Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

1 Wakorintho 10:13—“Mungu Ni Mwaminifu”

1 Wakorintho 10:13—“Mungu Ni Mwaminifu”

 “Hakuna majaribu ambayo yamewapata ninyi ila yale yaliyo ya kawaida kwa watu. Lakini Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na majaribu hayo ataifanya pia njia ya kutokea ili mweze kuyavumilia.”​—1 Wakorintho 10:13, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”​—1 Wakorintho 10:13, Union Version.

Maana ya 1 Wakorintho 10:13

 Mstari huu unaonyesha sifa yenye kuvutia sana ya Mungu, yaani, uaminifu wake. Watumishi washikamanifu wa Mungu wanaweza kuwa na uhakika kwamba atawasaidia hasa wanapokabili majaribu au vishawishi.

 “Hakuna majaribu ambayo yamewapata ninyi ila yale yaliyo ya kawaida kwa watu.” Huenda watumishi wa Mungu wakashawishiwa kufanya jambo linalomchukiza. Ijapokuwa majaribu hayo huenda yakawa magumu, si mambo yasiyo ya kawaida kwa sababu watu wengi wamepatwa na majaribu kama hayo. a Hivyo, waabudu wa Mungu wanaweza kuwa na uhakika kwamba wao pia wanaweza kuvumilia mambo kama hayo.

 “Mungu ni mwaminifu.” Yehova b Mungu ni mwenye kuaminika na mwenye kutegemeka. Sikuzote ametimiza ahadi aliyotoa kwamba hatawaacha wale wanaompenda na wanaojitahidi kubaki washikamanifu na wanaomtii. (Kumbukumbu la Torati 7:9; Zaburi 9:10; 37:28) Kwa hiyo, wale wanaomwabudu wanaweza kuwa na uhakika kwamba atatimiza ahadi mbili zinazotutia moyo zinazoendelea kutajwa katika mstari huo.

 “Hatawaacha mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili.” Mungu huonyesha uaminifu wake kwa kutoruhusu majaribu yawe magumu hivi kwamba mtu ashindwe kuyavumilia. Yeye anajua kile ambacho waabudu wake wote wanaweza kuvumilia na wasichoweza.​—Zaburi 94:14.

 “Pamoja na majaribu hayo ataifanya pia njia ya kutokea ili mweze kuyavumilia.” Mungu anaweza ama kuondoa jaribu ama kuwapa waabudu wake kile wanachohitaji ili wavumilie. Kwa mfano, anaweza kutoa mwongozo kupitia roho yake takatifu, faraja kutoka katika Biblia, au msaada unaofaa kutoka kwa waabudu wenzao.​—Yohana 14:26; 2 Wakorintho 1:3, 4; Wakolosai 4:11.

Muktadha wa 1 Wakorintho 10:13

 Mstari huu unapatikana katika barua ambayo mtume Paulo aliliandikia kutaniko la Kikristo la Korintho. Katika sehemu hii ya barua yake, Paulo alitumia historia ya Israeli la kale kuwa mfano wa kuwaonya Wakorintho. (1 Wakorintho 10:11) Paulo anaorodhesha idadi ya majaribu ambayo Waisraeli walikabili, kutia ndani ibada ya sanamu na ukosefu wa maadili kingono. (1 Wakorintho 10:6-10) Baadhi yao walishindwa na vishawishi hivyo. Kwa kurejelea mifano yao, Paulo anawakumbusha Wakristo kwamba hawapaswi kuwa na uhakika kupita kiasi, wakifikiri kwamba hawawezi kushindwa na vishawishi. (1 Wakorintho 10:12) Hata hivyo, anawatia moyo kwa maneno ya 1 Wakorintho 10:13. Watumishi washikamanifu wa Mungu wanaweza kudumisha uaminifu wao wanapokabili jaribu lolote lile.

 Tazama video hii fupi uone muhtasari wa kitabu cha 1 Wakorintho.

a Neno la Kigiriki linalotajwa kuwa “jaribu” linaweza kumaanisha kishawishi.

b Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?