Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kupata Wapi Majibu?

Unaweza Kupata Wapi Majibu?

Unaweza Kupata Wapi Majibu?

LENGO moja la dini ni kufundisha kuhusu kusudi la uhai. Hata hivyo, watu wengi wametambua kwamba mahitaji yao ya kiroho hayajatoshelezwa na mafundisho ya dini zao. Denise aliyelelewa na wazazi Wakatoliki, anakumbuka: “Katekisimu ya Baltimore inatia ndani swali hili, ‘Kwa nini Mungu alituumba?’ na inajibu hivi, ‘Mungu alituumba ili kuonyesha wema Wake na kushiriki nasi furaha Yake ya milele mbinguni.’

“Hilo halikunieleza ni kwa nini nipo hapa,” Denise anaendelea. “Ikiwa ninangojea tu kwenda mbinguni, ninapaswa kuwa nikifanya nini sasa?” Watu wengi wana mawazo kama ya Denise. Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba asilimia 66 hivi ya wale waliohojiwa wanaamini kwamba kanisa na masinagogi mengi hayawasaidii watu kupata kusudi maishani.

Kwa sababu hiyo, wanatafuta majibu kwingineko, iwe ni kupitia sayansi au falsafa za aina mbalimbali. Kwa nini watu wanaendelea kutafuta majibu, ingawa ni wachache tu wanaoonekana kupata uradhi?

Tuna Uhitaji wa Kiroho

Dakt. Kevin S. Seybold anasema kwamba kuna “mwelekeo wa wanadamu ulimwenguni pote wa kuabudu kitu fulani.” Katika miaka ya karibuni wanasayansi kadhaa wamefikia mkataa wa kwamba wanadamu wamezaliwa na mwelekeo wa kutafuta kusudi halisi maishani. Watu fulani wanaamini kwamba chembe za urithi na utendaji wa wanadamu unaonyesha kwamba wanadamu wana uhitaji wa asili wa kuwa na uhusiano na nguvu zisizo za kawaida.

Ingawa wasomi wanatilia shaka wazo la kwamba wanadamu wana uhitaji wa kiroho, watu wengi hawahitaji uchunguzi wa kisayansi ili waamini jambo hilo. Ni uhitaji huo wa kiroho ambao hufanya tujiulize yale ambayo watu fulani wameyaita maswali muhimu zaidi: Kwa nini tupo hapa? Tunapaswa kufanya nini na maisha yetu? Je, tunawajibika kwa Muumba Mweza-Yote?

Ukitenga wakati kuchunguza ulimwengu wa asili, utapata baadhi ya majibu ya maswali hayo. Kwa mfano, fikiria vitu vya asili vyenye kutatanisha, kuanzia viumbe vyenye chembe moja hadi makundi ya nyota yaliyo mbali sana angani. Je, havituonyeshi kwamba kuna Mbuni, au Muumba mwenye akili? Biblia inasema hivi: “Kwa maana sifa [za Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba hawana sababu ya kujitetea.”—Waroma 1:20.

Tosheleza Uhitaji Wako wa Kiroho

Biblia inasema hivi kuhusiana na jinsi Mungu alivyowaumba wanadamu: “Ameweka milele vilevile ndani ya mioyo yao.” (Mhubiri 3:11, Zaire Swahili Bible) Tumezaliwa na tamaa ya kuishi, si kufa. Tuna tamaa ya kupata kusudi la maisha, kujua majibu ya maswali.

Kwa hiyo, ni kawaida kwa wanadamu kuuliza maswali. Baada ya kutaja kuhusu maendeleo ya kisayansi na kitekinolojia, mhariri wa jarida The Wall Street Journal aliandika: “Bado tunajiuliza sisi ni nani na kwa nini tupo hapa na tunaelekea wapi.” Kwa hekima, tutatafuta majibu kutoka chanzo bora zaidi. Biblia inasema hivi kuhusu Chanzo hicho: “[Mungu] ndiye aliyetufanya, wala si sisi wenyewe.”—Zaburi 100:3.

Je, haipatani na akili kumtazamia Yule aliyefanya miujiza kama ile ya uumbaji atosheleze uhitaji wetu wa kiroho? Yesu Kristo alipendekeza kwamba tufanye hivyo. Alitambua kwamba Muumba wetu ambaye ndiye Chanzo pekee cha uhai, anaweza kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho.—Zaburi 36:5, 9; Mathayo 5:3, 6.

Kwa kweli, kupata jibu linalotegemeka la swali hili, Kwa nini tupo hapa? ni muhimu ili kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho. Tafadhali fikiria maoni yenye kupendeza ya Muumba wetu kuhusu jambo hilo.