Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Elisha aliomba “sehemu mbili” za roho ya Eliya?

Kabla tu ya Eliya kukamilisha mgawo wake wa kutoa unabii Israeli, nabii mchanga Elisha alimwomba hivi: “Tafadhali, sehemu mbili za roho yako zije kwangu.” (2 Wafalme 2:9) Katika maana ya kiroho, yaonekana Elisha alikuwa akiomba fungu mara mbili kama lile alilopewa mwana mzaliwa wa kwanza. (Kumbukumbu la Torati 21:17) Tukichunguza kwa ufupi masimulizi hayo yatatusaidia kuelewa jambo hilo na tutajifunza kutokana na yale yaliyotukia.

Kupatana na mwongozo wa Yehova, nabii Eliya alimtia mafuta Elisha achukue mahali pake. (1 Wafalme 19:19-21) Kwa miaka sita hivi, Elisha alimhudumia Eliya kwa uaminifu naye aliazimia kufanya hivyo mpaka mwisho. Hata katika siku ya mwisho ya Eliya akiwa nabii wa Israeli, Elisha alishikamana na mshauri na mwalimu wake. Ingawa Eliya alimsihi Elisha aache kumfuata, nabii huyo mchanga alisema hivi mara tatu: “Mimi sitakuacha.” (2 Wafalme 2:2, 4, 6; 3:11) Naam, Elisha alimwona nabii huyo mwenye umri mkubwa zaidi kuwa baba yake wa kiroho.—2 Wafalme 2:12.

Hata hivyo, Eliya alikuwa na wana wengine wa kiroho mbali na Elisha. Eliya na Elisha walishirikiana na kikundi cha wanaume kilichojulikana kuwa “wana wa manabii.” (2 Wafalme 2:3) Masimulizi katika Wafalme wa Pili yanaonyesha kwamba “wana” hao pia walikuwa na uhusiano wa karibu na baba yao wa kiroho, Eliya. (2 Wafalme 2:3, 5, 7, 15-17) Hata hivyo, kwa kuwa Elisha alikuwa ametiwa mafuta kuchukua mahali pa Eliya, yeye ndiye aliyekuwa mwana wa kiroho wa Eliya muhimu zaidi. Alikuwa kama mzaliwa wa kwanza. Katika Israeli la kale, mwana mzaliwa wa kwanza halisi, alipokea sehemu mbili za urithi wa baba yake, lakini wana wale wengine walipokea sehemu moja tu. Kwa hiyo, Elisha aliomba sehemu mbili za urithi wa kiroho wa Eliya.

Kwa nini Elisha alitoa ombi hilo wakati huo hasa? Kwa sababu alikuwa karibu kuanza mgawo mzito, yaani, kuwa nabii katika Israeli badala ya Eliya. Elisha alitambua kwamba ili kutimiza majukumu yaliyohusiana na mgawo huo mzito, alihitaji nguvu za kiroho zinazopita uwezo wake, ambazo ni Yehova tu ambaye angeweza kuzitoa. Alihitaji kuwa jasiri kama Eliya. (2 Wafalme 1:3, 4, 15, 16) Kwa hiyo, aliomba sehemu mbili za roho ya Eliya, yaani, roho ya ujasiri na ya kuwa mwenye “wivu kwelikweli kwa ajili ya Yehova.” Sifa hizo nzuri hutokana na roho ya Mungu. (1 Wafalme 19:10, 14) Eliya aliitikiaje?

Eliya alijua kwamba Elisha alikuwa ameomba kitu ambacho Mungu tu ndiye aliyekuwa na haki ya kukitoa. Kwa hiyo, Eliya alimjibu hivi kwa unyenyekevu: “Umeomba jambo gumu. Ukiniona wakati nitakapochukuliwa kutoka kwako, itakuwa hivyo kwako.” (2 Wafalme 2:10) Na kwa kweli, Yehova alimruhusu Elisha amwone Eliya akipanda katika dhoruba ya upepo. (2 Wafalme 2:11, 12) Elisha alipewa kile alichoomba. Yehova alimpa roho aliyohitaji ili kuanza mgawo wake mpya na kukabiliana na majaribu ambayo yangempata.

Leo, Wakristo waliotiwa mafuta (ambao nyakati nyingine wanaitwa jamii ya Elisha), na watumishi wa Mungu kwa ujumla, wanaweza kutiwa moyo sana na masimulizi hayo ya Biblia. Nyakati nyingine, huenda tukahisi kwamba hatuna uwezo na hatustahili tunapopewa mgawo mpya, au huenda ujasiri wetu wa kuendelea na kazi ya kuhubiri Ufalme unapungua tunapokabili ubaridi au upinzani katika eneo letu. Hata hivyo, tunapomwomba Yehova atusaidie, atatupatia roho takatifu kwa kuwa tunaihitaji ili kukabiliana na magumu na hali zinazobadilika-badilika. (Luka 11:13; 2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:13) Naam, kama vile Yehova alivyomwimarisha Elisha ili aweze kutimiza majukumu yake mazito zaidi, atatusaidia sote pia, vijana kwa wazee, kutimiza huduma yetu.—2 Timotheo 4:5.