Hamia kwenye habari

Tuliamua Kurahisisha Maisha Yetu

Tuliamua Kurahisisha Maisha Yetu

Madián na Marcela walikuwa wakiishi maisha yenye starehe katika mji wa Medellín, Kolombia. Madián alipata mshahara mzuri ambao uliwawezesha kuishi katika nyumba maridadi. Lakini jambo fulani lilitokea ambalo liliwafanya wafikirie upya kuhusu mambo wanayopaswa kutanguliza wakiwa watumishi wa Yehova Mungu. Wanaeleza hivi: “Katika mwaka wa 2006 tulihudhuria kusanyiko la pekee lililokuwa na kichwa ‘Uwe na Jicho Rahisi.’ Hotuba nyingi zilikazia uhitaji wa kurahisisha maisha yetu ili kumtumikia Mungu kikamili zaidi. Tulipotoka kusanyikoni, tulitambua kwamba tulikuwa tukifanya kinyume na hotuba hizo. Tulikuwa tukinunua vitu kila wakati, kwa hiyo tulikuwa na deni kubwa sana.”

Hotuba hizo ziliwafanya Madián na Marcela kutambua uhitaji wa kufanya mabadiliko kwa hiyo, wakaanza kurahisisha maisha yao. “Tulianza kwa kupunguza matumizi yetu. Tulihamia nyumba ndogo zaidi, tukauza gari na kununua pikipiki.” Mbali na hilo, waliacha kwenda kutembea kwenye maduka makubwa ili wasishawishike kununua vitu. Walianza kutumia muda mwingi zaidi kuzungumza na majirani wao kuhusu Biblia. Na wakaanza kushirikiana zaidi na marafiki ambao wanamtumikia Yehova Mungu kwa bidii wakiwa mapainia wa pekee. a

Pia, Madián na Marcela waliamua kupanua huduma yao zaidi kwa kuhamia kutaniko dogo la kijijini lililohitaji msaada. Ili kufanya hivyo, Madián aliacha kazi yake. Msimamizi wake alifikiri amerukwa na akili. Kwa hiyo, Madián alizungumza naye, akamuuliza: “Wewe unapata pesa nyingi sana, lakini je, una furaha?” Msimamizi huyo alikubali kwamba hakuwa na furaha kwa sababu alikuwa na matatizo mengi ambayo hangeweza kutatua. Kwa hiyo, Madián akamwambia: “Kwa hiyo, unaona jambo kuu maishani si unapata pesa ngapi, bali jambo unalopaswa kuzingatia ni unawezaje kupata furaha ya kweli. Kuwafundisha watu kumhusu Mungu hunifanya mimi na mke wangu tuwe na furaha, na tungependa kuwa na furaha zaidi, kwa hiyo tumeamua kutumia muda mwingi zaidi katika kazi hiyo.”

Kwa sababu ya kufuatia miradi ya kiroho, Madián na Marcela wanajihisi wakiwa wameridhika na wakiwa na furaha ya kweli. Kwa miaka 13 iliyopita, wametumikia katika makutaniko yaliyo na uhitaji mkubwa zaidi kaskazini magharibi mwa Kolombia. Sasa wanafurahia pendeleo la kutumikia wakiwa mapainia wa pekee.

a Mapainia wa pekee huwekwa rasmi na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ili kuhubiri habari njema kwa wakati wote katika maeneo fulani. Wanapokea posho kidogo ya kuwasaidia kushughulikia mahitaji yao ya msingi.