Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jenga Utu wa Mtoto Wako!

Jenga Utu wa Mtoto Wako!

Jenga Utu wa Mtoto Wako!

MFINYANZI stadi anaweza kutumia udongo usio na thamani yoyote kutengeneza chombo kizuri sana. Si mafundi wengi wanaoweza kutumia kitu duni kama udongo kutengeneza vitu vingi vizuri. Kwa maelfu ya miaka watu wamewategemea wafinyanzi kupata vikombe, sahani, nyungu, gudulia, na vyombo vinginevyo.

Wazazi vilevile wanaweza kunufaisha jamii kwa kujenga utu na tabia za watoto wao. Biblia inalinganisha kila mmoja wetu na udongo, na Mungu amewapa wazazi wajibu muhimu wa “kufinyanga” watoto wao kana kwamba wao ni “udongo” mikononi mwao. (Ayubu 33:6; Mwanzo 18:19) Kutengeneza chombo maridadi kwa udongo si kazi rahisi. Hali kadhalika, kumlea mtoto ili awe mtu mzima mwenye kutegemeka na mwenye akili ni kazi ngumu inayotaka jitihada nyingi.

Kuna uvutano mwingi unaowaathiri watoto wetu. Jambo la kusikitisha ni kwamba uvutano mwingine unapotosha. Kwa hivyo, mzazi mwenye hekima atajitahidi kujenga utu wa mtoto na kumlea “katika njia impasayo,” akiwa na uhakika kwamba mtoto “hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”—Mithali 22:6.

Wanapofanya kazi hii muhimu na yenye kufurahisha ya kulea mtoto, ni lazima wazazi Wakristo wenye hekima watumie wakati kukinza ushawishi mbaya unaoweza kuathiri utu wa mtoto wao. Upendo wao utajaribiwa vilivyo wanapolea mtoto kwa subira “katika nidhamu na mafundisho ya Kikristo.” (Waefeso 6:4, BHN) Bila shaka kazi ya wazazi itarahisishwa sana wakianza mapema.

Anza Mapema

Wafinyanzi hupenda kutumia udongo laini unaoweza kufinyangwa kwa urahisi. Lakini udongo unapaswa pia kuwa mgumu vya kutosha ili umbo la chombo lisiharibike baada ya kuundwa. Kwa kawaida wafinyanzi hupenda kusafisha udongo na kuutumia kabla ya miezi sita kuisha. Hali kadhalika, wakati bora wa kuanza kujenga utu wa mtoto ni wakati anapoweza kuongozwa kwa urahisi.

Wataalamu wa watoto wanasema kwamba mtoto mwenye umri wa miezi minane amekwisha tambua matamshi ya lugha ya mama, ana uhusiano wa karibu na wazazi wake, ameanza kutumia akili na kuchunguza mazingira yake. Ni heri kuanza kujenga utu wake akiwa bado mchanga. Mtoto wako atanufaika kama nini ikiwa yeye, kama Timotheo, ‘atayajua maandishi matakatifu tangu utoto sana’!—2 Timotheo 3:15. *

Watoto wachanga huiga wazazi wao. Mbali na kuiga sauti, na ishara za uso na mikono, wao hujifunza kuonyesha upendo, fadhili, na huruma wanapowaona wazazi wao wakionyesha sifa hizo. Tukitaka kuwalea watoto wetu kupatana na sheria za Yehova, kwanza ni lazima sisi wenyewe tupende kwa moyo wote maagizo ya Mungu. Wazazi wanaothamini kwa moyo Neno la Mungu husukumwa waongee kwa ukawaida na watoto wao kumhusu Yehova na kuhusu Neno lake. Biblia inahimiza hivi: ‘Yanene uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.’ (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Francisco na Rosa walio na watoto wawili wachanga wanaeleza jinsi wanavyofuata ushauri huo. *

“Mbali na mazungumzo ya kawaida, sisi hujitahidi kuongea na kila mtoto kwa angalau dakika 15 kila siku. Tunapotambua kwamba wana tatizo fulani, sisi hutumia muda mrefu zaidi kuongea nao. Kwa mfano, hivi majuzi mwana wetu mwenye umri wa miaka mitano alirudi nyumbani kutoka shuleni na kutuambia kwamba hamwamini Yehova. Inaonekana kwamba mwanadarasa mwenzake alikuwa amemfanyia mzaha na kumwambia kwamba hakuna Mungu.”

Wazazi hao walitambua kwamba watoto wanahitaji kujenga imani katika Muumba wao. Watoto huvutiwa sana na uumbaji wa Mungu. Wao hupenda kama nini kumpapasa-papasa mnyama, kuchuma maua ya kondeni, au kucheza kwenye mchanga ufuoni! Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao kuelewa kwamba Mungu ndiye aliyeviumba vitu hivyo vyote. (Zaburi 100:3; 104:24, 25) Huenda hawataacha kamwe kuheshimu na kustaajabia uumbaji wa Yehova. (Zaburi 111:2, 10) Mtoto anapoelewa hayo anaweza kusitawisha tamaa ya kumpendeza Mungu na hofu ya kutompendeza. Jambo hilo litamsukuma ‘ajiepushe na maovu.’—Mithali 16:6.

Ijapokuwa watoto wengi wadogo wana hamu ya kujifunza, nao hujifunza kwa urahisi, utii si jambo rahisi kwa mtoto. (Zaburi 51:5) Nyakati nyingine wao husisitiza kufanya jinsi wanavyopenda au kupewa kila kitu kinachowapendeza. Ni lazima wazazi wawe imara na wenye subira, na watoe nidhamu ili kukomesha mielekeo hiyo. (Waefeso 6:4) Phyllis na Paul ambao wamefaulu kulea watoto watano vizuri, wamejionea jambo hilo.

Phyllis akumbuka: “Ijapokuwa kila mtoto alikuwa na utu tofauti na wale wengine, kila mmoja wao alitaka kufanya kama alivyopenda. Haikuwa rahisi, lakini hatimaye walielewa kwamba hawawezi kufuata mapendezi yao sikuzote.” Mume wake Paul anasema hivi: “Tuliwaeleza sababu za maamuzi yetu iwapo walikuwa na umri wa kutosha kuzielewa. Kwa upole, tuliwafundisha kuheshimu mamlaka ambayo Mungu ametupatia.”

Ijapokuwa mtoto anaweza kuwa na matatizo utotoni, wazazi wengi wameona kwamba matatizo makubwa huzuka ujanani, wakati ambapo kijana hukabili majaribu mengi mapya.

Kugusa Moyo wa Kijana

Ni lazima mfinyanzi aufinyange udongo kabla haujakauka. Ili amalize kazi yake, nyakati nyingine yeye huongeza maji ili udongo ubaki laini. Hali kadhalika, itawabidi wazazi kujitahidi sana kuzuia moyo wa kijana usiwe mgumu. Bila shaka wao hutumia Biblia hasa ili ‘kukaripia, kunyoosha mambo, na kumwandalia kijana vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.’—2 Timotheo 3:15-17.

Hata hivyo, huenda kijana asikubali ushauri wa wazazi kwa utayari kama alivyofanya alipokuwa mtoto mdogo. Huenda vijana wakaanza kutia maanani maoni ya marika wao, na jambo hilo litafanya mawasiliano ya moyoni pamoja na wazazi wao yakome. Huo ndio wakati wa kuonyesha subira na busara zaidi kwa kuwa uhusiano kati ya wazazi na watoto hubadilika. Kijana hupambana na mabadiliko ya mwili na hisia. Itambidi kuanza kufanya maamuzi na kuweka miradi atakayofuatia maishani mwake. (2 Timotheo 2:22) Ushawishi wa vijana wenzake unaweza kumwathiri sana kijana katika kipindi hicho kigumu.

Ushawishi huo si tukio moja tu linalotambulika wazi. Badala yake, kwa kawaida vijana hushawishiwa hatua kwa hatua kwa maneno na matendo yanayowavunja moyo wasishikilie maadili na msimamo wao. Vijana wengi huhofia kutengwa na vijana wenzao, kwa hiyo, wale wanaowashawishi hulenga udhaifu huo. Kijana anayepambana na haya na anayetaka kukubaliwa na wengine anaweza kuanza kufuatia “vitu vilivyo katika ulimwengu” ambavyo vijana wengine hufuatia.—1 Yohana 2:15-17; Waroma 12:2.

Isitoshe, huenda kijana asiye mkomavu avutiwe na maneno na matendo ya vijana wenzake. Semi kama “Ujifurahishe” na “Fanya kile unachopenda” huenda zikavutia sana. María anakumbuka yaliyompata: “Niliwasikiliza vijana wenzangu walioamini kwamba vijana wana haki ya kujifurahisha kabisa bila kufikiria matokeo. Nusura nijiingize katika taabu kubwa kwa sababu nilitaka kufanya yale ambayo rafiki zangu shuleni walifanya.” Mzazi anawezaje kumsaidia kijana wake kushinda ushawishi huo?

Kwa maneno na matendo, mhakikishie tena na tena kwamba unamjali. Jitahidi kujua maoni yake kuhusu mambo mbalimbali na kuelewa matatizo yake, ambayo mara nyingi huwa magumu kuliko yale ambayo wewe ulikabili shuleni. Kijana wako anahitaji kujua kwamba utamsikiliza anapokueleza yaliyo moyoni mwake. (Mithali 20:5) Kwa kuangalia tu sura yake au jinsi anavyojiendesha, unaweza kujua kama ana tatizo au amechanganyikiwa. Msaidie ijapokuwa hajasema, na ‘ufariji moyo wake.’—Wakolosai 2:2.

Bila shaka, ni muhimu sana kuwa imara kuhusiana na yaliyo haki. Mara kwa mara mtoto hupinga uamuzi fulani wa wazazi, lakini si vizuri kumruhusu mtoto apindue uamuzi unaofaa. Kwa upande mwingine, hakikisha kwamba unaelewa hali vizuri kabla ya kuamua kumtia mtoto nidhamu kwa upendo au kabla ya kuamua jinsi utakavyomtia nidhamu ikiwa inahitajiwa.—Mithali 18:13.

Ushawishi Hata Kutanikoni

Chombo cha udongo kinaweza kuonekana kuwa kimekamilika, lakini kama hakijachomwa katika tanuru huenda kikaathiriwa na kile kitakachowekwa ndani. Majaribu na magumu yanafananishwa na moto katika Biblia kwa sababu hayo yanafanya sifa zetu ziwe dhahiri. Biblia inataja hasa majaribu ya imani, hata hivyo, kanuni hiyo inahusu pia majaribu ya kawaida maishani. (Yakobo 1:2-4) Jambo linaloshangaza ni kwamba vijana wanaweza kukabili majaribu magumu kutanikoni.

Ijapokuwa kijana wako anaonekana kuwa na hali nzuri ya kiroho, huenda anasitasita kati ya mapendezi mawili. (1 Wafalme 18:21) Kwa mfano, vijana fulani waliohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme walimshawishi Megan afuate mtindo wa ulimwengu:

“Nilivutiwa na vijana fulani ambao waliuona Ukristo kuwa wenye kuchosha na kizuizi cha kupata raha. Walisema mambo kama haya: ‘Mara nitakapofikia umri wa miaka 18, nitaacha kweli,’ au ‘Ninatamani kama nini maisha ya nje.’ Walijitenga na vijana waliopinga maoni hayo, na kuwaita watakatifu.”

Mtu mmoja tu au wawili wenye mwelekeo mbaya wanaweza kuwachochea wengine wote. Na kwa kawaida, mtu mmoja-mmoja katika kikundi fulani hufuata wale wengine. Huenda hekima na adabu zikapuuzwa kwa sababu ya ujinga na ushupavu. Vijana Wakristo katika nchi nyingi wamejikuta taabani kwa sababu ya kuwafuata vijana wenye mwenendo mbaya.

Bila shaka vijana wanahitaji kujifurahisha kwa kushirikiana na wengine kwa kadiri fulani. Mzazi anawezaje kuwaandalia watoto wake ushirika huo? Panga burudani kwa ajili ya watoto, na upange mambo yanayopendeza ambayo familia yenu inaweza kufanya pamoja, au mkiwa pamoja watu wengine, vijana kwa wazee. Wafahamu rafiki za mtoto wako. Wakaribishe kwa chakula, au uwakaribishe nyumbani jioni moja. (Waroma 12:13) Mtie mtoto wako moyo ajifunze kucheza ala fulani ya muziki, lugha ya kigeni, au ufundi fulani. Mara nyingi angeweza kufanya hivyo akiwa salama nyumbani.

Masomo Yanaweza Kumlinda

Masomo ya shuleni yanaweza pia kumsaidia kijana asifuatie raha kupita kiasi. Loli, ambaye amekuwa msimamizi wa shule moja kubwa kwa miaka 20 anasema hivi: “Nimewaona vijana wengi wa Mashahidi waliosoma kwenye shule hii. Wengi walikuwa na mwenendo mzuri, lakini wengine walijiendesha kama wale wanafunzi wengine. Wale waliokuwa na mwenendo mzuri walitia maanani masomo yao. Mimi hupendekeza kwa dhati kwamba wazazi wajihusishe na masomo ya watoto wao, wawajue walimu wao, na kuwasadikisha watoto wao kwamba matokeo mazuri shuleni ni muhimu. Baadhi yao watafanya vizuri sana, lakini wote wataweza kuwa na matokeo mazuri na walimu watawastahi.”

Masomo yanaweza kuwasaidia vijana kufanya maendeleo ya kiroho pia. Wakiwa shuleni, wanaweza kujifunza mazoea mazuri ya kusoma, jinsi ya kukaza fikira, na kuwa watu wanaotegemeka. Bila shaka watatiwa moyo kujifunza na kufundisha Neno la Mungu vizuri zaidi wakiwa wasomaji stadi na wakielewa yale wanayosoma. (Nehemia 8:8) Wakitumia muda wa kutosha katika masomo yao ya shuleni na katika kujifunza mambo ya kiroho, hawatakuwa na nafasi ya kufuatia raha kupita kiasi.

Sifa kwa Mzazi na kwa Yehova

Vyombo vingi vya udongo huko Ugiriki ya kale vilikuwa na jina la mfinyanzi na vilevile la yule msanii aliyevipamba. Hali kadhalika, kwa kawaida kuna watu wawili katika familia wanaosaidiana kulea watoto. Baba na mama hushirikiana katika kujenga utu wa mtoto, na ni kana kwamba “majina” ya wote wawili yanaonekana kwenye utu wake. Kama vile mfinyanzi au msanii stadi, wewe unaweza kujivunia kazi yako unapolea kijana awe mtu mwema na mwenye adabu.—Mithali 23:24, 25.

Utafaulu katika kazi hiyo muhimu kwa kadiri unavyojitahidi kujenga utu wa mtoto wako. Tumaini letu ni kwamba utaweza kusema hivi: “Sheria ya Mungu wake imo moyoni mwake. Hatua zake hazitelezi.” (Zaburi 37:31) Ni muhimu sana kujenga utu wa mtoto wako.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Wazazi fulani huwasomea watoto wao waliozaliwa karibuni Biblia. Huenda ikawa sauti tulivu ya msomaji na furaha ambayo mtoto huhisi anaposomewa, itafanya apende kusoma baadaye maishani.

^ fu. 9 Baadhi ya majina yamebadilishwa.