Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Hawana Watoto?

Kwa Nini Hawana Watoto?

Kwa Nini Hawana Watoto?

DELE na Fola, * ambao ni mume na mke, waliishi na kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society nchini Nigeria. Muda mfupi baada ya kuanza kutumikia huko, mama ya Fola alikuja kuwatembelea. Alikuwa amesafiri kutoka mbali ili kuja kuzungumzia jambo lililomhangaisha sana, jambo ambalo mara nyingi lilimkosesha usingizi usiku.

“Mnanifanyia mambo mazuri,” akawaambia. “Nyinyi hunitumia zawadi na kunitembelea. Wonyesho huo wa upendo ni wenye thamani kubwa kwangu. Lakini jambo hilo hunitia wasiwasi pia ninapojiuliza ni nani atakayewafanyia mambo hayo mtakapofikia umri wangu? Mmeoana kwa miaka miwili sasa, na hamna watoto. Je, hamwoni kwamba wakati umefika wa kuondoka Betheli na kupata watoto?”

Mama alisababu hivi: Dele na Fola wametumikia Betheli kwa muda wa kutosha. Sasa ndio wakati wa kufikiria wakati wao ujao. Bila shaka watu wengine wanaweza kufanya kazi yao. Dele na Fola hawahitaji kuacha huduma ya wakati wote, lakini wanaweza kufanya utumishi wa aina nyingine ambao utawawezesha kupata watoto na kufurahia kuwa wazazi.

Hangaiko la Mama

Hangaiko la mama linaeleweka. Tamaa ya kuzaa watoto ni ya asili na ya kawaida katika tamaduni zote na nyakati zote. Kuzaa watoto hutokeza furaha na matumaini makubwa. “Uzao wa tumbo ni thawabu,” yasema Biblia. Naam, uwezo wa kuzaa watoto ni zawadi yenye thamani kubwa kutoka kwa Muumba wetu mwenye upendo.—Zaburi 127:3.

Katika jamii nyingi, watu waliooana hushinikizwa sana na jamii wazae watoto. Kwa mfano, nchini Nigeria, ambako mwanamke wa kawaida huzaa watoto sita, ni jambo la kawaida kwenye arusi kusikia watu wanaowatakia mema maarusi wakisema: “Miezi tisa kuanzia sasa, tunatarajia kusikia mtoto akilia nyumbani kwenu.” Maarusi wanaweza kupewa kitanda cha mtoto kikiwa zawadi ya arusi. Mama-wakwe hutazama kalenda kwa makini. Ikiwa bibi-arusi hatashika mimba katika muda wa mwaka mmoja hivi, wanachunguza waone kama kuna tatizo wanaloweza kusaidia kutatua.

Kwa maoni ya akina mama wengi, watu huoana kusudi wazae watoto na kuendeleza ukoo wa familia. Mama ya Fola alimwuliza: “Kwa nini uliolewa kama hutapata watoto? Ulizaliwa na mtu; wewe pia zaa watoto wako mwenyewe.”

Mbali na kuzaa, kuna mambo mengine yafaayo kufikiriwa. Katika mataifa mengi ya Afrika, serikali hazina maandalizi mengi ya kuwatunza wazee. Kwa kawaida, watoto ndio hutunza wazazi wao waliozeeka, kama vile wazazi hao walivyowatunza walipokuwa wachanga. Kwa hiyo, mama ya Fola alisababu kwamba watoto wake wasipopata watoto wao wenyewe, miaka ya baadaye wangekuwa wapweke, wasiotakwa, na maskini, bila mtu wa kuwazika wakifa.

Katika sehemu nyingi za Afrika, kutokuwa na watoto huonwa kuwa laana. Katika sehemu nyingine, wanawake hata hutakiwa wathibitishe wanaweza kuzaa kabla ya kuolewa. Wanawake wengi wasioweza kupata mimba hutafuta dawa na matibabu kwa bidii sana, wakijaribu kumaliza hali yao ya utasa.

Kwa sababu ya mitazamo hiyo, watu waliooana wanaokataa kimakusudi kupata watoto, huonwa kuwa wanajinyima kitu chenye manufaa. Mara nyingi wao huonwa kuwa watu wasio wa kawaida, wasiofikiria wakati ujao, na wa kusikitikiwa.

Furaha na Wajibu

Watu wa Yehova wanatambua kwamba kuna furaha na wajibu pia katika kulea watoto. Biblia yasema hivi kwenye 1 Timotheo 5:8: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii kitu wale walio wake mwenyewe, na hasa kwa ajili ya wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.”

Ni lazima wazazi waandalie familia zao kimwili na kiroho pia, jambo ambalo huchukua wakati na jitihada nyingi. Hawana mtazamo wa kusema kwamba Mungu ndiye mwenye wajibu wa kuwatunza watoto kwa kuwa yeye ndiye aliyewapa. Wanatambua kwamba kulea watoto kulingana na kanuni za Biblia ni wajibu wa wakati wote ambao wazazi wamepewa na Mungu; haupaswi kuachiwa watu wengine.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

Kazi ya kulea watoto ni ngumu hasa katika ‘siku hizi za mwisho’ ambazo ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Hali za uchumi unaozorota na pia hali ya kutomcha Mungu inayozidi kuikumba jamii hufanya iwe vigumu zaidi kulea watoto leo. Hata hivyo, kotekote ulimwenguni, Wakristo wengi waliooana wanakabiliana na magumu hayo na wanalea watoto wanaomcha Mungu “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Yehova huwapenda na kuwabariki wazazi hao kwa kazi yao ngumu.

Sababu Inayofanya Wengine Wasipate Watoto

Kwa upande mwingine, Wakristo wengi waliooana hawana watoto. Wengine ni tasa, lakini hawaasilishi watoto. Wengine wanaoweza kuzaa huamua wasifanye hivyo. Watu hao waliooana hawaamui wasipate watoto kwa sababu hawataki kuwajibika au kwa sababu wanaogopa kukabiliana na magumu ya kulea watoto. Badala yake, wameazimia kuzingatia kabisa sehemu mbalimbali za huduma ya wakati wote ambazo kulea watoto kungefanya isiwezekane kuzizingatia. Baadhi yao ni mishonari. Wengine humtumikia Yehova katika kazi ya kusafiri au katika Betheli.

Wao, kama Wakristo wote, hutambua kwamba kuna kazi ya hima ya kufanya. Yesu alisema: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” Kazi hiyo inafanywa leo. Ni kazi muhimu kwa kuwa “mwisho” utamaanisha kuharibiwa kwa wale wasiosikiliza habari njema.—Mathayo 24:14; 2 Wathesalonike 1:7, 8.

Wakati wetu wafanana na wakati Noa na familia yake walipojenga safina kubwa ambayo iliwahifadhi katika Furiko kubwa. (Mwanzo 6:13-16; Mathayo 24:37) Ingawa wana wote watatu wa Noa walikuwa wameoa, hakuna aliyepata mtoto hadi baada ya Gharika. Huenda walifanya hivyo kwa sababu walitaka kuzingatia kabisa na pia kutumia nguvu zao zote kufanya kazi waliyokuwa nayo wakati huo. Huenda sababu nyingine ikawa kwamba hawakutaka kupata watoto katika ulimwengu ulioshuka hadhi na wenye jeuri ambapo ‘maovu ya mwanadamu yalikuwa makubwa na kwamba kila kusudi alilowaza moyoni mwake lilikuwa baya tu sikuzote.’—Mwanzo 6:5.

Ingawa jambo hilo halimaanishi kwamba ni makosa kupata watoto leo, Wakristo wengi waliooana huepuka kupata watoto ili kujihusisha kabisa na kazi ya hima ambayo Yehova amewapa watu wake waifanye. Watu wengine waliooana wamengoja kwa muda kabla ya kupata watoto; wengine wameamua wasipate watoto na wanafikiria uwezekano wa kuzaa watoto katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu. Je, kufanya hivyo ni kutofikiria wakati wao ujao? Je, kuna kitu wanachokosa maishani? Je, wasikitikiwe?

Maisha Salama na Yenye Furaha

Ndoa ya Dele na Fola, waliotajwa hapo awali, sasa imedumu kwa zaidi ya miaka kumi, na bado wameamua kuendelea bila watoto. “Jamaa zetu bado hutushinikiza tupate watoto,” asema Dele. “Hangaiko lao kubwa ni usalama wetu wa wakati ujao. Sikuzote sisi huwashukuru kwa kuwa wanatujali, lakini sisi huwaeleza kwa busara kwamba tunafurahia tunachofanya. Kuhusu usalama, sisi huwaambia kwamba tunamtumaini Yehova, ambaye anajali hali njema ya wote wale wanaodumu wakiwa waaminifu-washikamanifu kwake. Pia sisi huwaeleza kwamba kupata watoto si uhakikisho kwamba watoto hao watawatunza wazazi wao watakapokuwa wazee. Watoto wengine hawawajali wazazi wao, wengine hawana uwezo wa kuwasaidia, na bado wengine hufa kabla ya wazazi wao. Kwa upande mwingine, wakati wetu ujao ni hakika tukiwa na Yehova.”

Dele na wengine kama yeye hutumaini ahadi hii ya Yehova kwa watumishi wake waaminifu: “Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.” (Waebrania 13:5) Pia wanaamini kwamba “mkono wa BWANA haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia.”—Isaya 59:1.

Sababu nyingine ya kuwa na hakika yatokana na kuona jinsi Yehova anavyotegemeza watumishi wake waaminifu. Mfalme Daudi aliandika: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa.” Fikiria hilo. Je, unajua mtumishi yeyote wa Yehova ambaye “ameachwa”?—Zaburi 37:25.

Badala ya kukumbuka yaliyopita kwa majuto, wale waliotumia maisha yao wakimtumikia Yehova na Wakristo wenzao huridhika wanapoukumbuka wakati huo. Ndugu Iro Umah amekuwa mtumishi wa wakati wote kwa miaka 45 na sasa anatumikia akiwa mwangalizi asafiriye nchini Nigeria. Yeye asema: “Ingawa mimi na mke wangu hatuna watoto, tunakumbuka kwamba sikuzote Yehova ametutunza kiroho na kimwili. Hatujapungukiwa na chochote. Hatatuacha tunapozeeka. Miaka hiyo ya utumishi wa wakati wote imekuwa ndiyo yenye furaha zaidi maishani mwetu. Tunashukuru kwamba tunaweza kuwatumikia ndugu zetu, nao wanathamini utumishi wetu, na hutusaidia.”

Ingawa watu wengi waliooana hawakuzaa watoto wa kimwili, wamezaa watoto wa aina nyingine: Wanafunzi Wakristo wanaomwabudu Yehova. Mtume Yohana alikuwa na umri upatao miaka 100 alipoandika: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 4) Uaminifu wa “watoto” wa Yohana—aliowafunza “kweli”—ulimletea furaha kubwa.

Watu hupata furaha kama hiyo leo. Bernice, ambaye ni Mnigeria, aliolewa miaka 19 iliyopita na ameamua asipate watoto. Kwa miaka 14 iliyopita, ametumikia akiwa painia. Anapokaribia ule wakati maishani ambapo haitawezekana kuzaa watoto wake mwenyewe, hajuti kutumia maisha yake katika kufanya wanafunzi. Yeye asema: “Ninafurahi kuona watoto wangu wa kiroho wakikua. Hata kama ningalikuwa na watoto wangu mwenyewe, sina hakika kama wangalikuwa na ukaribu zaidi na mimi kuliko wale ambao nimesaidia kujifunza kweli. Wao huniona kama mama yao mzazi, nao huzungumza nami mambo yenye kuwafurahisha na matatizo yao na kuniomba ushauri. Wao huniandikia barua, nasi hutembeleana.

“Wengine huona ni laana kutozaa watoto wako mwenyewe. Wanasema kwamba utateseka uzeeni. Lakini mimi nina maoni tofauti. Ninajua kwamba maadamu namtumikia Yehova kwa nafsi yote, atanithawabisha na kunitunza. Hatanitupa kamwe nitakapokuwa mzee.”

Mungu Anawapenda na Kuwathamini

Wale ambao wamezaa na wamelea watoto ambao “waendelea kutembea katika kweli” wana sababu nyingi za kushukuru. Si ajabu kwamba Biblia husema: “Baba yake mwenye haki atashangilia; naye amzaaye mtoto mwenye hekima atamfurahia. Na wafurahi baba yako na mama yako; na afurahi aliyekuzaa”!—Mithali 23:24, 25.

Wakristo ambao hawakupata furaha ya kuzaa watoto wamebarikiwa katika njia nyinginezo. Wengi wa Wakristo hao waliooana wametimiza fungu muhimu katika kuendeleza masilahi ya Ufalme kwa njia kubwa. Kwa miaka iliyopita, wamepata uzoefu, hekima, na ustadi unaowawezesha kusaidia kwa njia kubwa kazi ya Ufalme. Wengi wako katika mstari wa mbele katika kazi hiyo.

Ingawa hawakupata watoto kwa sababu ya masilahi ya Ufalme, Yehova amewabariki kwa kuwapa familia yenye upendo ambayo huthamini sana jinsi ambavyo wamejidhabihu. Ni kama vile Yesu alivyosema: “Hakuna ambaye ameacha [kihalisi, “ameachilia mbali”] nyumba au akina ndugu au akina dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara mia sasa katika kipindi hiki cha wakati, nyumba na akina ndugu na akina dada na akina mama na watoto na mashamba . . . na katika mfumo wa mambo unaokuja uhai udumuo milele.”—Marko 10:29, 30.

Wale wote walio waaminifu ni wenye thamani kama nini kwa Yehova! Waaminifu-washikamanifu hao wote, wale walio na watoto na pia wale wasio na watoto, wanahakikishiwa hivi na mtume Paulo: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu na mwaendelea kuhudumu.”—Waebrania 6:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Watu waliooana ambao hawana watoto wamebarikiwa kwa kupewa familia ya kiroho yenye upendo