Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Vijana Huuliza . . . Nifanyeje Ikiwa Ndugu Yangu Amejiua? (Juni 2008) Kabla ya kufa, dada yangu mkubwa alikuwa na ugonjwa wa kushuka moyo kwa miaka mitano. Kwa kuwa niliona jinsi alivyoteseka kwa sababu ya ugonjwa huo, nilijiambia, ‘Ana maisha yenye kusikitisha!’ Hata hivyo, makala hiyo ya Amkeni! ilidokeza kwamba tufikirie mambo mazuri tuliyofurahia na aliyekufa. Nilipofikiria mambo niliyofurahia na dada yangu, nilihisi kwamba “hakuwa na maisha yenye kusikitisha” lakini aliishi maisha yenye furaha, kulikuwa na pindi nyingi zenye furaha kuliko pindi zenye magumu.

S. Y., Japani

Vijana Huuliza . . . kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniamini? (Aprili 2008) Kusoma na kufuata kanuni za Biblia zinazopatikana katika Amkeni! kulinifunza kwamba kutegemeka na kukomaa ni kama kupanda ngazi, si mlango ambao unaingia moja kwa moja. Ili nipewe uhuru zaidi, nilihitaji kuwathibitishia wazazi wangu kwamba wanaweza kuniamini. Nilipaswa kumaliza kazi zangu za nyumbani na za shuleni. Asanteni sana kwa makala kama hiyo.

T. L., Marekani

Maisha ya Albino (Julai 2008) Kwa kuwa nina tatizo hilo, mwanzoni nilifurahi kuona makala hiyo. Hata hivyo, nilihuzunika kuona neno “albino” likitumiwa tena na tena katika makala hiyo. Neno hilo limetumiwa kwa njia nyingi zenye kuwashushia heshima watu wenye hali hii.

A. L., Marekani

“Amkeni!” lajibu: Ikiwa kuna msomaji wetu yeyote aliyefadhaishwa tunaomba radhi. Tulitoa neno “albino” kwenye vitabu vya kitiba. Hata hivyo, tunakubali kwamba watu fulani wamelitumia neno hilo kwa njia mbaya. Kwa upande mwingine, maalbino wengi wanalikubali jina hilo na hawaudhiki linapotumiwa. Kwa kweli, hatukukusudia kumwumiza mtu yeyote.

Asanteni sana kwa kuchapisha makala hiyo, kwa kuwa mimi pia ni albino kama John. Nilithamini sana kusoma makala hiyo kuhusu ualbino ambayo imeandikwa kwa njia sahihi, yenye ufikirio, na yenye kuelimisha. Kwa sababu hiyo, rafiki zangu wanaelewa vizuri zaidi hali yangu.

T. M., Marekani

Upendo Wenye Nguvu Kuliko Kimbunga! (Agosti 2008) Makala kama hizi hunikumbusha kwamba sipaswi kuwa na wasiwasi kuhusu wakati ujao bali ninapaswa kumtegemea Mungu zaidi. Miaka mitatu iliyopita nilionyeshwa upendo kama huo wakati nyumba ya wazazi wangu wasio waamini ilipobomolewa na mafuriko. Mashahidi wa Yehova wa kutaniko la eneo hilo waliwasaidia upesi sana. Ninamshukuru sana Yehova kwamba niko katika tengenezo lake.

D. W., Poland

Mhindi—Mmea wa Ajabu (Agosti 2008) Familia yetu ilikuza mahindi katika shamba letu, lakini hatukuvuna mahindi yenye ukubwa uleule. Lakini sasa, baada ya kusoma makala hiyo tunaelewa sababu. Tulikuwa tukipanda aina tano au sita za mbegu, kwa hiyo hazikuwa zikichavushwa kama vile shamba kubwa linavyochavushwa. Mwaka uliopita, tulipochavusha kwa uangalifu nyuzi zote za mahindi, tulivuna mahindi matamu yenye ukubwa uleule. Asanteni sana.

R. W., Japani