Mimi Ni Nani?

Mimi Ni Nani?

Vijana Huuliza

Mimi Ni Nani?

Michael anamwona Brad akija, na anahofia kitakachotukia. “Sema Mikey, hebu onja!” Brad anasema. Brad anapofungua mkono wake, Michael anaona kitu alichojua ataona—msokoto wa bangi. Hataki kuukubali, lakini pia hataki kudharauliwa na vijana wenzake. Michael anasema kwa woga, “Si leo, labda wakati mwingine. . . . Sawa?”

Jessica anamwona Brad akija, na yuko tayari kwa ajili ya kitakachotukia. “Sema, Jess, hebu onja!” Brad anasema. Brad anapofungua mkono wake, Jessica anaona kitu alichojua ataona—msokoto wa bangi. “Hapana, sitaki,” Jessica anamjibu kwa ujasiri. “Nina mipango fulani ya wakati ujao na hivyo sitaki kuhatarisha afya yangu. Pia, Brad, . . . Mtu mwenye akili timamu hawezi kuvuta bangi!”

KATIKA visa vilivyotajwa hapo juu, kwa nini Jessica anaweza kufaulu kukabiliana msongo huo? Kwa sababu ana kitu ambacho Michael hana. Unajua ni nini? Ni kitambulisho. Si eti ana kadi inayoonyesha jina na picha yake. Kitambulisho hicho ni hisia ya ndani inayokutambulisha wewe ni nani na unaongozwa na viwango gani. Unapokuwa na kitambulisho hicho, unakuwa na nguvu za kushinda majaribu na hivyo kudhibiti maisha yako badala ya kuacha wengine wayadhibiti. Unaweza kukuza uwezo huo jinsi gani? Huenda kwanza ikafaa kujibu maswali yafuatayo.

1 NINA SIFA GANI NZURI?

Kwa nini ni muhimu: Kujua uwezo wako na sifa zako nzuri kutafanya ujiamini zaidi.

Fikiria hili: Kila mmoja wetu ana vipawa mbalimbali. Kwa mfano, watu fulani wana kipawa katika uchoraji au muziki, ilhali wengine wana uwezo mzuri katika michezo. Raquel, anajua sana kurekebisha magari. * Anasema, “Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilitambua kuwa nilitaka kuwa mekanika.”

Mfano katika Biblia: Mtume Paulo aliandika: “Hata kama sina ustadi wa kusema, hakika sivyo nilivyo katika ujuzi.” (2 Wakorintho 11:6) Kwa kuwa aliyafahamu Maandiko vizuri, Paulo alifaulu kubaki imara alipopingwa na watu wengine. Hakuruhusu maoni yao yasiyofaa yadhoofishe imani yake.—2 Wakorintho 10:10; 11:5.

Jichunguze. Hapa chini, andika kipawa au ustadi ulio nao.

․․․․․

Sasa eleza kuhusu sifa fulani nzuri uliyo nayo. (Kwa mfano, wewe huwajali wengine? ni mkarimu? mwenye kutegemeka? unatunza wakati?)

․․․․․

“Mimi hujaribu kuwasaidia watu. Ikiwa mtu fulani anataka kuzungumza nami, hata kama nina shughuli nyingi mimi huacha jambo ninalofanya na kumsikiliza.”Brianne.

Ikiwa ni vigumu kwako kutaja sifa uliyo nayo, fikiria sifa moja ambayo zamani ulikuwa nayo ulipokuwa mtoto lakini sasa umeiacha baada ya kukomaa, na uiandike hapa chini.—Ili upate mifano kadhaa, ona sanduku  “Vijana Wenzako Wanasema Nini?”

․․․․․

2 NINA UDHAIFU GANI?

Kwa nini ni muhimu: Kama vile tu ni rahisi kwa mnyororo kukatika ikiwa una kiunganishi fulani dhaifu, ndivyo pia utambulisho wako unavyoweza kuharibika ikiwa utaruhusu udhaifu wako udhibiti maisha yako.

Fikiria hili: Hakuna mtu ambaye hana dhambi. (Waroma 3:23) Kila mmoja wetu ana udhaifu fulani ambao angependa kuushinda. Msichana mmoja anayeitwa Seija anauliza, “Kwa nini mimi hukasirishwa na mambo madogo-madogo? Hata jambo dogo sana hunikasirisha, nami hushindwa kudhibiti hisia zangu!”

Mfano katika Biblia: Paulo alitambua udhaifu wake. Aliandika hivi: “Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi.”—Waroma 7:22, 23.

Jichunguze. Ni udhaifu gani unaohitaji kuushinda?

․․․․․

“Nimegundua kwamba kila ninapotazama video za kimahaba, ninatamani kuanzisha urafiki wa kimapenzi. Kwa hiyo, sasa ninajua ninapaswa kuwa mwangalifu sana ninapochagua burudani ya aina hiyo.”—Bridget.

3 NINA MIRADI GANI?

Kwa nini ni muhimu: Unapojiwekea miradi, maisha yako yanakuwa na mwelekeo na kusudi. Pia, utaweza kuepuka watu na hali ambazo huenda zikakuzuia kutimiza mambo ambayo umeamua kutimiza.

Fikiria hili: Je, unaweza kuingia ndani ya teksi na kumwomba dereva wa gari hilo aendeshe akizunguka jengo moja hadi mafuta yaishe? Huo ni ujinga—na pia kutakugharimu sana! Miradi humsaidia mtu awe na mwelekeo maishani. Unakuwa na mahali pa kwenda na unapanga jinsi utakavyofika huko.

Mfano katika Biblia: Paulo aliandika hivi: “Jinsi ninavyokimbia si bila uhakika.” (1 Wakorintho 9:26) Badala ya kuishi bila mwelekeo, Paulo alijiwekea miradi na akajaribu sana kuifikia.—Wafilipi 3:12-14.

Jichunguze. Hapa chini andika miradi mitatu ambayo ungependa kutimiza kufikia mwaka ujao.

1 ․․․․․

2 ․․․․․

3 ․․․․․

Sasa chagua mradi ambao unaona ukiwa muhimu zaidi kwako, kisha uandike kile unachoweza kufanya sasa hivi ili uanze kuufikia.

․․․․․

“Nisipokuwa na mengi ya kufanya, mimi hujipata nikifanya mambo bila mwelekeo. Ni afadhali uwe na miradi maishani halafu utie bidii kuifikia.”José.

4 NINA MSIMAMO GANI?

Kwa nini ni muhimu: Bila kuwa na msimamo, maamuzi yako hayatakuwa imara. Kama tu kinyonga, utabadili msimamo wako kila mara ili ukubaliwe na vijana wenzako—ishara ya wazi ya kwamba huna utambulisho wako mwenyewe.

Fikiria hili: Biblia inawahimiza Wakristo ‘wajihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’ (Waroma 12:2) Ikiwa matendo yako yanategemea msimamo wako ulio thabiti, huwezi kuyumbishwa—bila kujali wengine wanafanya nini.

Mfano katika Biblia: Alipokuwa kijana, nabii Danieli “aliazimia moyoni mwake” kwamba angetii sheria za Mungu, ingawa alikuwa ametenganishwa na familia yake na waabudu wenzake. (Danieli 1:8) Kwa kufanya hivyo, alidumisha utambulisho wake. Danieli aliishi kulingana na msimamo wake.

Jichunguze. Una msimamo gani? Kwa mfano:

● Unaamini kwamba kuna Mungu? Ikiwa ndivyo, kwa nini unaamini hivyo? Ni uthibitisho gani unaokusadikisha kwamba yeye yuko?

● Unaamini kwamba viwango vya maadili ambavyo Mungu ameweka ni kwa ajili ya faida yako? Ikiwa ndivyo, kwa nini unaamini hivyo? Kwa mfano, nini kinachokusadikisha kwamba kutii sheria za Mungu kuhusu kuepuka kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa kutafanya uwe na furaha zaidi kuliko kuishi “bila kujali” kama vijana wenzako wanavyofanya?

Hayo si maswali ya kujibu upesi tu. Chukua wakati wa kuchunguza sababu zinazofanya uamini hivyo. Unapofanya hivyo, utaweza kutetea imani yako vizuri zaidi.—Methali 14:15; 1 Petro 3:15.

“Shuleni, vijana wanapenda kumdhihaki mtu kuhusu mambo ambayo hana uhakika nayo, na sikutaka kuonekana kuwa sina uhakika kuhusu imani yangu. Kwa hiyo, nilijitahidi kuwa na sababu thabiti za kuitetea imani yangu. Badala ya kuwaambia watu tu, ‘Ah, siwezi kufanya hivyo kwa sababu dini yangu hainiruhusu,’ niliwaeleza kwamba sikutaka kufanya hivyo kwa sababu ‘Sidhani kama ni sawa kufanya hivyo.’ Hivyo ndivyo nilivyoamini.” Danielle.

Hatimaye, ungependa kufananishwa na nini—jani lililoanguka na linalopeperushwa na upepo huku na huku au na mti unaohimili hata dhoruba kali? Ukidumisha utambulisho wako ukiwa thabiti, utakuwa kama mti huo. Na hilo litakusaidia kujibu swali hili, Mimi ni nani?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

  “Kadiri ambavyo nimekua mkubwa, nimejifunza jinsi ninavyoweza kuchanganua mambo ninapofanya maamuzi, iwe ni makubwa au madogo, na pia kuepuka mambo yatakayomkasirisha Mungu.”

“Nilipokuwa mchanga, nilijiambia kwamba ikiwa mtu yeyote alikuwa tofauti na mimi, basi hakuwa mtu wa kawaida. Lakini sasa ninafurahi kwamba kila mtu ni tofauti, na pia ninapendezwa na maoni ya wengine.”

[Picha]

Jeremiah

Jennifer

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Mnaona nina vipawa gani? Ni sifa gani ambazo ninapaswa kufanyia kazi? Ninyi mlifanya nini ili mwe na msimamo thabiti kuhusu viwango ambavyo Mungu ameweka?

[Mchoro katika ukurasa wa 26]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

SIFA NZURI

UDHAIFU

MIRADI

MSIMAMO

[Picha katika ukurasa wa 28]

Unapokuwa na utambulisho thabiti, unakuwa kama mti ulio na mizizi imara unaoweza kuhimili dhoruba kali