Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha “Sheria ya Fadhili” Ikuchochee

Acha “Sheria ya Fadhili” Ikuchochee

LISA a anasema hivi: “Jambo lililonichochea zaidi ni jinsi ndugu na dada walivyonionyesha fadhili.” Alikuwa akizungumzia jambo lililomvutia kujifunza kweli. Ndivyo ilivyokuwa pia kwa Anne, aliyesema hivi: “Nilivutiwa zaidi na fadhili walizonionyesha kuliko mafundisho yao.” Sasa dada hao wawili wanafurahia kusoma na kutafakari Biblia, lakini walichochewa sana na fadhili walizoonyeshwa.

Tunaweza kuonyeshaje fadhili na hivyo kugusa mioyo ya watu wanaotuzunguka? Acheni tuzungumzie njia mbili, kupitia ulimi wetu na kupitia matendo yetu. Kisha, tutazungumzia tunapaswa kuwaonyesha nani fadhili.

“SHERIA YA FADHILI” KWENYE ULIMI WAKO

Mwanamke mwenye uwezo anayetajwa katika Methali sura ya 31 ana “sheria ya fadhili” kwenye ulimi wake. (Met. 31:26) Anairuhusu “sheria” hiyo iongoze mambo anayosema na jinsi anavyoyasema. Akina baba pia wanapaswa kuwa na “sheria” hii kwenye ulimi wao. Wazazi wengi wanajua vizuri sana kwamba maneno makali yanaweza kumwathiri kwa njia mbaya mtoto wao. Ikiwa wazazi watazungumza kwa ukali bila hisia, inaelekea mtoto wao hatasikiliza mambo wanayosema. Hivyo, wazazi wanapozungumza kwa fadhili, itakuwa rahisi zaidi kwa watoto wao kuwasikiliza na kuwatii.

Iwe wewe ni mzazi au la, unaweza kuzungumzaje kwa fadhili? Tunapata dokezo kwenye sehemu ya kwanza ya andiko la Methali 31:26 linalosema: “Hufumbua kinywa chake kwa hekima.” Hilo linahusisha kuchagua maneno kwa uangalifu na kuzungumza kwa hekima. Mara nyingi ni vizuri kujiuliza hivi: ‘Je, maneno ninayotaka kusema yatachochea hasira au yataleta amani?’ (Met. 15:1) Naam, ni jambo la hekima kufikiria kabla ya kuzungumza.

Methali nyingine inasema hivi: “Maneno yanayosemwa bila kufikiri huchoma kama upanga.” (Met. 12:18) Tunapofikiria jinsi maneno yetu na njia yetu ya kusema inavyowaathiri wengine, inaelekea tutaweza kudhibiti maneno yanayotoka kinywani mwetu. Naam, kutumia “sheria ya fadhili” kutatusaidia kuepuka kusema maneno yanayoumiza na kwa ukali. (Efe. 4:31, 32) Tutaondoa akilini mawazo yasiyofaa na badala yake kuzungumza kwa njia inayojenga, na kwa uchangamfu. Yehova aliweka mfano mzuri kuhusiana na hilo, alipomwimarisha mtumishi wake Eliya aliyekuwa anaogopa. Malaika aliyemwakilisha Yehova alizungumza naye kwa “sauti tulivu, ya chini.” (1 Fal. 19:12) Hata hivyo, kuwa na fadhili kunahusisha mengi zaidi ya kuzungumza tu kwa fadhili. Ni lazima pia tuonyeshe matendo ya fadhili. Jinsi gani?

MATENDO YA FADHILI HUWACHOCHEA WENGINE

Tunamwiga Yehova tunapozungumza na kutenda kwa fadhili. (Efe. 4:32; 5:1, 2) Lisa, aliyenukuliwa awali, alieleza hivi kuhusu fadhili ambazo alionyeshwa na Mashahidi: “Familia yetu ilipolazimika kuhama ghafla, ndugu wawili na wake zao waliomba ruhusa kazini kwao ili kutusaidia kufunga mizigo. Wakati huo sikuwa nimeanza kujifunza Biblia!” Matendo hayo ya fadhili yalimchochea Lisa kuichunguza kwa ukaribu kweli.

Anne, aliyetajwa mwanzoni, alithamini pia fadhili alizoonyeshwa na Mashahidi. Alisema hivi: “Kwa sababu ya hali zilivyo ulimwenguni, niliwatilia shaka watu. Ilikuwa vigumu kwangu kuwaamini watu.” Aliendelea kusema hivi: “Nilipokutana na Mashahidi wa Yehova nilikuwa na shaka kuhusu nia yao. Nilijiuliza, ‘Kwa nini wanapendezwa nami?’ Lakini mwalimu wangu wa Biblia alinionyesha fadhili za kweli, nami nikaanza kumtumaini.” Kulikuwa na matokeo gani mazuri? Anasema hivi: “Baadaye nilianza kukazia fikira mambo niliyokuwa nikijifunza.”

Ona kwamba Lisa na Anne waliguswa sana moyo na matendo ya fadhili kutoka kwa ndugu na dada kutanikoni, na jambo hilo liliwasaidia kuanza kujifunza kweli. Fadhili walizoonyeshwa kutanikoni ziliwasaidia kufungua mioyo yao.

JIFUNZE KUWAONYESHA WENGINE FADHILI KWA KUMWIGA MUNGU

Huenda baadhi ya watu wanatumia maneno yenye fadhili na wanatabasamu kwa sababu ya utamaduni na malezi yao. Tabia hizo nzuri zinazotokana na desturi au utamaduni zinafaa. Lakini ikiwa tunafanya hivyo kwa sababu tu ya utamaduni wetu, huenda hatuonyeshi fadhili inayotoka kwa Mungu.​—Linganisha Matendo 28:2.

Fadhili ya kweli inayotoka kwa Mungu ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Hivyo, kusitawisha fadhili kunahusisha kukubali kuongozwa na roho takatifu ya Mungu. Kufanya hivyo, kunapatana na tamaa yetu ya kumwiga Yehova na Yesu. Na tukiwa Wakristo, tunapendezwa sana na wengine. Hivyo, tunachochewa na upendo wetu kwa Yehova Mungu na pia kwa wanadamu wenzetu. Basi, tunatokeza sifa yenye nguvu ya fadhili inayotoka moyoni na ambayo inamfurahisha Mungu.

TUNAPASWA KUWAONYESHA NANI FADHILI?

Inaweza kuwa rahisi kuwaonyesha fadhili wale ambao wametuonyesha fadhili au wale tunaowafahamu. (2 Sam. 2:6) Njia moja tunayofanya hivyo ni kwa kuwashukuru. (Kol. 3:15) Lakini namna gani ikiwa tunahisi kwamba mtu fulani hastahili kuonyeshwa fadhili?

Fikiria hili: Yehova ametuwekea mfano bora wa jinsi ya kuonyesha fadhili zisizostahiliwa, na Neno lake linatufundisha somo muhimu kuhusu jinsi ya kuonyesha sifa hiyo. Usemi “fadhili zisizostahiliwa” umetumiwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Mungu anatuonyeshaje fadhili?

Fikiria mamilioni ya watu ambao Yehova amewaonyesha fadhili zake kwa kuwaandalia mambo wanayohitaji ili waendelee kuwa hai. (Mt. 5:45) Isitoshe, hata kabla ya wanadamu kumjua Yehova aliwaonyesha fadhili. (Efe. 2:4, 5, 8) Kwa mfano, aliwapatia wanadamu wote zawadi bora kabisa, yaani, Mwana wake mzaliwa-pekee. Mtume Paulo aliandika kwamba Yehova aliandaa fidia “kulingana na utajiri wa fadhili zake zisizostahiliwa.” (Efe. 1:7) Zaidi ya hilo, ingawa tunatenda dhambi na kumkasirisha Yehova, anaendelea kutuongoza na kutufundisha. Mafundisho na maneno yake ni kama “mvua ya rasharasha.” (Kum. 32:2) Bila shaka, hatuwezi kumlipa kikamili kwa fadhili zake zote anazotuonyesha. Na ukweli ni kwamba wakati wetu ujao unategemea fadhili za Yehova.​—Linganisha 1 Petro 1:13.

Bila shaka, tunavutiwa na kuchochewa na fadhili za Yehova. Matokeo yake ni kwamba badala ya kuwaonyesha watu wachache fadhili, tunajitahidi kumwiga Yehova kwa kuwa na mazoea ya kuonyesha fadhili kila siku. (1 The. 5:15) Tunapoonyesha fadhili kwa ukawaida, tutakuwa kama joto la moto wakati wa baridi. Tutawafariji watu wetu wa familia, waabudu wenzetu, wafanyakazi wenzetu, wanafunzi wenzetu, na jirani zetu.

Wafikirie watu wa familia yako au katika kutaniko watakaoimarishwa na maneno na matendo yako ya fadhili. Huenda kuna mtu fulani kutanikoni ambaye hasa anahitaji msaada wa kutunza nyumba na bustani yake, au kusaidiwa shughuli za kawaida kama vile kufanya ununuzi. Pia, ikiwa utakutana na mtu fulani katika huduma anayehitaji msaada, je, unaweza kumsaidia kwa njia fulani hususa?

Acheni tumwige Yehova, na sikuzote maneno na matendo yetu yaongozwe na “sheria ya fadhili.”

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.