Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Ni jambo gani lisilo la kawaida ambalo Yesu aliwatendea wagonjwa wa ukoma?

Wayahudi wa kale waliogopa ugonjwa wa ukoma ambao uliwasumbua watu wengi nyakati za Biblia. Ugonjwa huo hatari ungeweza kushambulia mfumo wa neva wa mgonjwa na kumsababishia madhara ya kudumu na ulemavu. Wakati huo hakukuwa na tiba ya ugonjwa wa ukoma. Hivyo, watu waliougua ugonjwa huo walitengwa na jamii na waliamriwa kuwatahadharisha wengine kuhusu hali yao.—Mambo ya Walawi 13:45, 46.

Viongozi wa dini ya Kiyahudi walitunga sheria kuhusu watu wenye ukoma ambazo zilitofautiana sana na yale ambayo Maandiko husema, hivyo walifanya maisha ya watu wenye ukoma kuwa magumu sana. Kwa mfano, sheria za marabi zilisema kwamba mtu alipaswa kuwa umbali wa futi 6 kutoka kwa mgonjwa wa ukoma. Lakini ikiwa kungekuwa na upepo unaovuma, mgonjwa wa ukoma alipaswa kuwa umbali wa futi 150 hivi. Vitabu fulani vya Talmud vilieleza kwamba sheria ya Maandiko kuhusu watu wenye ukoma kuishi “nje ya kambi,” ilimaanisha kwamba watu hao walipaswa kuishi nje ya jiji. Hivyo, rabi mmoja alipomwona mtu mwenye ukoma ndani ya jiji, alimtupia mawe na kusema: “Nenda mahali pako, usije ukawatia unajisi watu wengine.”

Yesu alitenda kwa njia tofauti kabisa! Badala ya kuwafukuza watu wenye ukoma, kwa hiari aliwagusa na hata kuwaponya.—Mathayo 8:3.

Viongozi wa dini ya Kiyahudi waliruhusu talaka kwa msingi gani?

Cheti cha talaka cha mwaka wa 71/72 W.K.

Viongozi wengi wa dini wa karne ya kwanza W.K. walibishana kuhusu msingi wa kutoa talaka. Wakati fulani, baadhi ya mafarisayo walimjaribu Yesu kwa kumuuliza hivi: “Je, ni halali mwanamume kumtaliki mke wake kwa kila sababu?”—Mathayo 19:3.

Sheria ya Musa ilimruhusu mwanamume kumtaliki mke wake ikiwa “amepata kitu fulani kisichofaa katika mwanamke huyo.” (Kumbukumbu la Torati 24:1) Katika siku za Yesu, kulikuwa na shule mbili za kirabi zilizokuwa na maoni yaliyotofautiana kuhusu ufafanuzi wa sheria hiyo. Shammai, shule iliyokuwa na msimamo mkali, ilifafanua kwamba msingi pekee wa kutoa talaka ni “upotovu wa maadili,” yaani, uzinzi. Kwa upande mwingine, shule ya Hillel ilifafanua kuwa mwanamume anaweza kumtaliki mke wake kwa sababu yoyote ile, hata kwa sababu ndogo tu. Kulingana na shule hii, mume angeweza kumtaliki mke wake ikiwa ameunguza chakula au iwapo angepata mwanamke mwingine ambaye ni mrembo zaidi.

Lakini Yesu alijibu jinsi gani swali aliloulizwa na Mafarisayo? Alisema hivi waziwazi: “Mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati, anafanya uzinzi.”—Mathayo 19:6, 9.