Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Tunamtii Mungu Kuliko Wanadamu’

‘Tunamtii Mungu Kuliko Wanadamu’

‘Tunamtii Mungu Kuliko Wanadamu’

Alipokuwa mwenye umri wa miaka 17, Adam alikuwa mmoja wa watu watatu walioshinda shindano lililothaminiwa na Jumba la Makumbusho ya Maangamizi Makuu la Marekani. Watu karibu 500 walioshiriki shindano hilo walichora au kuandika jambo lililoonyesha jinsi watu walivyovumilia mnyanyaso kwa ujasiri wakati wa utawala wa Wanazi. Adam ambaye ni Shahidi wa Yehova aliamua kutengeneza picha inayoonyesha mateso yaliyowapata washiriki wa dini yake wakati wa utawala wa Wanazi. Adam asema picha hiyo haikukusudiwa kuonyesha kushindwa au majuto, bali shangwe waliyo nayo Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya kushinda mnyanyaso katili wa serikali hiyo. Mtoto ameonyeshwa kwenye picha hiyo. Kwa nini? “Ili kuonyesha kwamba watoto pia walikuwa jasiri wakati wa mnyanyaso huo wa Wanazi,” asema Adam.

Inajulikana wazi kwamba wakati wa utawala wa Wanazi, Mashahidi wa Yehova walikataa kumpigia Hitler saluti na kuunga mkono chama chake cha kisiasa. Msimamo wao umeonyeshwa kwenye upande wa juu wa kulia wa picha ya Adam. Hapo barua iliyotumwa kwa serikali ya Ujerumani mnamo Oktoba 7, 1934, na makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova imenukuliwa. Sehemu ya barua hiyo inasema: “Sheria yenu inapingana moja kwa moja na sheria ya Mungu, na kama mitume waaminifu, ‘tunapaswa kumtii Mungu kuliko wanadamu,’ na ndivyo tutakavyofanya. (Matendo 5:29) . . . Kwa kuwa serikali na maafisa wenu bado wanajaribu kutulazimisha kuasi mamlaka iliyo kuu zaidi katika ulimwengu mzima, sasa hatuna budi kukujulisha kwamba, kwa msaada wa Yehova Mungu tutaendelea kumtii, na kumtegemea kabisa atuokoe kutoka kwa mnyanyaso na watu wote wanaotunyanyasa.”

Adam anafurahia picha yake sana. “Ingawa Mashahidi hao wa Yehova hawakutaka kumuumiza mtu yeyote, wao waliamini kwamba walipaswa kumwabudu Mungu peke yake, hata kama jambo hilo lilifanya wauawe,” yeye asema. Msimamo huo imara wa Mashahidi wa Yehova umeonyeshwa katika kichwa cha picha ya Adam kinachosema: “Tutamtii Mungu kuliko wanadamu!”