Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukweli Kuhusu Wakati Ujao

Ukweli Kuhusu Wakati Ujao

Je, umewahi kuwazia wakati wetu ujao utakuwaje? Biblia inaonyesha kwamba matukio muhimu ambayo yatawaathiri wanadamu wote duniani yatatokea hivi karibuni.

Yesu alifafanua jinsi ambavyo tungejua “kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia.” (Luka 21:31) Alitabiri kwamba, pamoja na mambo mengine mengi, kungekuwa na vita, matetemeko makubwa ya ardhi, upungufu wa chakula na magonjwa​—hayo ndiyo mambo tunayoshuhudia yakitukia leo.​——Luka 21:10-17.

Biblia inaongezea kusema kwamba katika siku za mwisho za utawala wa mwanadamu, watu wangejiendesha vibaya. Unaweza kusoma mambo hayo kwenye 2 Timotheo 3:1-5. Unapojionea mitazamo na matendo ya watu leo, bila shaka unakubali kwamba unabii huu unapatana kabisa na mambo yanayotukia katika siku zetu.

Hilo linamaanisha nini? Hivi karibuni, Ufalme wa Mungu utafanya mabadiliko makubwa ambayo yataboresha maisha duniani. (Luka 21:36) Katika Biblia, Mungu anaahidi kufanya mambo mazuri duniani na kwa ajili ya watu watakaoishi ndani yake. Acheni tuzungumzie mifano michache.

UTAWALA BORA

“Naye akapewa utawala, heshima, na ufalme, ili watu wa makabila, mataifa, na lugha zote wamtumikie. Utawala wake ni utawala wa milele ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake hautaangamizwa.”​DANIELI 7:14.

Hilo linamaanisha hivi: Unaweza kufurahia maisha chini ya serikali bora ambayo imesimamishwa na Mungu na amemweka rasmi Mwana wake awe Mfalme.

AFYA BORA

“Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”​ISAYA 33:24.

Hilo linamaanisha hivi: Hutakuwa mgonjwa tena wala kuwa mlemavu; kifo hakitakuwapo tena.

AMANI YA KUDUMU

“Anakomesha vita katika dunia yote.”​ZABURI 46:9.

Hilo linamaanisha hivi: Hakutakuwa tena na tishio la vita wala madhara yanayotokana na vita.

DUNIA ITAJAA WATU WAZURI

“Watu waovu hawatakuwepo tena . . . Wapole wataimiliki dunia.”​ZABURI 37:10, 11.

Hilo linamaanisha hivi: Hakutakuwa tena na watu waovu; ni wale tu walio tayari kumtii Mungu ndio watakaoishi duniani.

DUNIA NZIMA ITAKUWA PARADISO

“Watajenga nyumba na kuishi ndani yake, nao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.”​ISAYA 65:21, 22.

Hilo linamaanisha hivi: Dunia nzima itakuwa maridadi sana. Mungu atajibu sala zetu kwamba mapenzi yake yatendeke hapa “duniani.”​—Mathayo 6:10