Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Warusi Wathamini Sana Uhuru wa Kuabudu

Warusi Wathamini Sana Uhuru wa Kuabudu

Warusi Wathamini Sana Uhuru wa Kuabudu

TANGU KUPOROMOKA KWA MUUNGANO WA SOVIETI KATIKA MWAKA WA 1991, WATU WANAOISHI HUKO WAMEFURAHIA UHURU MKUBWA ZAIDI WA KUMWABUDU MUNGU. UHURU HUO UMETHAMINIWA SANA PIA NA WALE AMBAO WAMEHAMIA NCHI NYINGINEZO.

KWA watu wengi wanaoishi katika uliokuwa Muungano wa Sovieti, uhuru wa kukusanyika waziwazi ili kumwabudu Mungu ni pendeleo linalothaminiwa sana—pendeleo walilokuwa wamenyimwa kwa miongo mingi.

Baada ya Mapinduzi ya Bolsheviki mwaka wa 1917, ilikuwa hatari kusoma Biblia katika Urusi, na watu wengi walihatarisha uhuru wao kwa kufanya hivyo. Mashahidi wa Yehova walikuwa tofauti. Kwa kweli, gazeti Newsweek la Aprili 16, 1956—karibu miaka 44 iliyopita—lilimnukuu kijana mmoja huko Ujerumani Mashariki akisema: “Hakuna mtu mwingine anayesoma Biblia ila Mashahidi wa Yehova.” Hata hivyo, Mashahidi walitiwa gerezani na kwenye kambi za kazi ngumu kwa kukusanyika pamoja ili kujifunza Biblia na kwa kuhubiri ujumbe wa Biblia. Hata hivyo, popote walipoenda, walikazia uangalifu wao tumaini linalotegemea Biblia, kama ionyeshwavyo na sanduku lililo katika makala haya.

Muungano wa Sovieti ulipoanza kuporomoka mwaka wa 1991, Mashahidi wa huko walifanya mikusanyiko saba iliyokazia programu ya mafundisho ya Biblia. Kulikuwa na jumla ya wahudhuriaji 74,252. Mnamo mwaka wa 1993, miaka miwili tu baadaye, watu 112,326 walikusanyika kwenye mikusanyiko minane katika jamhuri 4 kati ya zilizokuwa jamhuri 15 za Muungano wa Sovieti. * Wengi wa maelfu hao walikuwa wamezuiliwa miaka mingi katika magereza na kambi za kazi ngumu za Sovieti. Wakristo hao waaminifu walishukuru sana kwa kupata uhuru wa kumwabudu Mungu bila kizuizi.

Kila mwaka tangu 1993, watu kutoka zile zilizokuwa jamhuri za Sovieti wamethamini sana pendeleo la kukusanyika kwa uhuru kwenye mikusanyiko ya Kikristo katika nchi yao. Kwa mfano, mwaka jana jumla ya Mashahidi wa Yehova 282,333 pamoja na rafiki zao walifurahia kuabudu pamoja kwenye Mikusanyiko ya Wilaya 80 ya “Neno la Mungu la Kiunabii” iliyofanywa katika zile zilizokuwa jamhuri za Sovieti. Na jumla ya watu zaidi ya 13,452 walibatizwa.

Ijapokuwa inashangaza, mwaka jana kulikuwa na mikusanyiko ya wilaya iliyotumia lugha ya Kirusi katika nchi nyingine ulimwenguni. Jumla ya watu 6,336 walihudhuria mikusanyiko hiyo minne katika nchi zilizo nje ya uliokuwa Muungano wa Sovieti! Mikusanyiko hiyo ilifanyiwa wapi? Na kwa nini watu wengi sana wanaosema lugha ya Kirusi hupendezwa sana na Biblia? Acheni tufikirie kwa ufupi swali la pili.

Wanatambua Uhitaji wa Kiroho

Urusi ina historia ndefu ya kidini. Makanisa yake makuu yenye madoido, yaliyojengwa karne nyingi zilizopita, ni miongoni mwa makanisa mashuhuri zaidi katika Jumuiya ya Wakristo. Hata hivyo, Kanisa Othodoksi la Urusi, kama vile Kanisa Katoliki la Roma, halijawafundisha watu kuhusu Biblia.

“Biblia,” chaeleza kitabu The Russian TragedyThe Burden of History, “haijawahi kuchangia fungu kubwa kwenye Othodoksi ya Mashariki ya Urusi. Kulingana na msomi wa kidini Mrusi Sergei Ivanenko, matokeo yamekuwa kwamba “kukosa ujuzi wa Biblia kwa wafuasi wa Othodoksi kumesababisha uhakika wa kwamba wanaparokia wengi wa makanisa ya Othodoksi wanaathiriwa sana na uvutano wa ushirikina, uchawi, na mizungu kuliko wasio waamini.”

Mwandishi mashuhuri Mrusi Tolstoy alitoa maoni kama hayo. Aliandika hivi: “Nilisadiki kwamba fundisho la kanisa la [Othodoksi la Urusi] lilikuwa udanganyi wa ujanja unaodhuru, na kihalisi ni mkusanyo wa ushirikina na ulozi mbaya sana, ambao huficha kabisa maana kamili ya mafundisho ya Kikristo.”

Hali hiyo ilichangia kusitawi kwa Ukomunisti wa Sovieti pamoja na propaganda yake ya kukana Mungu na itikio linalojulikana sana: “Dini ni kasumba ya watu.” Hata hivyo, Ukomunisti wenyewe ukawa namna fulani ya dini, mara nyingi iliitwa Dini ya Kikomunisti. Lakini Dini ya Kikomunisti haikudumu. Serikali ya Sovieti ilipoporomoka mwaka wa 1991, mamilioni ya watu walitatanika wakashindwa wataelekea wapi. Kwa kuchochewa na Mashahidi wa Yehova, maelfu ya Warusi walitafuta majibu kwenye Biblia.

Kwa sababu ya mfumo bora wa elimu, Warusi walipata kuwa miongoni mwa watu waliosoma zaidi ulimwenguni. Hivyo, Warusi wengi wakaja kuwa si wasomaji tu wa Biblia bali pia wapenzi wa mafundisho yake. Wakati huohuo, hasa katika mwongo wa miaka ya 1990, mamia ya maelfu ya watu kutoka ule uliokuwa Muungano wa Sovieti walihamia nchi nyingine, kama vile Marekani, Ugiriki, na Ujerumani. Tokeo lilikuwa nini?

Wako Huru Kuabudu Katika Ujerumani

Katika karne ya 18 na 19, Wajerumani wengi walihamia Urusi. Sophie, mwenye umri wa miaka 15, ndiye aliyekuwa mashuhuri zaidi, ambaye, mnamo mwaka wa 1762, alichukua hatamu za kuongoza Urusi baada ya mumewe. Katika muda mrefu aliotawala, Sophie, ambaye baadaye aliitwa Catherine Mkuu, alialika wakulima Wajerumani waishi Urusi. Kisha, wakati Ujerumani ilipovamia Muungano wa Sovieti katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, watu wengi waliokuwa wa asili ya Ujerumani walipelekwa Siberia na kwenye jamhuri nyingine za Sovieti kama vile Kazakhstan, Kyrgyzstan, na Uzbekistan. Hivi majuzi Wajerumani wengi wanaosema lugha ya Kirusi, na vilevile wengine kutoka ule uliokuwa Muungano wa Sovieti, walihamia Ujerumani ili kufurahia hali bora za kiuchumi.

Katika Desemba 1992 kutaniko la kwanza la lugha ya Kirusi katika Ujerumani lilianzishwa huko Berlin. Kufikia mwaka uliopita, makutaniko 52 na vikundi vidogo zaidi ya 43 vilifanywa kuwa mizunguko mitatu ya watu wanaosema lugha ya Kirusi huko Ujerumani. Kulikuwa na kilele cha wahudhuriaji 4,920 kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa lugha ya Kirusi wa “Neno la Mungu la Kiunabii” huko Cologne, uliofanywa kuanzia Julai 30 hadi Agosti 1, ambapo watu 164 walibatizwa wakionyesha wakfu wao kwa Yehova. Mapema zaidi, Aprili 1, katika makutaniko ya Ujerumani yanayosema lugha ya Kirusi, kulikuwa na watu 6,175 waliohudhuria sherehe ya Ukumbusho wa kifo cha Yesu.

Warusi Nchini Marekani

Pia watu wengi sana wanaosema lugha ya Kirusi wamehamia Marekani kutoka ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. Gazeti The New York Times liliripoti: “Kati ya mwaka wa 1991 na 1996, Warusi ndio waliokuwa kikundi cha wahamiaji kinachokua haraka zaidi huko Brooklyn. Katika kipindi hichohicho, Idara ya Uhamiaji na Huduma za Kusajili Wenyeji iliandikisha zaidi ya wahamiaji 339,000 huko Marekani kutoka ule uliokuwa Muungano wa Sovieti.”

Baadaye, gazeti la Times la Januari 1999 lilisema kwamba katika mwongo uliopita, Wayahudi wapatao 400,000 kutoka uliokuwa Muungano wa Sovieti walikuwa wamehamia New York City na viunga vyake. Kwa kuongezea, katika miaka ya hivi majuzi maelfu ya Warusi wamehamia katika sehemu nyingine za Marekani. Kwa mfano, kumekuwa na wahamiaji wengi Warusi wapatao 35,000 huko kaskazini mwa California, na kuifanya iwe kituo cha tatu kwa ukubwa cha wahamiaji kutoka ule uliokuwa Muungano wa Sovieti baada ya New York na Los Angeles. Watu hao wanaosema lugha ya Kirusi pia wamekubali fursa ya kujifunza Biblia, na mamia wamekuwa waabudu wa Mungu wa kweli, Yehova.

Katika Aprili 1, 1994, kutaniko la kwanza la Mashahidi wa Yehova linalosema lugha ya Kirusi lilianzishwa hivi majuzi huko Marekani, Brooklyn, New York. Hatimaye, makutaniko ya Kirusi yalianzishwa huko Pennsylvania, California, na Washington. Vikundi vya mafunzo vilianzishwa katika sehemu nyingi za nchi hiyo.

Wa Kwanza Nchini Marekani

Agosti uliopita tarehe 20 hadi 22, kilele cha wahudhuriaji 670 kutoka Marekani kote na Kanada walisisimuka kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya wa kwanza katika Kirusi uliofanywa New York City. Hotuba zote zilitolewa kwa lugha ya Kirusi, na drama ya mavazi kamili, iliyokazia simulizi la Biblia la Yakobo na Esau, ilifanywa na washiriki wa Kutaniko la lugha ya Kirusi la Los Angeles, California. Kwa kweli ilikuwa tukio kuu katika mkusanyiko huo.

Tukio jingine kuu lilikuwa ubatizo wa watu 14, wote wanaonekana kwenye picha iliyo katika makala haya. Baadhi yao walisafiri kilometa zipatazo 4,000 kutoka Portland, Oregon, na kutoka Los Angeles na San Francisco, California, ili kubatizwa kwenye mkusanyiko katika New York City. Hapo awali, hawa 14 walikuwa wameishi katika zile zilizokuwa jamhuri za Sovieti za Armenia, Azerbaijan, Belarus, Moldova, Ukrainia, na Urusi. Mambo yaliyowapata huonyesha jinsi wanavyothamini sana ujuzi wa Mungu na uhuru wa kumwabudu.

Svetlana (safu ya kwanza, wa tatu kutoka kushoto) alilelewa Moscow. Akiwa na umri wa miaka 17 aliolewa na mwimbaji mashuhuri aliyekuwa na umri mkubwa kumshinda, na wakahamia Marekani mwaka wa 1989 pamoja na mwana wao mchanga. Mume wake alisafiri kwa mapana na marefu, na wakatalikiana miaka mitano baada ya hapo.

Svetlana alipokutana na mfanyakazi mwenzi aliye Shahidi, rafiki zake walimwonya asijihusishe na “madhehebu ambayo yangedhibiti maisha [yake] na kuchukua pesa [zake] zote.” Hata hivyo, alitaka kujifunza Biblia. Alipoonyeshwa jina la Mungu katika Biblia, alisema hivi: “Nilivutiwa sana kuona kwamba ni Mashahidi peke yao waliokuwa wakilijulisha.”

Akiwa kijana, Andrei (safu ya nyuma, wa tatu kutoka kushoto) alitoka nyumbani kwao Siberia ili kupata mazoezi zaidi ya kuwa mwanariadha ile ambayo leo ni St. Petersburg. Punde baada ya hapo, Muungano wa Sovieti uliporomoka, na katika mwaka wa 1993, Andrei, akiwa na umri wa miaka 22 alihamia Marekani. Aeleza hivi: “Nilianza kufikiri juu ya Mungu na kuanza kwenda kwenye Kanisa Othodoksi la Urusi. Wakati mmoja, kwenye sherehe ya Ista ya Urusi, nilikaa kanisani usiku kucha nikitafuta kumkaribia Mungu.”

Karibu na wakati huo, Svetlana alikutana na Andrei, na akamweleza yale aliyokuwa akijifunza kwenye funzo lake la Biblia. Alikubali kuandamana naye kwenye mkutano wa Mashahidi wa Yehova, na baada ya hapo akakubali funzo la Biblia. Walifunga ndoa Januari 1999. Baada ya kubatizwa kwenye mkusanyiko walikuwa na shangwe kwelikweli.

Pavel (safu ya nyuma, wa nne kutoka kushoto) alizaliwa karibu na Qaraghandy, Kazakhstan, lakini baadaye akahamia Nal’chik, Urusi. Jiji hilo kubwa liko karibu na Chechnya na Dagestan, ambako kumekuwa na mapigano makali sana. Pavel alikutana na Mashahidi huko mara ya kwanza Agosti 1996, lakini akahamia San Francisco mwezi uliofuata. Alikuwa amejihusisha na dawa za kulevya na kuzaa binti, aliyebaki Urusi pamoja na mama yake.

Mara tu baada ya kuwasili Marekani, Pavel aliwafikia Mashahidi wa Yehova na kukubali funzo la Biblia. Alirekebisha maisha yake na kumwandikia mkewe barua kuhusu itikadi zake mpya. Sasa anajifunza na Mashahidi, na mipango inafanywa aende Marekani ili waweze kufunga ndoa na Pavel na kumtumikia Yehova pamoja huko California wakiwa na binti yao.

George (safu ya mwisho, wa pili kutoka kushoto) alizaliwa na kulelewa Moscow. Alihamia Marekani mwaka wa 1996, na mwaka uliofuata akafunga ndoa na Flora, aliyekuwa mwenyeji wa Azerbaijan. George alihudhuria ibada katika Kanisa Othodoksi la Urusi, lakini baada ya kusoma nakala ya gazeti Mnara wa Mlinzi, alikuwa na maswali kuhusu fundisho la Utatu. Barua aliyoandikia Watch Tower Society ilipojibiwa, alipokea broshua Je! Uamini Utatu? Mnamo mwaka wa 1998 yeye na Flora walianza kujifunza Biblia. Sasa yeye pia anapanga kubatizwa.

Tukio jingine kuu la mkusanyiko lilikuwa kupokea salamu kutoka Moscow, ambapo watu 15,108 walikusanyika kwa ajili ya mkusanyiko wao kwenye mwisho-juma huohuo. Wajumbe katika New York City walisisimuka kama nini kusikia tangazo kwamba watu 600 walikuwa wamebatizwa huko! Hiyo ilikuwa kweli hasa kwa sababu ya ripoti zenye kuogofya za magazeti na televisheni zilizokuwa zimeanza kutokea Marekani na kwingineko katika juma lililotangulia tarehe ya mkusanyiko.

Kilichokuwa Kikitokea Moscow

Katika Julai 21, 1999, Mashahidi walitia sahihi mkataba wa kutumia Stediamu ya Olympic iliyo karibu na sehemu ya kati ya Moscow karibu tu na kanisa kubwa la Othodoksi la Urusi. Lakini juma moja kabla ya mkusanyiko kuanza, ilikuwa dhahiri kwamba kungekuwa na upinzani. Kufikia Jumatano, Agosti 18, kibali cha kutumia stediamu hakikuwa kimepokewa bado, hata ingawa malipo yalikuwa yametolewa tayari. Maofisa walisaidiwa kuona kwamba, kama ionyeshwavyo na sanduku kwenye ukurasa wa 28, Mashahidi wa Yehova ni tengenezo la kidini linalotambuliwa kisheria nchini Urusi.

Kwa sababu karibu wajumbe 15,000 wa mkusanyiko walikuwa wakijitayarisha kuhudhuria Ijumaa asubuhi, wawakilishi wa Mashahidi walianza kuwa na wasiwasi. Wajumbe fulani walikuwa wakisafiri hadi Moscow kutoka majiji na miji iliyo umbali wa kilometa nyingi. Hatimaye, baada ya mazungumzo ya saa kadhaa, karibu saa 2:00 usiku, Alhamisi, Agosti 19, wasimamizi wa stediamu walifurahi kuwajulisha wawakilishi wa Mashahidi kwamba mkusanyiko huo unaweza kufanywa. Wasimamizi wa jiji walikuwa wamesema kwamba hawakupinga mkusanyiko huo.

Asubuhi iliyofuata maelfu walimiminika kwenye stediamu hiyo. Mashahidi wa kujitolea walikuwa wamefanya kazi usiku kucha ili kutayarisha kuwasili kwa wajumbe. Pia asubuhi hiyo ya kwanza waandishi wa habari walikuwepo, ambao mapema zaidi walikuwa wamearifiwa kuhusu upinzani wa kufanywa kwa mkusanyiko huo. “Pongezi!” mmoja wao akasema kwa mshangao. “Tunaterema kusikia kwamba mkusanyiko wenu utafanywa.”

Kielelezo cha Mwenendo Wenye Utaratibu

Wasimamizi wa stediamu waliona kwamba lingekuwa jambo la busara kuchukua hatua za usalama. Hivyo, walinda-usalama wakiwa na vifaa vya kugundua chuma kama vile vinavyotumiwa kuchunguza abiria kwenye viwanja vya ndege waliwekwa kwenye kila kiingilio. Pia polisi waliwekwa ndani ya stediamu yote. Mkusanyiko uliendelea kwa njia yenye utaratibu licha ya tisho kubwa.

Mnamo Jumamosi alasiri mtu fulani alipiga simu akidokeza kwamba bomu lilikuwa limetegwa kwenye stediamu hiyo. Tisho hilo lilipokewa muda mfupi kabla ya hotuba mbili za mwisho siku hiyo. Kwa hiyo, kwa ombi la idhini la wasimamizi wa stediamu hiyo, tangazo fupi lilitolewa watu watoke kwenye stediamu mara moja. Watu walipofanya hivyo kwa njia ya utaratibu, maofisa wa stediamu na mapolisi walishangaa. Hawakuwa wamepata kuona jambo kama hilo! Waliuliza kama jambo hilo lilikuwa limefanyiwa mazoezi.

Hakuna bomu lililopatikana, na siku iliyofuata programu ilirefushwa ili itie ndani hotuba ambazo hazikuwa zimetolewa Jumamosi. Wasimamizi wa stediamu walipendezwa na mkusanyiko huo.

Ugiriki na Kwingineko

Mnamo mwisho-juma wa mwisho wa Agosti na wa kwanza katika Septemba, mikusanyiko ya wilaya ya Kirusi ilifanywa pia katika Ugiriki—kwanza huko Athens kisha Thessalonica. Kulikuwa na jumla ya wahudhuriaji 746, na 34 wakabatizwa. Kuna makutaniko 8 ya lugha ya Kirusi katika Ugiriki pia kuna vikundi vidogo zaidi ya 17 vya wahamiaji kutoka zile zilizokuwa jamhuri za kusini za Muungano wa Sovieti. Vikundi hivyo hufanya mikutano yao kwa lugha ya Kirusi na katika lugha nyinginezo zinazosemwa na wahamiaji hao.

Victor alikuwa mmojawapo wa wale waliobatizwa huko Athens. Alikuwa mkana-mungu, lakini katika Agosti 1998 alihudhuria mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova katika Athens, ambako mke wake alibatizwa. Alisema kwamba alivutiwa sana na upendo ulioonyeshwa na wajumbe hivi kwamba alichochewa kujifunza Biblia.

Mwanamume mmoja anayeitwa Ighor alipokea nakala ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani na baada ya kukisoma alitupa sanamu zote za kidini. Hata alianza kujitambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuandikia ofisi ya tawi ya Athens na kutembelewa na Mashahidi katika Novemba 1998, mara moja alihudhuria mkutano wa kutaniko wa kwanza na hajakosa hata mmoja tangu wakati huo. Sasa, baada ya kubatizwa, Ighor ana mradi wa kuwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova.

Watu wanaosema lugha ya Kirusi wamehamia nchi nyingine nyingi ulimwenguni ambazo hatujazitaja. Wengi wa watu hao pia hufurahia uhuru wao wa kujifunza Biblia na kukusanyika hadharani ili kumwabudu Mungu. Hilo ni pendeleo wanalolithamini sana!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Zifuatazo ni jamhuri 15 ambazo sasa ni nchi huru: Armenia, Azerbaijan, Belarus, Estonia, Georgia, Kazakhstan, Kyrgyzstan, Latvia, Lithuania, Moldova, Tajikistan, Turkmenistan, Ukrainia, Urusi, na Uzbekistan.

[Sanduku katika ukurasa wa 22]

Warusi Wanaopenda Biblia

Profesa Sergei Ivanenko, msomi wa kidini wa Urusi aliye mashuhuri, aliwataja Mashahidi wa Yehova kuwa watu waliojitoa kikweli kujifunza Biblia. Katika kitabu chake cha karibuni cha lugha ya Kirusi, O lyudyakh, nikogda nye rasstayushchikhsya s bibliey (Watu Ambao Hawakosi Biblia Zao Kamwe), aliandika hivi kuhusu historia yao ya mapema katika Muungano wa Sovieti: “Hata walipotiwa gerezani kwa sababu ya kushikilia kwa uaminifu itikadi zao, Mashahidi wa Yehova walipata njia za kutumia Biblia.” Ili kueleza hilo, alisimulia jambo lililoonwa lifuatalo.

“Wafungwa walikatazwa kuwa na Biblia. Biblia zilitwaliwa wakati wa upekuzi. Katika mojawapo ya kambi zilizokuwa kaskazini, mmojawapo wa Mashahidi wa Yehova alikuwa fundi wa stima na aliweka vitabu vya Biblia ndani ya transfoma iliyokuwa na nguvu nyingi sana za umeme. Kila sehemu ya Biblia ilifungwa kwa uzi kwenye waya hususa, na ni mtu huyo tu aliyejua ni uzi upi uliohitaji kuvutwa ili kutoa sehemu hiyo—kwa mfano, Gospeli ya Mathayo—bila kupigwa na umeme kwa njia ya kufisha. Bila shaka hakuna upekuzi wowote uliofua dafu, hata iwe askari walifanya jitihada gani, kwa hiyo Biblia hii ya pekee haikugunduliwa.”

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

Mashahidi wa Yehova Wasajiliwa Urusi

Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitangaza kwa bidii Ufalme wa Mungu huko Urusi kwa zaidi ya karne moja. Hata hivyo, kwa sababu ya vizuizi vya serikali, Mashahidi hawakupata kutambuliwa kisheria mwanzoni hadi Machi 27, 1991. Wakati huo, walikuwa wamesajiliwa kwa jina Administrative Center of the Religious Organizations of Jehovah’s Witnesses in the U.S.S.R.

Katika Septemba 26, 1997, sheria yenye kichwa “Kuhusu Uhuru wa Dhamiri na Ushirika wa Kidini” ilitungwa. Sheria hiyo mpya ilitangazwa na vyombo vya habari ulimwenguni pote. Kwa nini? Kwa sababu wengi waliona kutungwa kwa sheria hiyo kuwa jitihada za kuzuia utendaji wa kidini hasa wa dini ndogo-ndogo huko Urusi.

Hivyo, licha ya kusajiliwa kwa Mashahidi wa Yehova kulikopatikana kwa shida mnamo 1991, sheria mpya ya Urusi ya Uhuru wa Dhamiri iliwataka wao, vilevile matengenezo yote ya kidini, yasajiliwe upya. Maswali mengi yakazuka. Je, hilo lilionyesha kwamba wenye mamlaka wa Urusi walikuwa wamerudia sera ya kuwakandamiza Mashahidi wa Yehova? Au je, uvumiliano wa kidini na uhuru wa ibada unaohakikishwa chini ya Katiba ya Shirikisho la Urusi utategemezwa?

Hatimaye jibu lilipatikana. Mashahidi walifurahi kama nini kutambuliwa kisheria kwa mara nyingine tena wakati Wizara ya Haki ya Urusi ilipotoa cheti cha kusajiliwa kwa “Administrative Center for Jehovah’s Witnesses in Russia,” katika Aprili 29, 1999!

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mkusanyiko wa kwanza wa wilaya wa lugha ya Kirusi nchini Marekani

[Picha katika ukurasa wa 24]

Drama ya Biblia yafanywa New York na Kutaniko la lugha ya Kirusi la Los Angeles

[Picha katika ukurasa wa 25]

Hawa 14 waliobatizwa New York wanatoka kwenye jamhuri sita za uliokuwa Muungano wa Sovieti

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Zaidi ya watu 15,000 walikusanyika katika Stediamu ya Olympic ya Moscow