa maji kwa njia ya neno.” Kama maji yanavyosafisha kimwili, kweli ya Neno la Mungu ina uwezo wa kusafisha kiadili na kiroho. Kusafishwa huko kunawafanya wanafunzi wa Kristo wawe ‘watakatifu na bila dosari.’ (Waefeso 5:25-27) Hivyo, wote wanaotaka kupata kibali cha Mungu wanapaswa kujitahidi kuwa “bila doa na bila dosari” kiadili na kiroho. (2 Petro 3:11, 14) Neno la Mungu linawasaidia jinsi gani kufanya hivyo?

Wale wanaotaka kumpendeza Yehova Mungu wanakunywa maji ya kiroho kwa kujifunza Biblia kwa ukawaida. Ujuzi wanaopata unapogusa akili na mioyo yao, unawafanya wawe na tamaa kubwa ya kutii agizo hili la Biblia: “Mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Waroma 12:2.

Ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu unawawezesha watu kama hao kutambua kasoro na madoa katika mwenendo wao na kufikiri kwao. Kadiri wanavyotumia kanuni za Biblia maishani mwao, ndivyo Neno la Mungu, kama maji, linavyosaidia ‘kuwaosha’ hata kutokana na dhambi nzito.—1 Wakorintho 6:9-11.

Hivi ndivyo kijana mmoja huko Hispania alivyogeuzwa. Alfonso anaeleza hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka 18, maisha yangu hayakunifurahisha.” Alikuwa mraibu wa dawa za kulevya na mhalifu sugu. “Nilijihisi mchafu kwa sababu ya jinsi nilivyoutendea mwili wangu na kuwatendea wengine.

“Shuleni, nilimwona msichana fulani wa rika langu aliyekuwa safi na asiye na hila, jambo lililomfanya awe tofauti kabisa na wanafunzi wengine. Mfano wake ulinifanya nitamani kuishi maisha safi kama yake. Alipendekeza nihudhurie mkutano wa Mashahidi wa Yehova, nami nikahudhuria. Muda si muda nilianza kujifunza Biblia na kusitawisha urafiki pamoja na Mungu. Katika kipindi cha mwaka mmoja, nilisafisha maisha yangu, nikabatizwa na kuwa Shahidi. Mabadiliko hayo makubwa yaliwachochea wazazi wengi katika ujirani wetu kunijia na kuniomba niwasaidie vijana wao waliokuwa waraibu wa dawa za kulevya.”

Maji Yanayotokeza Uzima wa Milele

Pindi moja Yesu alimwambia mwanamke Msamaria aliyekuwa akiteka maji katika kisima cha Yakobo kuhusu “maji yaliyo hai.” Alisema hivi: “Yule atakayekunywa maji ambayo nitampa hatapatwa na kiu hata kidogo, lakini maji ambayo nitampa yatakuwa chemchemi ya maji ndani yake, inayobubujika ili kutokeza uzima wa milele.” (Yohana 4:10, 14) Maneno ya Yesu yalionyesha kwamba “maji yaliyo hai” yanawakilisha maandalizi ya Mungu kwa ajili ya uzima kama yanavyofafanuliwa katika Neno lake, Biblia. Yanawawezesha wanadamu kuishi milele. Sehemu muhimu ya maji hayo ya ufananisho ni dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu. “Mungu aliupenda ulimwengu sana,” akaeleza Yesu, “hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

Alfonso, aliyetajwa mapema, amekuja kuthamini sana “maji yaliyo hai” yanayotoka kwa Mungu. Akizungumza kuwahusu wale walioendelea kuishi maisha ya uhalifu na kutumia dawa za kulevya, Alfonso anasema hivi: “Ndugu yangu wa kimwili amekufa, na pia marafiki wangu wote wa zamani. Ujuzi wa Neno la Mungu ulinisaidia kuepuka matokeo hayo mabaya. Niko hai leo kwa sababu ya maandalizi ya kiroho ya Yehova.” Zaidi ya hayo, kwa sababu ya yale ambayo Alfonso amejifunza kutoka kwa Neno la Mungu, anatazamia kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa.—2 Petro 3:13.

Wote Wanaalikwa

Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, kuna ufafanuzi kuhusu “mto wa maji ya uzima, mwangavu kama fuwele, ukitiririka kutoka katika kiti cha ufalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 22:1) Mto huo unawakilisha maandalizi ya Mungu ambayo hatimaye yatawawezesha wanadamu kuwa wakamilifu kama Adamu na Hawa walivyokuwa mwanzoni mwa historia ya wanadamu.

Baada ya kuufafanua mto huo, simulizi hilo linatoa mwaliko huu: “Na yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.” (Ufunuo 22:17) Leo, mwaliko huo unatolewa duniani pote. Kila mwaka, Mashahidi wa Yehova katika nchi zaidi ya 235 wanatumia zaidi ya saa bilioni moja kuwasaidia watu watwae ujuzi wa Biblia unaoleta uzima.

Je, una kiu ya maji ya uzima? Kwa kunywa maji hayo safi kabisa, yaani, kwa kujifunza na kutumia maandalizi kutoka kwa Muumba wetu, wewe pia unaweza kuwa miongoni mwa wale ambao ‘wanajiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.’—1 Timotheo 6:19.

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Kama maji yanavyosafisha kimwili, kweli ya Biblia ina uwezo wa kusafisha kiadili na kiroho

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

VYANZO VYA MAJI KATIKA NYAKATI ZA BIBLIA

Katika nyakati za Biblia, watu walijitahidi juu chini kupata vyanzo vya maji vyenye kutegemeka. Abrahamu na Isaka walichimba visima karibu na Beer-sheba ili kuandalia jamaa zao na mifugo yao maji ya kutosha.—Mwanzo 21:30, 31; 26:18.

Visima visivyo na kina vilikauka katika majira marefu ya kiangazi. Kisima kilihitaji kuwa na kina kirefu ili kiwe na maji daima. (Methali 20:5) Kina cha kisima kimoja huko Lakishi ni mita 44. Kisima kingine, kilicho Gibeoni, kina kina cha mita 25 hivi na upana wa mita 11 hivi. Kuchimba kisima hicho kulihusisha kuondoa tani 3,000 za miamba. Yule mwanamke Msamaria aliyeenda kuteka maji katika kisima cha Yakobo alimwambia Yesu hivi: “Kisima ni kirefu.” Labda kiwango cha maji katika eneo hilo kilikuwa mita 23 chini ya ardhi.—Yohana 4:11.

Hapo kale matangi yalikuwa vyanzo vingine vya maji huko Mashariki ya Kati. Kuanzia Oktoba (Mwezi wa 10) mpaka Aprili (Mwezi wa 4), maji ya mvua yalikusanywa katika matangi hayo yaliyochimbwa ardhini. Mitaro ilichimbwa kando ya vilima ili kuyaelekeza maji ya mvua ndani ya matangi hayo. Waisraeli walichimba matangi makubwa ili kuhifadhi maji.—2 Mambo ya Nyakati 26:10.

Kazi ya kuteka maji kutoka katika visima na matangi ilikuwa ngumu, na ndivyo ilivyo leo. Wanawake kama Rebeka na binti za Yethro walitimiza wajibu muhimu sana kwa kuteka maji kila siku kwa ajili ya familia zao na mifugo yao.—Mwanzo 24:15-20; Kutoka 2:16.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Alfonso leo, akihubiri Neno la Mungu