Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nitaketi na Kukisoma Kando ya Moto Leo Usiku”

“Nitaketi na Kukisoma Kando ya Moto Leo Usiku”

Barua Kutoka Australia

“Nitaketi na Kukisoma Kando ya Moto Leo Usiku”

MANENO Australia vijijini yanamfanya mtu afikirie jangwa kavu, joto jingi, na maeneo makubwa yasiyo na kitu. Lakini maeneo hayo ya vijijini ni makao ya watu 180,000 hivi, karibu asilimia moja ya idadi ya watu katika taifa hilo.

Nilipokuwa mchanga, wazazi wangu ambao walikuwa Mashahidi wa Yehova, walinipeleka huko ili kuhubiri. Ukubwa wa maeneo hayo na umaridadi wake ulichochea fikira zangu. Pia niliwapenda wakaaji wa maeneo hayo, ambao ni wenye nguvu na wapole. Sasa nikiwa na familia yangu ndogo, nilitaka mke wangu na watoto wetu wawili, wenye umri wa miaka 10 na 12, wajionee mambo niliyojionea.

Kupanga Safari

Kwanza, tuliketi na kuhesabu gharama. Tulikuwa na pesa za kutuwezesha kusafiri mbali kadiri gani? Tungeweza kukaa huko kwa muda gani? Wenzi fulani wa ndoa na pia wahudumu wawili wa wakati wote katika kutaniko letu walijitolea kuungana nasi. Tulikubaliana kufunga safari wakati ambapo shule zingefungwa katikati ya mwaka. Kisha tukaiandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Australia huko Sydney ili kuomba eneo. Tuliambiwa tuhubiri eneo la mbali karibu na Goondiwindi, mji mdogo wa vijijini ulio kilomita 400 hivi kutoka Brisbane, tunakoishi.

Tulipata habari kwamba kuna kutaniko dogo la Mashahidi wa Yehova huko Goondiwindi. Hiyo ilikuwa baraka nyingine. Kukutana na wanaume na wanawake Wakristo kungekuwa jambo la pekee sana katika safari yetu. Tuliwasiliana na kutaniko hilo na kuwajulisha kwamba tungewatembelea. Itikio lao changamfu lilituonyesha kwamba wanatutazamia kwa hamu.

Muda mfupi kabla hatujafunga safari yetu, kikundi chetu kilikutana ili kuzungumzia jinsi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu katika maeneo ya vijijini. Tulitaka hasa kuheshimu tamaduni na desturi za Wenyeji wa Asili wa Australia ambao tungekutana nao. Kwa mfano, makabila fulani yanaona mashamba yao kuwa makao ya jamii yao. Lingekuwa kosa kuingia katika eneo lao bila kukaribishwa.

Kuingia Vijijini

Hatimaye, siku hiyo ya maana sana ikafika. Magari yetu mawili, yakiwa yamejaa kabisa watu na vitu, yalielekea vijijini. Tulipita mashamba yaliyolimwa kisha nchi tambarare zenye nyasi na mikalitusi. Jua jangavu liling’aa katika anga lisilo na mawingu. Saa kadhaa baadaye, tukafika Goondiwindi na kupumzika usiku huo katika nyumba tulizokodi katika kambi fulani.

Siku iliyofuata, Jumapili (Siku ya Yenga), ilipopambazuka jua liling’aa na hewa ilikuwa safi—hali ya hewa ilifaa sana kazi ya kuhubiri. Kwa kawaida, kiwango cha joto katika majira ya kiangazi kinapanda kuzidi nyuzi 40 Selsiasi! Eneo la kwanza tulilotembelea ni la jamii fulani ya Wenyeji wa Asili wa Australia lililo umbali wa kilomita 30 hivi. Tulielekezwa kwa Jenny, mwanamke mzee, aliye na mvi ambaye alikuwa kiongozi wa jamii hiyo. Alisikiliza kwa makini ujumbe wetu wa Kimaandiko na kwa furaha akachukua kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. * Kisha akatukaribisha tuingie katika eneo hilo na kuwahubiria wakaaji.

Watoto wenyeji walikimbia na kuwajulisha watu kuhusu ziara yetu. Kila mwenye nyumba tuliyempata alisikiliza ujumbe wetu kwa heshima na kukubali vichapo vya Biblia. Muda si muda vichapo vyetu vikaisha, na huo ukawa wakati wa kurudi mjini kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. Kabla hatujaondoka, tuliahidi kurudi ili kuwatembelea wale ambao hatukuwakuta.

Alasiri hiyo, Jumba la Ufalme lilijaa watu wenye furaha waliokutana, wakazungumza, na upesi wakawa marafiki. Mashahidi 25 wa Yehova katika kutaniko hilo wamekuwa wakiwapelekea watu 11,000 hivi ujumbe wa Ufalme katika eneo hilo la vijijini lenye ukubwa wa kilomita 30,000 za mraba. Shahidi mmoja aliyethamini alisema hivi: “Asanteni kwa kujitahidi kuja kutusaidia.” Baada ya mkutano wenye kuchangamsha, sote tulienda kupata viburudisho. Kabla ya kulala usiku huo, tuliwalisha wanyama wanaoitwa possum waliokuwa wakizurura katika kambi yetu.

“Kando ya Moto Leo Usiku”

Katika siku mbili zilizofuata, kikundi chetu kilitembelea baadhi ya nyumba zilizo katika eneo la mbali kandokando ya mpaka wa Queensland na New South Wales. Eneo hilo la vijijini lina mikalitusi iliyokauka na nchi tambarare zenye nyasi ambako kondoo na ng’ombe wanalisha. Njiani, tuliona kangaruu kadhaa waliotega masikio yao walipotuona. Emu wa kifahari walitembea kwa madaha kwenye uwanja wa farasi.

Jumanne (Siku ya 2) alasiri, tulikutana na kundi kubwa la ng’ombe wakitembea polepole barabarani. Kwa muda mrefu, wafanyakazi wa kulipwa wamekuwa wakilisha mifugo katika eneo hili, hasa wakati wa ukame. Muda si muda tulikutana na mfanyakazi mmoja akiwa amepanda farasi. Niliegesha gari kando ya barabara, nikashuka na kumsalimu kwa sauti. Alijibu, “Sijambo mwenzangu.” Mwanamume huyo mzee, pamoja na mbwa wake, walisimama ili tuzungumze.

Baada ya kuzungumza kwa muda juu ya ukame, nilianza kuuzungumzia ujumbe wetu. “Sijawahi kusikia chochote kutoka katika Biblia tangu utotoni!” mwanamume huyo akasema kwa mshangao. Aliwalaumu viongozi wa kidini kwa kusababisha kuzorota kwa maadili ulimwenguni. Lakini, bado aliiheshimu Biblia. Baada ya mazungumzo mazuri ya Kimaandiko, nilimpa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? * Alikishika kwa nguvu, akakiingiza katika mfuko wa shati lake, na kusema, “Ikiwa kitaniambia yale ambayo Biblia inafundisha, nitaketi na kukisoma kando ya moto leo usiku.”

Kurudi Nyumbani

Usiku huo katika Jumba la Ufalme, tuliwasimulia ndugu na dada zetu wa kiroho mambo tuliyoona. Waliahidi kuwarudia watu waliopendezwa tuliokutana nao. Mikutano ilipokwisha, ilikuwa vigumu kusema kwaheri. Tulipendana sana. Sote tulihisi tumeimarishwa na ubadilishanaji wa kitia-moyo cha kiroho.—Waroma 1:12.

Siku iliyofuata tulifunga safari kurudi nyumbani. Tukifikiria safari yetu, tunakubali kwamba Yehova alibariki sana jitihada zetu. Tulihisi tumeburudishwa kiroho. Tulipofika nyumbani, niliwauliza watoto wetu hivi: “Mngependa twende wapi likizo wakati ujao? Je, twende milimani?” Wakajibu “Hapana Baba, twende tukahubiri tena vijijini.” Mke wangu akaongezea: “Naam, twende. Hiyo ndiyo iliyokuwa likizo bora zaidi!”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 17 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.