Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

KUUTAZAMA ULIMWENGU

Kuyamulika Mahusiano

Kuyamulika Mahusiano

Inapohusu mahusiano, je, wewe huanza kwa kutafuta ushauri wa Biblia? Au hapo ndipo mahali pa mwisho unapotafuta ushauri? Ona jinsi hekima ya Biblia ilivyo bora inapolinganishwa na utafiti wa kisasa.

India

Kulingana na uchunguzi uliofanywa mwaka wa 2014, asilimia 61 ya vijana walio na umri wa kati ya miaka 18-25 wanaamini kwamba ngono kabla ya ndoa “ni jambo la kawaida.” Daktari mmoja jijini Mumbai alimweleza mwandishi wa gazeti la Hindustan Times kwamba kwa maoni yake, “vijana wanapoanzisha uhusiano wa kimapenzi haimaanishi kwamba wanakusudia kufunga ndoa. Huenda wanataka wafanye ngono mara moja na kuachana, wafanye ngono mara kwa mara bila kuwajibika, au waishi pamoja kwa muda fulani bila kuoana. Kwa maoni yao si lazima uhusiano huo uwe wa kudumu.”

JAMBO LA KUFIKIRIA: Je, katika visa vingi magonjwa ya zinaa na maumivu ya kihisia hutokea mtu anapofanya ngono kabla ya ndoa au baada ya ndoa?—1 Wakorintho 6:18.

Denmark

Kugombana mara kwa mara na washiriki wa familia kunahusianishwa sana na watu wanaokufa wakiwa na umri wa makamo. Watafiti katika Chuo Kikuu cha Copenhagen waliwachunguza watu 10,000 wenye umri wa makamo kwa kipindi cha miaka 11. Waligundua kwamba watu waliogombana mara nyingi na washiriki wa familia zao walikufa mapema ikilinganishwa na wale ambao hawakufanya hivyo. Mwandishi wa utafiti huo anasema kwamba kushughulikia wasiwasi, mahangaiko na mizozo kwa njia inayofaa “kunaweza kuwa njia muhimu ya kupunguza vifo vya mapema.”

BIBLIA INASEMA: “Yeyote anayezuia maneno yake ana ujuzi, na mtu mwenye utambuzi ana roho ya utulivu.”—Methali 17:27.

Marekani

Utafiti uliohusisha wenzi 564 waliofunga ndoa hivi karibuni huko Louisiana, ulionyesha kwamba watu wanaovunja uhusiano mara nyingi wakati wa uchumba na baada ya muda kurudiana, kuna uwezekano mkubwa kwamba wengi wao watatengana katika kipindi cha miaka mitano ya kwanza baada ya ndoa. Pia, ndoa zao huwa na migogoro mingi na zisizoridhisha.

BIBLIA INASEMA: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:6.