Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtoto Anapokosa Kufurahia Maisha Yake ya Utotoni

Mtoto Anapokosa Kufurahia Maisha Yake ya Utotoni

Mtoto Anapokosa Kufurahia Maisha Yake ya Utotoni

“Kufurahia maisha ya utotoni ndiyo haki ya kwanza kabisa ya watoto.”Kitabu “The Hurried Child.”

AMA kweli utakubali kwamba watoto wote wanapaswa kufurahia maisha yao ya utotoni bila kuwa na mahangaiko yoyote. Hata hivyo, inahuzunisha kuona kwamba wavulana na wasichana wengi hawafurahii maisha yao ya utotoni. Hebu fikiria kuhusu maelfu au hata mamilioni ya watoto, ambao wameathiriwa na vita na hivyo matarajio yao maishani kudidimia. Fikiria pia kuhusu watoto ambao maisha yao yameharibiwa na utumwa au mateso.

Wengi wetu hatuwezi kuwazia jinsi watoto wanavyohisi wanapolazimika kuishi barabarani kwa kuhisi kwamba maisha ya barabarani ni salama kuliko ya nyumbani. Huo ni wakati ambao wanahitaji kupendwa na kuhisi wakiwa salama. Badala yake, watoto hao wamelazimika kujifunza kuishi barabarani na kujilinda na wavamizi wowote ambao wangetaka kuwashambulia. Tena na tena, watoto wamevurugwa na matukio ya nyakati zetu ngumu.

“Laiti Ningalirudia Maisha Yangu ya Utotoni”

Carmen, mwenye umri wa miaka 22, alitaabika sana alipokuwa mtoto. * Kwa kuwa baba yao aliwatesa na mama yao akawapuuza, Carmen na dada yake walilazimika kuishi barabarani. Ijapokuwa kulikuwa na hatari nyingi, wao waliepuka madhara mengi ambayo huwapata watoto wengi ambao hutoroka nyumbani.

Hata hivyo, Carmen bado anajuta kwa kukosa kufurahia maisha yake ya utotoni. “Ni kana kwamba niliruka kutoka utotoni hadi umri wa miaka 22,” yeye asema akisikitika. “Sasa nimeolewa na nina mtoto, lakini bado natamani kufanya mambo yanayofanywa na wasichana wadogo, kama kucheza na wanasesere. Nataka kupendwa na kukumbatiwa na wazazi wangu. Laiti ningalirudia maisha yangu ya utotoni.”

Watoto wengi sana wanateseka kama Carmen na dada yake. Wanaishi barabarani, na hawafurahii maisha yao ya utotoni. Wengi wao hujiruzuku kwa kufanya uhalifu. Habari na takwimu zinaonyesha kwamba watoto wadogo sana wanajihusisha na uhalifu. Na isitoshe, wasichana wengi wanapata watoto wakiwa wadogo mno—wakiwa bado ni watoto.

Tatizo Lililofichika

Si ajabu kwamba watoto wengi wanapelekwa kwenye vituo vya utunzaji. Tahariri iliyochapishwa katika gazeti la Week-end Australian ilisema hivi: “Matatizo ya utunzaji yamezuka bila ya sisi kujua. Watoto wengi zaidi kutoka familia zilizovunjika au zenye matatizo wanapuuzwa.” Gazeti hilo pia lilisema hivi: “Wafanyakazi waliopewa daraka la kuwatunza watoto hao hukaa kwa miezi au hata miaka bila kuwajulia hali watoto hao, huku watoto wengine wakihamishwa huku na huku, na hivyo kukosa makao ya kudumu.”

Habari fulani ilisema kwamba msichana mmoja mwenye umri wa miaka 13 alipitia makao 97 kwa kipindi cha miaka mitatu. Alikaa usiku mmoja tu katika makao mengine. Sasa anakumbuka jinsi alivyokuwa mwenye majonzi mengi kwa sababu ya kudharauliwa na kukosa usalama. Watoto kama hao hawafurahii maisha yao ya utotoni hata kidogo.

Basi haishangazi kwamba wataalamu wanasema kuwa watoto wengi zaidi hawafurahii maisha yao ya utotoni. Ikiwa wewe ni mzazi, unapofikiria mambo hayo yenye kusikitisha, unapaswa kuona kwamba umebarikiwa kwa kuwa unaweza kuwaandalia watoto wako makao na mahitaji mengine. Lakini kuna hatari nyingine. Katika ulimwengu wa leo, si watoto wote wanaokosa kufurahia maisha yao ya utotoni kabisa. Wakati mwingine, maisha yao ya utotoni huharakishwa. Jinsi gani, na kukiwa na matokeo gani?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Jina limebadilishwa.