Hamia kwenye habari

Jionee Mambo Yaliyotendeka Katika Historia

Jionee Mambo Yaliyotendeka Katika Historia

Mnamo Oktoba 2012 katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, watu walianza rasmi kutembelea eneo hilo bila kuongozwa na mtu yeyote ili kujionea historia ya Mashahidi wa Yehova. * Mambo yanayoonyeshwa yanakazia jitihada, hatari, na mafanikio ambayo baadhi ya watu waliojitahidi kuishi maisha ya Kikristo, walikabili.

Wageni wanaweza kujionea historia ya Wakristo kuanzia mwaka wa 33 W.K. hadi kufikia sasa. Maonyesho hayo yamepangwa katika sehemu kuu nne ambazo zimepangwa kulingana na wakati wa matukio. Kila sehemu ina kichwa kinachotegemea andiko fulani la Biblia na kuna video fupi inayotoa utangulizi wa kila sehemu, na video hiyo imetafsiriwa katika lugha sita. Lugha hizo ni Kifaransa, Kiitaliano, Kijapani, Kikorea, Kireno, na Kihispania.

Sehemu Kuu za Maonyesho Hayo

Sehemu ya kwanza yenye kichwa, “Watu Wamelipenda Giza,” inatokana na andiko la Yohana 3:​19. Biblia ilitabiri kwamba watu waovu ‘wangesimama na kusema mambo yaliyopotoka.’ (Matendo 20:30) Mambo ambayo watu hao wangefanya yamekaziwa katika sehemu hii ya maonyesho.

Sehemu ya pili ina kichwa “Nuru na Iangaze,” maneno yanayotoka kwenye kitabu cha 2 Wakorintho 4:6. Sehemu hii inakazia mambo yaliyotendeka mwishoni mwa miaka ya 1800 hadi mwanzoni mwa miaka ya 1900. Sehemu hii inaanza na historia ya watu wanyoofu walioanza kujifunza Biblia na kufuata mambo waliyojifunza. Pia inazungumzia jinsi ujuzi na idadi yao ilivyoongezeka kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.

Sehemu inayofuata katika sehemu hii ya pili inaonyesha picha zilizowavutia watu wengi zijulikanazo kama “Photo-Drama of Creation.” Katika mwaka wa 1914, Wanafunzi wa Biblia (Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo) walianza kuonyesha picha hizo zilizoambatana na sauti. Miaka kadhaa baada ya mfululizo huo wa picha kutolewa, mamilioni ya watu walikuwa wakikusanyika sehemu mbalimbali kujionea picha hizo za hali ya juu. Sehemu hii ya maonyesho inatia ndani baadhi ya picha za awali, video fupi yenye utangulizi wa picha hizo, na zaidi ya picha 500 za slaidi zenye rangi.

Sehemu ya tatu ina kichwa “Yule Joka Mkubwa Akawa na Ghadhabu,” maneno yanayotoka kwenye kitabu cha Ufunuo 12:17. Sehemu hii ina habari zinazohusu minyanyaso ambayo wafuasi wa Kristo walikabili mwanzoni mwa karne ya 20 na ina habari zenye kusisimua za Wakristo ambao hawakushiriki vita wakati ulimwenguni ulipokuwa vitani. Video moja inasimulia kisa cha Remigio Cuminetti, Shahidi aliyekataa kuvaa sare ya jeshi la Italia na ambaye alikataa kushiriki Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Video nyingine inasimulia kisa cha Alois Moser. Alikataa kusema maneno “Heil Hitler!” jambo lililofanya afutwe kazi na hatimaye kupelekwa katika kambi ya mateso ya Dachau.

Pia katika sehemu hii ya maonyesho kuna chumba chenye giza ambacho ni mfano wa jela. Katika chumba hicho kuna picha za Mashahidi wa Yehova kutoka Ugiriki, Japani, Poland, na Serbia ambao walifungwa kwa sababu ya imani yao.

Sehemu ya nne ya maonyesho ina kichwa “Habari Njema kwa Mataifa Yote,” kinachotegemea andiko la Mathayo 24:14 na inaonyesha kazi ya Mashahidi wa Yehova kutoka mwaka wa 1950 hadi kufikia sasa. Picha mbalimbali zinaonyesha maendeleo ya kazi yetu, jinsi ambavyo tumeendelea kuhubiri bila kuacha, na upendo miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, sifa inayotutambulisha kuwa Wakristo wa kweli.

Kabla ya kuondoka eneo hilo la maonyesho, mgeni anaweza kujionea vibanda vinavyoonyesha Bible House na Brooklyn Tabernacle, sehemu ambazo zilitumiwa na Mashahidi wa Yehova zaidi ya miaka 100 iliyopita.

Kwa Nini Tulijenga Sehemu ya Maonyesho?

Ilichukua mwaka na miezi kadhaa kuchora na kujenga majengo ya sehemu hiyo. Mashahidi wa Yehova kutoka sehemu mbalimbali duniani walitoa vitu vyenye thamani sana ili viwekwe kwenye eneo hilo la maonyesho.

Kwa nini kazi yote hiyo ilifanywa? Alipoulizwa ni faida gani ambazo Mashahidi wa Yehova wangepata kwa kutembelea eneo hilo la maonyesho, mshiriki mmoja wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alisema maneno haya yanayojulikana sana, “Ili kujua tunakokwenda, ni lazima tujue tulikotoka.”

^ fu. 2 Maonyesho hayo yako 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York, na watu wanaalikwa kutembelea eneo hilo kuanzia siku ya Jumatatu hadi ya Ijumaa saa 2:00 asubuhi hadi saa 11:00 jioni. Kiingilio ni bure.