Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Hesabu 6:24-26—“BWANA Akubariki na Kukulinda”

Hesabu 6:24-26—“BWANA Akubariki na Kukulinda”

 “Yehova na awabariki na kuwalinda. Yehova awaangazie nuru ya uso wake, na kuwapa kibali chake. Yehova na ainue uso wake kuwaelekea na kuwapa amani.”​—Hesabu 6:24-26, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “BWANA akubariki na kukulinda; BWANA akuangazie nuru ya uso wake na kukuonyesha neema; BWANA anyanyue uso wake juu yako na kukupa salama.”​—Hesabu 6:24-26, Zaire Swahili Bible.

Maana ya Hesabu 6:24-26

 Maneno hayo yanarejelewa kuwa baraka ya kikuhani, au ya wazao wa Haruni, kwa sababu Haruni alikuwa kuhani mkuu wa kwanza katika taifa la Israeli. (Kutoka 28:1) Mungu ndiye Chanzo cha baraka hiyo. (Hesabu 6:22, 23) Alimwambia Musa hivi: “Mwambie hivi Haruni na wanawe: ‘Hivi ndivyo mtakavyowabariki Waisraeli,’” baada ya hapo Mungu akasema maneno yanayopatikana kwenye kitabu cha Hesabu 6:24-26. Makuhani waaminifu walitii amri hiyo ya Mungu. Isitoshe, waliheshimu jina la Mungu, Yehova. a Tunasoma hivi kwenye mstari wa 27: “Ni lazima [makuhani] waliweke jina langu juu ya Waisraeli, ili niwabariki Waisraeli.”

 “Yehova na awabariki na kuwalinda.” Yehova anawabariki waabudu wake kwa kuwalinda, kuwaongoza, na kuwapa mafanikio. (Methali 10:22) Katika Kiebrania, maneno hayo ya Hesabu 6:24-26 yameandikwa katika umoja. Hilo linaweza kuonyesha kwamba Mungu alikusudia si kulibariki taifa lote la Israeli tu, bali pia kumbariki kila Mwisraeli.

 “Yehova na awaangazie nuru ya uso wake, na kuwapa kibali chake.” Kumwomba Mungu ‘amwangazie mtu fulani nuru ya uso wake,’ ni ombi kwamba amwonyeshe kibali mtu huyo. b Maneno hayo pia yanaweza kutafsiriwa: “Tabasamu la BWANA na liwe juu yako.” (Hesabu 6:25, New International Reader’s Version) Yehova anawaonyesha watu wake kibali kwa kuwatendea kwa fadhili, huruma, na rehema.​—Isaya 30:18.

 “Yehova c na ainue uso wake kuwaelekea na kuwapa amani.” Yehova ‘anainua uso wake’ kuwaelekea waabudu wake kwa kuwakazia uangalifu kwa upendo na kuwapa amani. Kulingana na kitabu kimoja cha marejeo, “neno la Kiebrania linalotafsiriwa amani (shalom) halirejelei tu ukosefu wa ugomvi au matatizo, bali pia linarejelea kwamba mtu anajihisi vizuri na mzima, kimwili na kiroho.”

 Ili Waisraeli wanufaike kutokana na baraka zilizotajwa katika mistari hii, walipaswa kumtii Yehova. (Mambo ya Walawi 26:3-6, 9) Walipomtii, aliwasaidia kama alivyokuwa amewaahidi. Ilikuwa hivyo baadhi ya wafalme walipotawala, kama vile Sulemani na Hezekia.​—1 Wafalme 4:20, 25; 2 Mambo ya Nyakati 31:9, 10.

 Ingawa Wakristo hawatazamiwi kurudiarudia maneno ya baraka hiyo, wanaweza kusema maneno kama hayo wanaposali kwa Mungu kwa ajili ya wengine au wanapowatia moyo Wakristo wenzao. (1 Wathesalonike 5:11, 25) Yehova habadiliki. Anataka sikuzote kuwabariki na kuwalinda waabudu wake waaminifu. Hivyo, Wakristo wa kweli wanaweza kuwa na amani kwa sababu wanajua kwamba “uso” wa Yehova unawaangazia.

Muktadha wa Hesabu 6:24-26

 Sura kumi za kwanza za kitabu cha Hesabu zinaonyesha maagizo ambayo Waisraeli walipewa na Mungu walipokuwa wamepiga kambi karibu na Mlima Sinai wakiwa njiani kwenda kwenye Nchi ya Ahadi. Walipokuwa wamepiga kambi katika eneo hilo kwa mwaka mmoja hivi, Yehova aliwapanga kuwa taifa na kuwapa sheria ambazo zilijulikana kama agano la Sheria.

 Pia, Yehova alimwambia Musa jinsi Haruni na wanawe walipaswa kuwabariki Waisraeli, kwa sababu walichaguliwa kuwa makuhani. (Hesabu 6:22, 23) Baada ya hapo, Haruni na wazao wake walitumia maneno ya Hesabu 6:24-26 kulibariki taifa. Kadiri wakati ulivyopita, ikaja kuwa kawaida kwa kuhani kutoa baraka baada ya dhabihu ya mwisho kutolewa hekaluni kila siku.

 Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Hesabu.

a Jina Yehova ni tafsiri ya Kiswahili ya jina la kibinafsi la Mungu katika Kiebrania. Ili kujua kwa nini tafsiri nyingi za Biblia zinatumia jina la cheo Bwana badala ya jina la kibinafsi la Mungu, ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?

b Kwa kutofautisha, Biblia inasema kwamba Yehova alipochukizwa na matendo ya Waisraeli, aliwaficha uso wake.​—Isaya 59:2; Mika 3:4.

c Kulingana na toleo la funzo la NIV (NIV Study Bible), jina la Mungu limerudiwa-rudiwa katika mistari hii “ili kukazia maana na pia kuongeza uzito kwenye maneno yaliyo kwenye [mstari wa 27].” Hata hivyo, baadhi ya watu wanadai kwamba kurudiwa mara tatu kwa jina la Mungu katika mistari hiyo kunaunga mkono wazo la kwamba Mungu ni Utatu. Hilo si kweli. Kitabu kimoja kinachofafanua Biblia ambacho kinaunga mkono Utatu kinasema wazi kwamba kutumiwa kwa jina la Mungu mara tatu hapa “hakungempa kuhani aliyetoa baraka wazo hilo, wala watu waliopokea baraka hiyo hawangepata wazo hilo. Kwa maoni yao, kurudia jina la Mungu mara tatu kuliongeza ubora wa baraka hiyo na kuifanya iwe kamili.” (The Pulpit Commentary, Buku la 2, ukurasa wa 52) Kwa habari zaidi, ona makala “Je, Fundisho la Utatu Liko Katika Biblia?”