Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kuzuiaje Hasira Yangu?

Ninaweza Kuzuiaje Hasira Yangu?

Vijana Huuliza

Ninaweza Kuzuiaje Hasira Yangu?

Wewe hulipuka kwa hasira mara ngapi?

□ Sijawahi

□ Kila mwezi

□ Kila juma

□ Kila siku

Ni nani anayeweza kukufanya ulipuke kwa hasira?

□ Hakuna

□ Wanafunzi wenzangu

□ Wazazi

□ Ndugu na dada zangu

□ Wengine

Hapa chini, eleza hali zinazokufanya ukasirike.

□ ․․․․․

IKIWA utaweka alama ya ✔ kando ya “Sijawahi” na “Hakuna” na usijaze chochote kwenye sehemu ya mwisho, hongera—unaweza kuzuia hasira yako!

Hata hivyo, watu hutenda kwa njia tofauti wanapokuwa chini ya hali ngumu na wana udhaifu mbalimbali. Yakobo, mwandikaji wa Biblia alisema hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yakobo 3:2) Kuhusu hasira, huenda ukawa na maoni kama ya Serena, mwenye umri wa miaka 17. * “Mimi hupandwa na hasira,” anasema, “na mara nyingi mimi humlipukia mtu yeyote anayeniudhi. Inaweza kuwa wazazi wangu, dada yangu, au hata mbwa wangu!”

Kutofautisha Dhana na Mambo Hakika

Je, ni vigumu kwako kudhibiti hasira? Ikiwa ndivyo, unaweza kusaidiwa. Lakini, kwanza acha tukanushe dhana fulani.

Dhana: “Siwezi kuzuia hasira yangu—familia yetu imejaa watu wenye hasira!”

Jambo Hakika: Huenda ukawa na “mwelekeo wa ghadhabu,” labda kwa sababu ya kuathiriwa na watu wa familia, mazingira, au mambo mengine. Lakini wewe ndiye utakayeamua ikiwa utaghadhabika au hutaghadhabika. (Methali 29:22) Lakini swali ni, Je, utaruhusu hisia zako zikuongoze au utazidhibiti? Wengine wamejifunza kuzuia hasira, na wewe pia unaweza kufanya hivyo!—Wakolosai 3:8-10.

Andiko Muhimu: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.”—Waefeso 4:31.

Dhana: “Nikikasirika, ninaona ni afadhali kulipuka kuliko kufungia hasira.”

Jambo Hakika: Kufanya mambo yote mawili kunaweza kudhuru afya yako. Ni kweli kuna wakati wa ‘kuonyesha’ hangaiko lako. (Ayubu 10:1) Lakini je, hilo linamaanisha kwamba unapaswa kutembea kana kwamba uko tayari kulipuka? Unaweza kujifunza kukasirika bila kulipuka.

Andiko Muhimu: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, . . . akiendelea kujizuia.”—2 Timotheo 2:24.

Dhana: “Nikiwa ‘mpole kwa wote,’ kila mtu atanidharau.”

Jambo Hakika: Watu wanajua kwamba ni vigumu sana kujizuia, na watakuheshimu zaidi unapofanya hivyo.

Andiko Muhimu: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—Waroma 12:18.

Dhibiti Hasira Yako

Ikiwa unakasirika haraka, huenda umekuwa ukiwalaumu wengine kwa kufanya ukasirike. Kwa mfano, je, umewahi kusema, “Alinichokoza” au “Alinifanya nilipuke kwa hasira”? Ikiwa ndivyo, maneno yako yanadokeza kwamba wengine wanaongoza hisia zako. Unawezaje kuanza kuzidhibiti? Jaribu mambo yafuatayo.

Tambua daraka lako. Jambo la kwanza ni kutambua kwamba ni wewe tu unayeweza kujikasirisha. Kwa hiyo acha kuwalaumu wengine. Badala ya kusema, “Alinichokoza,” kubali kwamba ‘nilijiruhusu nichokozeke.’ Badala ya kusema “Alinifanya nilipuke kwa hasira,” kubali kwamba ‘niliamua kulipuka.’ Ukikubali kwamba una tatizo, itakuwa rahisi kubadilika. —Wagalatia 6:5.

Fikiria mapema hali zinazoweza kutokea. Biblia inasema: “Mtu mwangalifu huona hatari akajificha, lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.” (Methali 22:3, Biblia Habari Njema) Hivyo, jambo kuu ni kufikiria mapema hali zinazoweza kutokea. Jiulize, ‘Ni wakati gani ambapo yaelekea ni rahisi kwangu kukasirika?’ Kwa mfano, msichana anayeitwa Megan anasema hivi: “Ninafanya kazi usiku, na ninapomaliza, mimi hujihisi mchovu sana. Wakati huo inakuwa rahisi kwangu kukasirika.”

Swali: Ni hali gani zinazoweza kufanya iwe rahisi kwako kukasirika?

․․․․․

Panga utakavyojibu. Unapochokozwa, vuta pumzi ili utulie, zungumza kwa sauti ndogo na polepole. Badala ya kushutumu (“Wewe mwizi! Ulichukua fulana yangu bila kuuliza!”) jaribu kueleza jinsi kitendo hicho kilivyokuathiri. (“Mimi huhisi vibaya ninapotaka kuvaa fulana yangu na kugundua kwamba umeichukua bila kuniuliza.”)

Mazoezi: Fikiria jambo lililotukia hivi karibuni ambalo karibu likukasirishe.

1. Kwa nini ulichokozeka?

․․․․․

2. Ulitendaje? (Ulisema nini na/au ulitendaje?)

․․․․․

3. Ungetendaje kwa njia inayofaa?

․․․․․

Fikiria matokeo. Kuna kanuni kadhaa za Biblia zinazoweza kukusaidia kufanya hivyo. Kwa mfano:

Methali 12:18: “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma.” Maneno yanaweza kuumiza, na unapokasirika ni rahisi sana kusema maneno ambayo utajutia baadaye.

Methali 29:11: “Mtu mjinga huiachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima huituliza mpaka mwisho.” Mwishowe, unaonekana mjinga unapofoka kwa hasira.

Methali 14:30: “Moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.” Hasira ni mbaya kwa afya yako! Msichana anayeitwa Anita alisema hivi: “Familia yetu ina tatizo la kupanda kwa shinikizo la damu, na kwa kuwa mimi hufadhaika kwa urahisi ninakuwa mwangalifu sana nisipandwe na hasira.”

Tunajifunza nini? Fikiria matokeo ya maneno na matendo yako. Heather mwenye umri wa miaka 18 anasema hivi: “Mimi hujiuliza, ‘Vipi nikimkasirikia mtu huyu? Atanionaje? Kufanya hivyo kutaathirije uhusiano wetu? Ningehisije ikiwa mtu angenitendea hivyo?’” Unaweza kujiuliza maswali kama hayo kabla ya kuzungumza au kabla ya kutuma ujumbe iwe ni kwa kumwandikia barua, barua-pepe, kumpigia simu, au kumtumia ujumbe mfupi kupitia kompyuta au simu.

Swali: Kungekuwa na matokeo gani ikiwa mtu angekukasirisha kisha umtumie ujumbe kwa hasira?

․․․․․

Omba msaada. “Chuma hunoa chuma, kadhalika mtu hufundishwa na wenzake,” inasema Methali 27:17. (BHN) Mbona usimwulize mzazi au rafiki yako mkomavu jinsi anavyojidhibiti anapokasirika?

Chunguza maendeleo yako. Andika mambo ili uweze kuchunguza maendeleo yako. Kila wakati unaposhindwa kujidhibiti, andika (1) ni nini kilichotukia, (2) jinsi ulivyotenda, na (3) ungetendaje kwa njia inayofaa. Baada ya muda utaona kwamba unatenda kwa njia hiyo inayofaa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

Nyakati nyingine, hata watu tusiotazamia kwamba wanaweza kukasirika wamefanya hivyo kwa muda. Tunajifunza nini kutokana na mifano ya watu hawa?

▪ Musa.—Hesabu 20:1-12; Zaburi 106:32, 33.

▪ Paulo na Barnaba.—Matendo 15:36-40.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Kuandika hisia zangu au kumwelezea mama yangu hunisaidia kubaki nikiwa mtulivu.”—Alexis, Marekani.

“Nikifadhaika kabisa, kufanya mazoezi ya kutembea ili nitulie na kuwa nje kwenye hewa nzuri hunifanya nifikirie mambo vizuri.”—Elizabeth, Ireland.

“Mimi hujaribu kuondoa jambo hilo akilini na kujiuliza, ‘Itakuwaje nikianza kufoka?’ Sikuzote mimi hutambua kwamba hilo halitasuluhisha mambo!”—Graeme, Australia.

[Sanduku katika ukurasa wa 18]

JE, UNAJUA?

Nyakati nyingine, Mungu hukasirika. Hata hivyo, ana haki ya kukasirika, naye hudhibiti kabisa hasira yake. Hatendi kamwe kwa njia isiyofaa!—Ona Kutoka 34:6; Kumbukumbu la Torati 32:4; na Isaya 48:9.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wewe ndiye utakayeamua hasira yako itachemka kiasi gani