Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unabii Kuhusu Wachungaji Saba na Watawala Wadogo Wanane Unatuhusuje Leo?

Unabii Kuhusu Wachungaji Saba na Watawala Wadogo Wanane Unatuhusuje Leo?

“Tutasimamisha juu yake wachungaji saba, ndiyo, watawala wadogo wanane kutoka kati ya wanadamu.”MIKA 5:5.

1. Kwa nini njama ya Siria na Israeli haingefanikiwa?

KATI ya mwaka wa 762 K.W.K. na 759 K.W.K., mfalme wa Israeli na mfalme wa Siria walitangaza vita dhidi ya ufalme wa Yuda. Kwa nini? Walitaka kuvamia Yerusalemu, kumwondoa Mfalme Ahazi na kumweka mtu mwingine ambaye labda hakuwa mzao wa Mfalme Daudi. (Isa. 7:5, 6) Mfalme wa Israeli alifanya hivyo ingawa alijua Yehova alisema kwamba mzao wa Mfalme Daudi angeketi kwenye kiti Chake cha ufalme milele, na neno la Mungu halikosi kamwe kutimia.Yos. 23:14; 2 Sam. 7:16.

2-4. Eleza jinsi andiko la Isaya 7:14 na 16 lilivyotimizwa (a) katika karne ya nane K.W.K. (b) katika karne ya kwanza W.K.

2 Mwanzoni, ilionekana kwamba Siria na Israeli zingeushinda ufalme wa Yuda. Katika pambano moja tu, mashujaa 120,000 wa Ahazi waliuawa! Maaseya, “mwana wa mfalme,” aliuawa pia. (2 Nya. 28:6, 7) Hata hivyo, Yehova alikuwa akitazama. Alikumbuka ahadi aliyompa Daudi; hivyo, akamtuma nabii Isaya apeleke ujumbe wenye kutia moyo sana.

3 Isaya alisema hivi: “Tazama! Mwanamwali kwa kweli atapata mimba, naye atazaa mwana, naye hakika atamwita jina lake Imanueli. . . . Kabla ya mvulana huyo kujua jinsi ya kukataa lililo baya na kuchagua lililo jema, nchi ya wale wafalme wawili mnaowahofu [Siria na Israeli] na kuchukizwa kwa sababu yao itaachwa kabisa.” (Isa. 7:14, 16) Kwa kweli sehemu ya kwanza ya unabii huo inahusu kuzaliwa kwa Masihi. (Mt. 1:23) Hata hivyo, kwa kuwa ‘wafalme hao wawili,’ yaani, mfalme wa Siria na mfalme wa Israeli hawakuwa tena tishio kwa taifa la Yuda katika karne ya kwanza W.K., bila shaka unabii kuhusu Imanueli ulitimizwa kwa mara ya kwanza katika siku za Isaya.

 4 Muda mfupi baada ya Isaya kutoa tangazo hilo muhimu, mke wake alipata mimba na kuzaa mwana aliyeitwa Maher-shalal-hash-bazi. Inawezekana kwamba mwana huyo ndiye “Imanueli” aliyetajwa na Isaya. * Katika nyakati za Biblia, mtoto mchanga alipewa jina moja alipozaliwa. Labda jina hilo liliwakumbusha tukio fulani la pekee, lakini wazazi na watu wake wa ukoo walimpa jina lingine. (2 Sam. 12:24, 25) Hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba Yesu aliitwa Imanueli.Soma Isaya 7:14; 8:3, 4.

5. Mfalme Ahazi alifanya uamuzi gani wa kipumbavu?

5 Mataifa ya Israeli na Siria yalipokuwa yakikazia fikira jiji la Yuda, taifa lingine la kijeshi liliazimia kunyakua eneo hilo. Taifa hilo lilikuwa serikali kuu ya ulimwengu ya Ashuru iliyokuwa ikienea kwa kasi. Kulingana na Isaya 8:3 na 4, Ashuru lingechukulia mbali “mali za Damasko” na “nyara za Samaria” kabla ya kushambulia ufalme wa kusini wa Yuda. Badala ya kutegemea neno la Mungu lililosemwa kupitia Isaya, Ahazi asiye na imani alifanya na Ashuru mkataba ulioleta msiba. Mkataba huo ulifanya Yuda likandamizwe na Ashuru. (2 Fal. 16:7-10) Ahazi alikuwa mchungaji wa taifa la Yuda aliyeshindwa kutimiza daraka lake! Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Ninapofanya maamuzi muhimu, je, mimi humtegemea Mungu au wanadamu?’Met. 3:5, 6.

MCHUNGAJI MPYA ATENDA KWA NJIA TOFAUTI

6. Utawala wa Ahazi ulitofautianaje na wa Hezekia?

6 Ahazi alikufa mwaka wa 746 K.W.K., na Hezekia mwana wake akarithi ufalme maskini wa Yuda uliokuwa katika hali mbaya kiroho. Mfalme huyo kijana angetanguliza nini? Je, angeanza kuboresha uchumi wa Yuda uliozorota? Hapana. Hezekia alithamini mambo ya kiroho na alikuwa mchungaji mzuri wa taifa lake. Kwanza, alirudisha ibada safi na kuimarisha uhusiano kati ya Yehova na taifa hilo lililoasi. Alipoelewa mambo ambayo Mungu alitaka afanye, Hezekia alichukua hatua mara moja. Alituwekea mfano mzuri sana!2 Nya. 29:1-19.

7. Kwa nini Walawi walihitaji kuungwa mkono na mfalme mpya?

7 Walawi wangetimiza sehemu muhimu katika kazi ya kurudisha ibada safi. Hivyo, Hezekia alikutana nao na kuwahakikishia kwamba atawaunga mkono. Hebu wazia jinsi Walawi waaminifu waliohudhuria mkutano huo walivyotokwa na machozi ya furaha walipomsikia mfalme akitangaza hivi: “Yehova amewachagua ninyi msimame mbele zake ili kumhudumia.” (2 Nya. 29:11) Naam, Walawi waliagizwa waziwazi wawachochee watu warudie ibada safi!

8. Hezekia alichukua hatua gani nyingine ili kuboresha hali ya kiroho ya taifa hilo, na matokeo yalikuwa nini?

8 Hezekia aliwaalika wakaaji wote wa Yuda na Israeli kuhudhuria sherehe kubwa ya Pasaka, pamoja na Sherehe ya siku saba ya Keki Zisizo na Chachu. Watu walikuwa na shangwe sana hivi kwamba sherehe hiyo ikaendelea kwa siku saba zaidi. Biblia inasema hivi: “Kukawa na shangwe kubwa Yerusalemu, kwa maana tangu siku za Sulemani mwana wa Daudi mfalme wa Israeli hakukuwa na shangwe kama hiyo katika Yerusalemu.” (2 Nya. 30:25, 26) Watu wote walichochewa sana na karamu hiyo ya kiroho. Andiko la 2 Mambo ya Nyakati 31:1 linatuambia hivi: “Mara tu walipomaliza hayo yote, . . . wakazivunja nguzo takatifu na kuikata miti mitakatifu na kupabomoa  mahali pa juu na madhabahu.” Yuda lilipiga hatua kubwa katika kumrudia Yehova. Utakasaji huo wa kiroho ungewasaidia sana kukabiliana na matatizo ambayo yangetokea baadaye.

MFALME AJITAYARISHA KUKABILIANA NA MATATIZO

9. (a) Mipango ya Israeli ilikomeshwa jinsi gani? (b) Mwanzoni Senakeribu alifanikiwa jinsi gani huko Yuda?

9 Kama Isaya alivyotabiri, Waashuru waliushinda ufalme wa kaskazini wa Israeli na kuwapeleka wakaaji wake uhamishoni. Hilo lilikomesha mipango ya Israeli ya kumweka mtu mwingine kwenye kiti cha ufalme cha Daudi. Lakini namna gani mipango ya Ashuru? Waashuru sasa walikazia fikira ufalme wa Yuda. “Katika mwaka wa kumi na nne wa Mfalme Hezekia, Senakeribu mfalme wa Ashuru akapanda kuja juu ya majiji yote yenye ngome ya Yuda na kuyateka.” Inasemekana kwamba Senakeribu aliteka majiji 46 ya Yuda. Ungehisije ikiwa ungekuwa unaishi katika jiji la Yerusalemu wakati huo? Majeshi ya Ashuru yaliteka majiji ya Yuda, jiji moja baada ya lingine!2 Fal. 18:13.

10. Kwa nini huenda andiko la Mika 5:5 na 6 lilimtia moyo Hezekia?

10 Bila shaka, Hezekia alijua hatari iliyowakabili, lakini badala ya kuogopa na kuomba msaada kutoka kwa taifa la kipagani kama Ahazi, baba yake mwasi-imani alivyofanya, Hezekia alimtegemea Yehova. (2 Nya. 28:20, 21) Huenda alijua maneno yaliyosemwa na nabii Mika aliyeishi wakati huo na aliyetabiri hivi kuhusu Ashuru: “Mwashuru atakapokuja, . . . sisi pia tutasimamisha juu yake wachungaji saba, ndiyo, watawala wadogo wanane kutoka kati ya wanadamu. Nao wataichunga nchi ya Ashuru kwa upanga.” (Mika 5:5, 6) Bila shaka, maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yalimtia moyo Hezekia, kwa kuwa yanaonyesha kwamba jeshi hilo lisilo la kawaida lingesimamishwa dhidi ya Waashuru. Nalo lingewashinda kabisa wavamizi hao wakatili.

11. Unabii kuhusu wachungaji saba na watawala wadogo wanane ungetimizwa kwanza wakati gani?

11 Unabii kuhusu wachungaji saba na watawala wadogo (“wakuu,” Union Version) wanane ungetimizwa kwanza kwa njia  muhimu zaidi miaka mingi baada ya kuzaliwa kwa Yesu, yule “mtawala katika Israeli, ambaye asili yake ni kutoka nyakati za kale.” (Soma Mika 5:1, 2.) Utatimizwa wakati ujao ambapo “Mwashuru” wa siku hizi atakapotishia kuwaangamiza watumishi wa Yehova. Kupitia Mwana wake anayetawala sasa, Yehova atatumia jeshi gani kukabiliana na adui huyo anayeogopesha? Tutaona itakavyokuwa. Lakini kwanza, acheni tuchunguze mambo tunayojifunza kutokana na hatua alizochukua Hezekia alipokabili tishio la Waashuru.

HEZEKIA ACHUKUA HATUA ZIFAAZO

12. Hezekia na wenzake walichukua hatua gani ili kuwalinda watu wa Mungu?

12 Yehova yuko tayari sikuzote kutufanyia mambo tusiyoweza kufanya, lakini anatazamia tufanye yote tuwezayo. Hezekia alishauriana na “wakuu wake na wanaume wake wenye nguvu,” nao wakaamua “kuyaziba maji ya mabubujiko yaliyokuwa nje ya jiji . . . Tena [Hezekia] akajipa moyo na kujenga ukuta wote uliovunjika na kusimamisha minara juu yake, na upande wa nje ukuta mwingine, . . . na kutengeneza silaha kwa wingi na ngao.” (2 Nya. 32:3-5) Wakati huo, Yehova alitumia wanaume kadhaa mashujaa, yaani, Hezekia, wakuu wake, na manabii wenye nguvu kiroho, ili kuwalinda na kuwachunga watu Wake.

13. Ni hatua gani muhimu zaidi aliyochukua Hezekia ili kuwatayarisha watu kukabiliana na shambulizi? Eleza.

13 Kisha Hezekia alifanya jambo muhimu zaidi kuliko tu kuziba maji au kuimarisha kuta za jiji. Akiwa mchungaji anayejali, Hezekia aliwakusanya watu na kuwatia moyo kwa maneno haya: “Msiogope wala msiwe na hofu kwa sababu ya mfalme wa Ashuru . . . , kwa maana kuna wengi walio pamoja nasi kuliko wale walio pamoja naye. Yeye, mkono wa nyama uko pamoja naye, lakini sisi, Yehova Mungu wetu yuko pamoja nasi ili kutusaidia na kupigana vita vyetu.” Hicho kilikuwa kikumbusho kinachoimarisha imani kama nini, yaani, Yehova angewapigania watu wake! Waliposikia maneno hayo, Wayahudi “wakaanza kujitegemeza juu ya maneno ya Hezekia mfalme wa Yuda.” Ona kwamba “maneno ya Hezekia” ndiyo yaliyowatia moyo. Yeye, wakuu wake, wanaume wenye nguvu, pamoja na nabii Mika na Isaya walikuwa wachungaji wazuri, kama Yehova alivyotabiri kupitia nabii wake.2 Nya. 32:7, 8; soma Mika 5:5, 6.

Maneno ya Hezekia yaliwatia moyo

14. Rabshake alifanya nini, na watu walitendaje?

14 Mfalme wa Ashuru alipiga kambi huko Lakishi, upande wa kusini-magharibi wa Yerusalemu. Akiwa huko, aliwatuma wajumbe watatu ili waamuru jiji la Yerusalemu lijisalimishe. Msemaji wake aliyejulikana kwa jina la cheo, Rabshake, alitumia mbinu kadhaa. Aliongea Kiebrania na kuwasihi watu wamsaliti mfalme na kujitiisha chini ya Waashuru. Aliwaahidi kwa uwongo kwamba angewapeleka kwenye nchi nzuri ambako wangekuwa na maisha mazuri. (Soma 2 Wafalme 18:31, 32.) Kisha, Rabshake akadai kwamba Yehova angeshindwa kuwakomboa Wayahudi kutoka mkononi mwa Waashuru kama tu miungu ya mataifa ilivyoshindwa kuwalinda watu walioiabudu. Kwa hekima, watu hawakusema lolote kuhusu madai hayo ya uchongezi, na hivyo ndivyo watumishi wa Yehova wanavyofanya leo.Soma 2 Wafalme 18:35, 36.

15. Wakaaji wa Yerusalemu walipaswa kufanya nini? Yehova aliliokoa namna gani jiji hilo?

15 Bila shaka, jambo hilo lilimkasirisha Hezekia, lakini badala ya kuomba mataifa ya kigeni yamsaidie, alimwita nabii Isaya. Isaya alimwambia hivi Hezekia:  “[Senakeribu] hataingia katika jiji hili wala hatapiga mshale humo.” (2 Fal. 19:32) Wakaaji wa Yerusalemu walipaswa tu kuwa imara. Yehova angelipigania Yuda. Na kwa kweli, alilipigania! “Ikawa kwamba usiku huo malaika wa Yehova alitoka, akapiga na kuwaua watu 185,000 katika kambi ya Waashuru.” (2 Fal. 19:35) Yuda liliokolewa, si kwa sababu Hezekia aliziba chemchemi za maji na kujenga kuta za jiji hilo, bali kwa sababu Mungu alichukua hatua.

MAMBO TUNAYOJIFUNZA

16. Ni nani leo wanaofananishwa na (a) wakaaji wa Yerusalemu (b) “Mwashuru” (c) wachungaji saba na watawala wadogo wanane?

16 Unabii kuhusu wachungaji saba na watawala wadogo wanane utatimizwa kwa njia kubwa zaidi katika siku zetu. Wakaaji wa jiji la kale la Yerusalemu walishambuliwa na Waashuru. Hivi karibuni, watu wa Yehova wanaoonekana kuwa hawana ulinzi watashambuliwa na “Mwashuru” wa siku hizi akikusudia kuwaangamiza. Maandiko yanataja shambulizi hilo pamoja na lile la ‘Gogu wa Magogu,’ shambulizi la “mfalme wa kaskazini,” na shambulizi la “wafalme wa dunia.” (Eze. 38:2, 10-13; Dan. 11:40, 44, 45; Ufu. 17:14; 19:19) Je, mashambulizi hayo yanatofautiana? Si lazima. Huenda Biblia inarejelea shambulizi lilelile kwa kutumia majina tofauti-tofauti. Unabii wa Mika unaonyesha Yehova atatumia ‘silaha gani ya siri’ dhidi ya “Mwashuru,” yule adui mkatili? Atatumia silaha isiyo ya kawaida, yaani, “wachungaji saba, ndiyo, watawala wadogo wanane”! (Mika 5:5) Wazee wa kutaniko ndio wachungaji na watawala wadogo (au, “wakuu,” UV) katika jeshi hilo lisilo la kawaida. (1 Pet. 5:2) Bila shaka, Yehova ameweka leo wanaume wengi wanaothamini mambo ya kiroho ili wachunge kondoo wake wenye thamani, wawaimarishe watu wake kukabiliana na shambulizi linalokuja la “Mwashuru” wa siku hizi. * Unabii wa Mika unasema kwamba wanaume hao “wataichunga nchi ya Ashuru kwa upanga.” (Mika 5:6) Naam, “upanga wa roho,” yaani, Neno la Mungu, ni mojawapo ya ‘silaha zao za vita.’2 Kor. 10:4; Efe. 6:17.

17. Wazee wanajifunza mambo gani manne kutokana na habari tuliyochunguza?

17 Wazee wanaosoma makala hii wanajifunza mambo haya muhimu kutokana na habari tuliyochunguza: (1) Hatua inayofaa zaidi tunayoweza kuchukua ili tuwe tayari kukabiliana na shambulizi linalokuja la “Mwashuru” ni kuimarisha imani yetu katika Mungu na kuwasaidia ndugu zetu kufanya hivyo pia. (2) “Mwashuru” atakaposhambulia, ni lazima wazee wasadiki kabisa kwamba Yehova atatukomboa. (3) Wakati huo, tengenezo la Yehova litatupatia mwongozo unaookoa uhai, na huenda tukaona haufai. Ni lazima sote tuwe tayari kutii maagizo yoyote ambayo huenda tukapokea, iwe yanaonekana yanafaa au hayafai. (4) Wote wanaotegemea elimu ya kilimwengu, vitu vya kimwili, au mashirika ya wanadamu wanapaswa kurekebisha maoni yao sasa. Ni lazima wazee wawe tayari kumsaidia yeyote anayeyumba-yumba katika imani sasa.

18. Kutafakari habari hii kutatunufaisha jinsi gani wakati ujao?

18 Sawa na Wayahudi waliozingirwa na maadui jijini Yerusalemu siku za Hezekia, watumishi wa Mungu wataonekana hawana ulinzi. Wakati huo utakapofika, acheni sote tuimarishwe na maneno ya Hezekia. Tukumbuke kwamba adui zetu ‘wana mkono wa nyama, lakini sisi, Yehova Mungu wetu yuko pamoja nasi’!2 Nya. 32:8.

^ fu. 4 Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “mwanamwali” katika Isaya 7:14 linaweza kumaanisha mwanamke aliyeolewa au bikira. Kwa hiyo, neno hilohilo linaweza kumhusu mke wa Isaya na Maria, bikira Myahudi.

^ fu. 16 Katika Biblia, mara nyingi nambari saba humaanisha kitu kilichokamilika. Nyakati nyingine nambari nane, yaani, saba ukiongeza moja, humaanisha wingi.

(Tazama fungu la 12 na 13)