Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Jihadharini na Chachu ya Mafarisayo”

“Jihadharini na Chachu ya Mafarisayo”

“Jihadharini na Chachu ya Mafarisayo”

Yesu aliwaonya wanafunzi wake hivi: “Jihadharini na chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki.” (Luka 12:1) Onyo hili pia liliandikwa na Mathayo, naye anaeleza wazi kwamba Yesu alikuwa akishutumu “mafundisho” ya Mafarisayo.—Mt. 16:12.

Nyakati nyingine Biblia inatumia neno “chachu,” au hamira, kumaanisha uchafu. Bila shaka mafundisho na mtazamo wa Mafarisayo ulikuwa na matokeo mabaya kwa wasikilizaji wao. Kwa nini mafundisho ya Mafarisayo yalikuwa hatari?

1 Mafarisayo walijiona kwa kiburi kuwa waadilifu, nao waliwadharau watu wa kawaida.

Mtazamo huo wa kujiona kuwa waadilifu unaonekana katika mojawapo ya mifano ya Yesu. Alisema hivi: “Yule Farisayo akasimama na kuanza kusali mambo haya akisema moyoni, ‘Ee Mungu, ninakushukuru ya kuwa mimi si kama wale watu wengine, wanyang’anyi, wasio waadilifu, wazinzi, au hata kama mkusanya-kodi huyu. Mimi hufunga mara mbili kwa juma, mimi hutoa sehemu ya kumi ya vitu vyote ninavyojipatia.’ Lakini yule mkusanya-kodi akiwa amesimama umbali fulani hakutaka hata kuinua macho yake kuelekea mbinguni, bali alikuwa akipigapiga kifua chake, akisema, ‘Ee Mungu, unirehemu mimi mtenda-dhambi.’”—Luka 18:11-13.

Yesu aliusifu mtazamo wa unyenyekevu wa mkusanya-kodi huyo aliposema hivi: “Ninawaambia ninyi, Mtu huyu alishuka kwenda nyumbani kwake akiwa amethibitishwa kuwa mwadilifu zaidi kuliko yule mwingine [Farisayo]; kwa sababu kila mtu anayejiinua atafedheheshwa, bali yule anayejinyenyekeza atainuliwa.” (Luka 18:14) Ingawa wakusanya-kodi walijulikana kuwa watu wasio wanyoofu, Yesu alitaka kuwasaidia baadhi yao waliomsikiliza. Angalau wakusanya-kodi wawili, yaani, Mathayo na Zakayo, walikuja kuwa wafuasi wake.

Vipi ikiwa tutafikiri kwamba sisi ni bora zaidi ya wengine kwa sababu ya uwezo tuliopewa na Mungu au mapendeleo yetu au kwa sababu ya makosa na udhaifu wa wengine? Tunapaswa kung’oa haraka mawazo kama hayo kwa sababu Maandiko yanasema: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli.”—1 Kor. 13:4-6.

Tunapaswa kuwa na mtazamo kama wa mtume Paulo. Baada ya kusema kwamba “Kristo Yesu alikuja ulimwenguni ili kuwaokoa watenda-dhambi,” Paulo aliongeza hivi: “Kati ya hao mimi ni wa kwanza kabisa.”—1 Tim. 1:15.

Maswali ya kutafakari:

Je, ninatambua kwamba mimi ni mtenda-dhambi na kwamba wokovu wangu unategemea fadhili zisizostahiliwa za Yehova? Au ninaona miaka mingi ya utumishi mwaminifu, mapendeleo ya utumishi katika tengenezo la Mungu, au vipawa kuwa sababu ya kujiona bora kuliko wengine?

2 Mafarisayo walitaka kuwapendeza wengine kwa kujionyesha hadharani kuwa waadilifu. Walitamani umaarufu na majina makubwa ya cheo.

Lakini Yesu alionya hivi: “Kazi zote wanazozifanya wao huzifanya ili watazamwe na watu; kwa maana wanapanua vibweta vyenye maandiko ambavyo wao huvaa kama ulinzi, na kuongeza ukubwa wa pindo zenye nyuzinyuzi za mavazi yao. Wao hupenda mahali penye kuonekana zaidi kwenye milo ya jioni na viti vya mbele katika masinagogi, na salamu katika masoko na kuitwa Rabi na watu.” (Mt. 23:5-7) Angalia tofauti iliyopo kati ya mtazamo wao na mtazamo wa Yesu. Ingawa alikuwa Mwana mkamilifu wa Mungu, alikuwa mnyenyekevu. Mwanamume fulani alipomwita “mwema,” Yesu alisema: “Kwa nini unaniita mwema? Hakuna mtu aliye mwema, ila mmoja, Mungu.” (Marko 10:18) Katika pindi nyingine, Yesu aliosha miguu ya wanafunzi wake, na hivyo akawaachia wafuasi wake mfano wa unyenyekevu.—Yoh. 13:1-15.

Mkristo wa kweli anapaswa kuwatumikia waamini wenzake. (Gal. 5:13) Jambo hilo linawahusu hasa wale wanaotaka kustahili kuwa waangalizi katika kutaniko. Ni vizuri ‘kujitahidi kufikia cheo cha mwangalizi,’ lakini mtu anapaswa kuweka lengo au mradi huo kwa sababu anatamani kuwasaidia wengine. “Cheo” hiki si nafasi ya kujitafutia umaarufu au mamlaka. Wale wanaotumikia wakiwa waangalizi wanahitaji kuwa ‘wanyenyekevu moyoni,’ kama Yesu alivyokuwa.—1 Tim. 3:1, 6; Mt. 11:29.

Maswali ya kutafakari:

Je, nina mwelekeo wa kuwapendelea wale wenye mapendeleo ya utumishi kutanikoni, huenda nikitarajia kupata umaarufu au mapendeleo zaidi? Je, mimi hupenda kukazia uangalifu zaidi sehemu za utumishi wa Mungu ambazo zinaonekana zinanifanya nijulikane au nisifiwe? Je, kwa kweli ninajaribu kuwa maarufu mbele ya wengine?

3 Sheria na mapokeo ya Mafarisayo yalifanya iwe vigumu kwa watu wa kawaida kufuata Sheria za Mungu.

Yehova aliwapa Waisraeli Sheria ya Musa ili iwaonyeshe jinsi ya kumwabudu. Hata hivyo, haikueleza mambo madogo-madogo. Kwa mfano, Sheria ilikataza kufanya kazi siku ya Sabato, lakini haikusema waziwazi kazi ilitia ndani nini au haikutia ndani nini. (Kut. 20:10) Mafarisayo walitaka kujaza mapengo hayo kwa kutunga sheria zao, kutoa maelezo zaidi, na mapokeo. Yesu alishika Sheria ya Musa lakini alipuuza sheria zilizotungwa ovyoovyo na Mafarisayo. (Mt. 5:17, 18; 23:23) Yesu hakuifuata Sheria kidesturi tu. Yeye alitambua kusudi la Sheria na uhitaji wa rehema na huruma. Alikuwa na usawaziko, hata wafuasi wake walipokosea. Kwa mfano, ingawa aliwahimiza mitume wake watatu wakae macho na kuendelea kukesha usiku ambao alikamatwa, walilala tena na tena. Hata hivyo, kwa huruma alisema: “Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.”—Marko 14:34-42.

Maswali ya kutafakari:

Je, ninatunga sheria ngumu ovyoovyo au kugeuza maoni yangu binafsi kuwa sheria? Je, nina usawaziko kuhusu yale ninayotarajia wengine watimize?

Tafakari tofauti iliyopo kati ya mafundisho ya Yesu na yale ya Mafarisayo. Je, unaona mambo ambayo unaweza kuboresha? Kama ndivyo, kwa nini usiazimie kufanya hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Mafarisayo walivaa vibweta vyenye maandiko.—Mt. 23:2, 5

[Picha katika ukurasa wa 29]

Tofauti na Mafarisayo wenye kiburi, wazee Wakristo wanyenyekevu huwatumikia wengine

[Picha katika ukurasa wa 30]

Je, wewe una usawaziko kama Yesu kuhusu yale unayotarajia wengine watimize?