Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni nini maana ya usemi huu kwenye Waebrania 12:4: “Bado hamjakinza kamwe hadi damu”?

Usemi ‘kukinza hadi damu’ humaanisha kuendelea kuvumilia hata kufikia kifo, yaani mtu kumwaga damu yake kihalisi.

Mtume Paulo alijua kwamba kwa sababu ya imani yao, baadhi ya Wakristo Waebrania walikuwa tayari ‘wamevumilia shindano kubwa chini ya mateso.’ (Waebrania 10:32, 33) Akizungumzia hayo, yaelekea Paulo alitumia mfano wa jitihada zilizoonyeshwa katika mashindano ya michezo ya Wagiriki ambayo yangetia ndani kukimbia, kupigana mwereka, kupigana ngumi, na kurusha kisahani na mkuki. Kwa sababu hiyo, Paulo aliwasihi Wakristo wenzake hivi katika Waebrania 12:1: “Acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.”

Katika mistari mitatu inayofuata, kwenye Waebrania 12:4, huenda Paulo aliamua kutumia mfano wa mashindano ya kupigana ngumi badala ya ule wa kukimbia. (Mifano hiyo miwili inatajwa kwenye 1 Wakorintho 9:26.) Mabondia wa kale walifunga ngumi na viwiko vyao kwa kamba za ngozi. Kamba hizo huenda zilikuwa na “vyuma au vipande vidogo-vidogo vya metali ambavyo viliwaumiza sana mabondia.” Michezo ya kikatili ya aina hiyo ilisababisha kuvuja damu sana na wakati mwingine kifo.

Hata hivyo, Wakristo Waebrania walikuwa na mifano mingi ya watumishi waaminifu wa Mungu ambao walinyanyaswa na kutendwa kikatili hata kufikia kifo, yaani “hadi damu.” Ona yaliyomfanya Paulo azungumzie mambo yaliyowapata watumishi waaminifu wa kale:

“Walipigwa kwa mawe, walijaribiwa, walikatwa vipande-vipande kwa msumeno, walikufa kwa kuchinjwa kwa upanga, walienda wakizunguka huku na huku katika ngozi za kondoo, katika ngozi za mbuzi, huku wakiwa katika uhitaji, katika dhiki, chini ya kutendwa vibaya.” Baadaye, Paulo alimtaja Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu: “Alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu, na ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.”—Waebrania 11:37; 12:2.

Naam, wengi ‘walikinza hadi damu,’ yaani hata kufikia kifo. Ukinzani wao haukuwa tu pambano la moyoni dhidi ya dhambi ya kukosa imani. Walikuwa waaminifu-washikamanifu waliponyanyaswa kikatili, wakidumisha uaminifu wao hadi kifo.

Wapya katika kutaniko la Yerusalemu, ambao huenda walikuwa Wakristo baada ya mnyanyaso mkali kupungua, hawakuwahi kupatwa na majaribu makali kama hayo. (Matendo 7:54-60; 12:1, 2; Waebrania 13:7) Hata hivyo, baadhi yao walivunjwa moyo na majaribu madogo-madogo na wakaacha kuendelea katika shindano; ‘wakachoka na kuzimia katika nafsi zao.’ (Waebrania 12:3) Walihitaji kufanya maendeleo kufikia ukomavu, ili wawe na uwezo wa kuvumilia lolote ambalo huenda lingewapata, hata kama lingehusisha kuumizwa kimwili hata kufikia kifo.—Waebrania 6:1; 12:7-11.

Katika nyakati za kisasa, Wakristo wengi ‘wamekinza hadi damu,’ na wameuawa kwa sababu ya kukataa kuacha Ukristo. Badala ya kuruhusu maneno ya Paulo kwenye Waebrania 12:4 yatutie hofu, yanapaswa kutufanya tuazimie kudumisha uaminifu wetu kwa Mungu hadi kifo. Baadaye katika barua hiyohiyo kwa Waebrania, Paulo aliandika: “Acheni sisi tuendelee kuwa na fadhili isiyostahiliwa, ambayo kupitia hiyo twaweza kumtolea Mungu katika njia ya kukubalika utumishi mtakatifu kwa hofu ya kimungu na kicho.”—Waebrania 12:28.