Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mkaribie Mungu

‘Mimi Mwenyewe Sitawasahau Ninyi’

‘Mimi Mwenyewe Sitawasahau Ninyi’

JE, KWELI Yehova anawajali watu wake? Ikiwa ndivyo, anawajali kwa kadiri gani? Tunaweza kujua majibu ya maswali hayo kupitia njia moja tu—maneno ya Mungu mwenyewe. Katika Biblia, Yehova anafunua waziwazi jinsi anavyohisi. Fikiria maneno ya Isaya 49:15.

Ili kuonyesha hisia zake nyingi kuelekea watu wake, Yehova, kupitia Isaya, anatumia mmoja kati ya mifano yenye kugusa moyo zaidi ambayo tunaweza kuwazia. Anaanza kwa swali hili lenye kuchochea fikira: “Je, mke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya hivi kwamba asimhurumie mwana wa tumbo lake?” Bila kufikiria, huenda jibu likaonekana kuwa wazi. Mama anayenyonyesha anawezaje kumsahau mtoto wake mchanga? Mtoto wake anamtegemea kabisa mchana na usiku, naye hulia anapomhitaji mama yake! Lakini swali la Yehova linahusisha mambo mengi zaidi.

Kwa nini mama anamnyonyesha mtoto wake na kumtimizia mahitaji yake? Je, ni ili ambembeleze aache kulia? La. Kwa kawaida mama ‘anamhurumia mwana wa tumbo lake.’ Kitenzi cha Kiebrania ambacho hapa kimetafsiriwa ‘hurumia’ pia kinatafsiriwa “kuonyesha rehema.” (Kutoka 33:19; Isaya 54:10) Usemi huo wa Kiebrania unaweza kumaanisha huruma nyororo kuelekea mtu anayehitaji msaada au aliye dhaifu. Huruma za mama kuelekea mtoto wake mchanga ni moja kati ya hisia zenye nguvu zaidi tunazoweza kuwazia.

Kwa kusikitisha, akina mama fulani hawahurumii watoto wao wanaotamani kunyonya. Yehova anasema: “Hata hawa wanawake wanaweza kusahau.” Tunaishi katika ulimwengu ambapo wanaume na wanawake wengi si ‘washikamanifu, na hawana upendo wa asili.’ (2 Timotheo 3:1-5) Nyakati nyingine tunasikia kuhusu akina mama ambao wanawapuuza, wanawatendea vibaya, au kuwatupa watoto wao wachanga. Kitabu kimoja cha marejeo kinaeleza hivi kuhusu Isaya 49:15: “Akina mama si wakamilifu na mara kwa mara upendo wao unashindwa na uovu. Hata upendo ulio mkuu zaidi wa wanadamu unaweza kushindwa.”

Yehova anatuhakikishia hivi: “Lakini mimi mwenyewe sitakusahau wewe.” Sasa tunaweza kuelewa jambo ambalo Yehova alitaka tujue alipouliza swali linalotajwa kwenye Isaya 49:15. Jambo analofanya hapa si kulinganisha tu, bali ni kutofautisha. Tofauti na mama wasio wakamilifu, ambao huenda wakashindwa kuwahurumia watoto wao wachanga, Yehova hatakosa wala hatasahau kamwe kuwaonyesha huruma waabudu wake wenye uhitaji. Kwa kufaa, kitabu cha marejeo ambacho kimetajwa kinasema hivi kuhusu Isaya 49:15: “Huo ndio wonyesho wenye nguvu zaidi wa upendo wa Mungu unaotajwa katika Agano la Kale.”

Je, si jambo lenye kufariji kujifunza kuhusu “huruma nyororo za Mungu wetu”? (Luka 1:78) Tunakutia moyo ujifunze jinsi unavyoweza kumkaribia Yehova zaidi. Mungu huyu mwenye upendo anawahakikishia waabudu wake hivi: ‘Sitawaacha wala kuwatupa hata kidogo.’—Waebrania 13:5.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Februari:

Isaya 43-62