Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumwamini Mungu Ambaye Huenda Hatumjui

Kumwamini Mungu Ambaye Huenda Hatumjui

Kumwamini Mungu Ambaye Huenda Hatumjui

WATU wawili kati ya watatu nchini Ujerumani wanamwamini Mungu. Hata hivyo, watu zaidi ya elfu moja walipoulizwa wafafanue Mungu wanayemwamini, karibu kila mtu alitoa jibu tofauti. “Wajerumani wana maoni tofauti-tofauti kuhusu Mungu kama vile wao wenyewe wanavyotofautiana,” laripoti gazeti FOCUS. Ingawa watu wanapaswa kupongezwa kwa kumwamini Mungu, ni jambo lenye kusikitisha kumwamini Mungu usiyejua utu wake, sivyo?

Si Wajerumani tu walio na tatizo la kukosa uhakika kuhusu utu wa Mungu, hata watu wa nchi nyingine za Ulaya wana tatizo hilohilo. Uchunguzi uliofanywa nchini Austria, Uholanzi, na Uingereza ulionyesha kwamba watu wengi wanakubali kuwa Mungu ni “mwenye mamlaka ya juu sana na hawezi kufafanuliwa.” Vijana hasa, hata wale wanaomwamini Mungu, humwona kuwa fumbo.

Je, Unamjua Mungu Kibinafsi?

Kuna tofauti kubwa sana kati ya kumfahamu mtu tu, na kumjua kibinafsi. Kusikia habari juu ya mtu fulani kama vile mtawala aliye mbali, mchezaji mashuhuri, au mcheza sinema, ni kutambua tu kwamba yuko. Hata hivyo, kumjua mtu kibinafsi kunahusisha mambo mengi zaidi. Kunahusisha kujua sifa za mtu huyo, mwenendo wake, hisia zake, mambo anayopenda na asiyopenda, na mambo anayokusudia kufanya wakati ujao. Kumjua mtu kibinafsi hutuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye.

Watu wengi wamekata kauli kwamba kumjua Mungu kijuujuu tu au kutambua kwamba yeye yuko hakutoshi. Wamechukua hatua ya kumjua Mungu kwa undani zaidi. Je, wamenufaika kwa kufanya hivyo? Paul, mwanamume anayeishi kaskazini mwa Ujerumani na ambaye wakati fulani alimjua Mungu kijuujuu tu, aliamua kumjua Mungu kibinafsi. Paul anasema hivi: “Kumjua Mungu kibinafsi hutaka wakati na jitihada, lakini unanufaika sana kwa kufanya hivyo. Kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Muumba hufanya maisha yawe bora.”

Je, kuna manufaa yoyote kutumia wakati na kujitahidi kumjua Mungu kwa undani zaidi? Tafadhali soma makala inayofuata.

[Blabu katika ukurasa wa 3]

Kuna tofauti kubwa sana kati ya kumfahamu mtu tu, na kumjua kibinafsi