Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Ulimwengu Wetu Ungekuwa Tofauti’

‘Ulimwengu Wetu Ungekuwa Tofauti’

‘Ulimwengu Wetu Ungekuwa Tofauti’

Jitihada za kufuta kusanyiko la Mashahidi wa Yehova katika Moscow mapema mwezi wa Agosti zilivuta uangalifu mwingi sana. (Ona ukurasa wa 27 na 28 kwa maelezo zaidi.) Andrei Zolotov, Jr., aliripoti kwenye The Moscow Times la Agosti 21, 1999, kwamba “Vladimir Kozyrev, naibu mkurugenzi wa uwanja wa michezo, alisema kwamba wasimamizi hawakuwa wakipinga Mashahidi wa Yehova kufanya mkutano wao. Alisema kuwa hakujua amri [ya kuufuta] ilitoka wapi.”

Katika barua iliyochapishwa katika The Moscow Times juma moja lililofuata, msomaji mmoja alipongeza gazeti hilo kwa kuchapisha makala ambayo “kwa kweli ilikuwa bila upendeleo” na akasema kwamba “ilihitaji kukaziwa uangalifu na wasomaji.” Yeye alisema: “Hadithi yenu juu ya matatizo mengi ambayo Mashahidi wa Yehova walipata walipokuwa wakijitayarisha kwa ajili ya kusanyiko lao la kila mwaka [ilifunua] walivyotendewa isivyo haki.”

Kisha mwandikaji wa barua hiyo akasema kwamba Mashahidi wa Yehova “wanajulikana sana ulimwenguni pote (na sasa pia katika Urusi) . . . Wao . . . wanajulikana kuwa watu wazuri sana, wenye fadhili na wasikivu ambao ni rahisi sana kushughulika nao, hawaweki kamwe mkazo wowote kwa watu wengine na wanatafuta amani daima katika mahusiano na wengine bila kujali itikadi zao za kidini iwe ni Wakristo Waothodoksi, Waislamu au Wabuddha. Miongoni mwao hakuna watu wapokeao rushwa, walevi au waraibu wa dawa za kulevya, na sababu ya kuwa hivi ni sahili: Wao hujaribu tu kuongozwa na masadikisho yao yanayotegemea Biblia katika kila jambo wanalofanya au wanalosema. Ikiwa watu wote ulimwenguni wangejaribu kuishi kulingana na Biblia kama vile Mashahidi wa Yehova wafanyavyo, ulimwengu wetu mkatili ungekuwa tofauti kabisa.”

Wenye mamlaka ambao wamewachunguza Mashahidi wa Yehova na kushughulika nao moja kwa moja wanathibitisha maelezo hayo. Kwa kielelezo, wenye mamlaka kama hao waliwapa kibali Mashahidi kujenga hili Jumba la Kusanyiko lililo zuri na jipya huko St. Petersburg, Urusi. Wakati wa kuweka wakfu jumba hili mapema mwezi wa Septemba 18, jumba hili lilikuwa limejaa watazamaji wenye furaha 2,257, na wengine 2,228 walisikiliza programu hiyo kwenye Majumba ya Ufalme katika St. Petersburg na kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Solnechnoye iliyo karibu.