Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Uwezavyo Kutosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho

Jinsi Uwezavyo Kutosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho

Jinsi Uwezavyo Kutosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho

‘KATIKA miaka kumi iliyopita, vitabu zaidi ya 300 vinavyozungumzia jinsi hali ya kiroho inavyoweza kuathiri kazi, vimejaa katika maduka ya vitabu. Baadhi ya vitabu hivyo ni Jesus CEO na The Tao of Leadership,’ lasema gazeti U.S.News & World Report. Jambo hilo linaonyesha tu kwamba katika nchi nyingi zilizositawi, watu wanazidi kutamani mwongozo wa kiroho maishani. Likieleza kuhusu jambo hilo, jarida la kibiashara Training & Development linasema: “Wakati huu ambapo maisha yetu yanategemea sana teknolojia, tunatafuta kupata kusudi, maana, na uradhi zaidi maishani.”

Hata hivyo, unaweza kupata wapi mwongozo wa kiroho unaoridhisha? Zamani, watu walitegemea dini mashuhuri ziwasaidie kupata “kusudi” na “maana zaidi” maishani. Leo, wengi wamezikataa dini mashuhuri. Uchunguzi uliofanyiwa mameneja na wasimamizi wakuu 90 ulionyesha kwamba “watu hutofautisha kabisa dini na hali ya kiroho,” kinasema kichapo Training & Development. Wale waliohojiwa walisema kwamba dini “haivumilii nayo huleta mgawanyiko,” lakini hali ya kiroho “hukubali na kuunganisha wote.”

Vivyo hivyo, vijana wengi katika jamii zisizojishughulisha sana na dini, kama za Australia, New Zealand, Uingereza, na Ulaya, huona kuna tofauti kati ya dini na hali ya kiroho. Akiandika katika kichapo Youth Studies Australia, Profesa Ruth Webber, anasema: “Vijana wengi wanaamini kwamba kuna Mungu au nguvu fulani zisizo za asili, lakini hawaoni kama kanisa ni muhimu au linaweza kuwasaidia kuonyesha hali ya kiroho.”

Dini ya Kweli Huboresha Hali ya Kiroho

Inaeleweka ni kwa nini watu wana maoni hayo yenye shaka kuhusu dini. Dini nyingi zimejihusisha sana na hila za kisiasa na unafiki wa kimaadili nazo zimemwaga damu nyingi ya watu wasio na hatia katika vita vingi vya kidini. Hata hivyo, ingawa wengine wamekataa dini kwa sababu zimejaa unafiki na udanganyifu, wamekosea kuikataa Biblia pia wakifikiri kwamba inaunga mkono mazoea hayo.

Kwa kweli, Biblia hushutumu unafiki na uasi-sheria. Yesu aliwaambia hivi viongozi wa dini wa siku zake: “Ole wenu ninyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa sababu mnafanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, ambayo kwa nje yanaonekana kwa kweli kuwa mazuri lakini ndani yamejaa mifupa ya wafu na kila namna ya ukosefu wa usafi. Katika njia hiyo ninyi pia, kwa kweli, mnaonekana kwa nje kuwa waadilifu kwa watu, lakini ndani mmejaa unafiki na uasi-sheria.”—Mathayo 23:27, 28.

Isitoshe, Biblia huwahimiza Wakristo wasijihusishe na mambo yoyote ya kisiasa. Badala ya kuwahimiza waumini wauane, huwaagiza wawe tayari kufiana. (Yohana 15:12, 13; 18:36; 1 Yohana 3:10-12) Badala ya kuwa “isiyovumilia na yenye kuleta mgawanyiko,” dini ya kweli ambayo inategemea Biblia “huunganisha wote.” Mtume Petro alisema: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.

Biblia Ni Mwongozo Unaotegemeka ili Kuwa na Hali Nzuri ya Kiroho

Biblia inatuambia kwamba wanadamu wameumbwa kwa mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:26, 27) Hiyo haimaanishi kwamba wanadamu wanafanana na Mungu kihalisi, bali inamaanisha kwamba wanadamu wana uwezo wa kudhihirisha sifa za Mungu kutia ndani mambo ya kiroho.

Hivyo, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba Mungu pia angetuonyesha njia ya kutosheleza mahitaji yetu ya kiroho, na pia kutuandalia mwongozo unaofaa ambao unaweza kutusaidia kutofautisha mambo yenye manufaa na yale yanayoweza kutudhuru kiroho. Kama vile Mungu alivyotuumba tukiwa na mfumo bora wa kinga, ambao hutukinga na magonjwa na kutusaidia tuwe na afya nzuri, yeye pia alitupatia dhamiri, au sauti ya ndani, inayoweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayofaa na kuepuka mazoea yanayotudhuru kimwili na kiroho. (Waroma 2:14, 15) Kama tujuavyo, ili mfumo wetu wa kinga ufanye kazi vizuri, ni lazima ulishwe vizuri. Vivyo hivyo, ili dhamiri yetu ifanye kazi, tunahitaji kuilisha chakula kizuri cha kiroho.

Akitaja chakula kitakachotusaidia kudumisha hali nzuri ya kiroho, Yesu alisema: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mathayo 4:4) Semi za Yehova zimeandikwa katika Neno lake Biblia, nazo ni ‘zenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.’ (2 Timotheo 3:16) Kwa hiyo, ni jukumu letu kujitahidi kula chakula hicho cha kiroho. Tutanufaika kiroho na kimwili kadiri tunavyozidi kuijua Biblia na kujitahidi kutumia kanuni zake maishani.—Isaya 48:17, 18.

Je, Jitihada Hiyo Inafaa?

Kwa kweli, inachukua muda kuboresha hali yetu ya kiroho kwa kujifunza Biblia; na inaonekana inazidi kuwa vigumu kupata wakati wa kufanya hivyo. Lakini tutapata thawabu tukitafuta wakati wa kuboresha hali yetu ya kiroho. Wasikilize wataalamu fulani wenye shughuli nyingi wanapoeleza kwa nini ni muhimu kutumia wakati kushughulikia hali yao ya kiroho.

Marina, ambaye ni daktari, anasema: “Sikuwa nimewahi kufikiria hali yangu ya kiroho hadi nilipoanza kufanya kazi katika hospitali fulani na kuanza kuguswa moyo sana na jinsi wengine wanavyoteseka. Ndipo nikafahamu kwamba nilipaswa kutambua na kutosheleza uhitaji wangu wa kiroho ili nipate uradhi na utulivu, kwa kuwa mtu anayefanya kazi kama yangu anaweza kulemewa na pilikapilika za maisha na kushughulikia mahangaiko ya wengine.

“Sasa ninajifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Funzo hilo hunisaidia kuchunguza matendo na malengo yangu kwa njia inayofaa na pia hunisaidia kuwa na maoni yanayofaa na hivyo kuwa na usawaziko maishani. Ninafurahia sana kazi yangu. Lakini funzo la Biblia ndilo ambalo limeboresha hali yangu ya kihisia-moyo na kunisaidia kudhibiti hisia zisizofaa, kupunguza wasiwasi, na kuwa mwenye subira na mwenye kuwahurumia watu zaidi. Kutumia kanuni za Biblia kumeboresha ndoa yangu pia. Jambo muhimu zaidi ni kwamba nimemjua Yehova na ninapata kwa kiasi kidogo roho yake takatifu ambayo imefanya maisha yangu yawe na maana zaidi.”

Nicholas, ambaye ni msanifu wa majengo, anasema: “Kabla ya kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, sikupendezwa kabisa na mambo ya kiroho. Nilikuwa na mradi mmoja tu maishani, yaani, kufanikiwa katika kazi niliyochagua. Katika funzo langu la Biblia nimejifunza kwamba mbali na kazi kuna mambo mengine maishani, na kwamba kufanya mapenzi ya Yehova huleta furaha ya kweli na ya kudumu.

“Ninafurahia kazi yangu, lakini Biblia ndiyo imenifunza umuhimu wa kuishi maisha rahisi kwa kuzingatia mambo ya kiroho. Kwa kufanya hivyo, mimi na mke wangu tumeepuka mikazo inayoletwa na maisha ya kufuatia vitu vya kimwili. Pia tumepata marafiki wengi wa kweli kwa kushirikiana na wale ambao wana mtazamo kama wetu kuhusu maisha.”

Vincent, ambaye ni mwanasheria, anasema: “Kazi nzuri inaweza kuleta furaha ya kiasi fulani. Hata hivyo, nimeona kwamba kuna mengi yanayohitajiwa ili kupata furaha na uradhi. Kabla ya kujua mafundisho ya Biblia kuhusu jambo hilo, ninakumbuka wakati mmoja nikigutuka kwamba maisha hayana maana kabisa—kuzaliwa, kukua, kufunga ndoa, kufanya kazi ili kuwaandalia watoto mahitaji ya kimwili, kuwazoeza kufuata mkondo uleule wa maisha, na mwishowe kuzeeka na kufa.

“Baada tu ya kuanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova ndipo nilipojibiwa kwa njia yenye kuridhisha maswali yangu kuhusu kusudi la maisha. Funzo langu la Biblia limeniwezesha kumjua Yehova kuwa mtu na kukuza upendo mwingi kwake. Jambo hilo hunisaidia kudumisha hali nzuri ya kiroho ninapojitahidi kuishi kupatana na lile ninalojua kuwa kusudi lake. Sasa, mimi na mke wangu tunafurahi kujua kwamba tunatumia maisha yetu kwa njia inayofaa kabisa.”

Wewe pia unaweza kupata maana na kusudi la maisha kwa kujifunza Biblia. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia. Kama Marina, Nicholas, na Vincent, unaweza kupata uradhi unaotokana na kujifunza kumhusu Yehova na makusudi yake kwa wanadamu kwa ujumla na kwako binafsi. Utafurahi kutosheleza mahitaji yako ya kiroho sasa na pia kuwa na taraja la kuishi milele ukiwa na afya kamilifu ya kimwili. Taraja hilo ni la wale tu “wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Sala ni njia moja ya kusitawisha hali yetu ya kiroho. Yesu alitumia wakati kuwafunza wanafunzi wake jinsi ya kusali na kuwapa ile ambayo kwa ukawaida inaitwa Sala ya Bwana. Sala hiyo inamaanisha nini kwako leo? Inaweza kukunufaishaje? Utapata majibu katika makala mbili zinazofuata.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Marina

[Picha katika ukurasa wa 7]

Nicholas

[Picha katika ukurasa wa 7]

Vincent