Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulitoka Wapi?

Tulitoka Wapi?

Tulitoka Wapi?

KWA NINI JIBU LA SWALI HILO NI LA MAANA? Watu wengi wanafundishwa kwamba uhai ulitokea duniani kimuujiza tu. Wanaambiwa kwamba matukio fulani yalitukia yenyewe tu bila mpango na kutokeza wanadamu kupitia mageuzi, wakiwa na uwezo wao wa kihisia, kiakili, na tamaa ya kujua kusudi la maisha.

Lakini fikiria hili: Kwa kweli ikiwa tulitokana na mageuzi na hakuna Muumba, kwa njia fulani wanadamu wangekuwa mayatima. Wanadamu hawangekuwa na mtu mwenye hekima ya juu zaidi wa kumwomba mashauri. Hatungekuwa na mtu wa kutusaidia kusuluhisha matatizo yetu. Tungelazimika kutegemea hekima ya wanadamu ili kuepuka misiba ya kimazingira, kusuluhisha migogoro ya kisiasa, na kushughulikia matatizo ya kibinafsi.

Je, wazo hilo linakuletea amani ya akili? Ikiwa sivyo, fikiria kuhusu kumtegemea mtu mwenye hekima inayozidi ya wanadamu. Wazo hilo halituvutii tu bali pia linapatana na akili.

Yale Ambayo Biblia Inasema

Biblia inafundisha kwamba wanadamu waliumbwa moja kwa moja na Mungu. Hatukutokana na mageuzi ambayo hayategemei akili. Badala yake, sisi ni watoto wa Baba mwenye upendo na mwenye akili. Ona habari zifuatazo ambazo zinasemwa wazi katika Biblia.

Mwanzo 1:27. “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.”

Zaburi 139:14. “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha. Kazi zako ni za ajabu, kama vile nafsi yangu inavyojua vema.”

Mathayo 19:4-6. “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”

Matendo 17:24, 25. “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama Huyu alivyo, Bwana wa mbingu na dunia, hakai katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono, wala hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote, kwa sababu yeye mwenyewe huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.”

Ufunuo 4:11. “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.”

Jinsi Jibu la Biblia Linavyoleta Amani ya Kweli ya Akili

Kujua kwamba “kila familia . . . duniani hupata jina kutokana” na Mungu kunabadili maoni yetu kuhusu watu wengine. (Waefeso 3:15) Kuwa na ujuzi huo pia kunaongoza jinsi tunavyojiona na kuona matatizo yetu. Fikira zetu zitabadilika katika njia zifuatazo.

Tunapokabili maamuzi mazito, hatutahangaishwa kupita kiasi na maoni ya watu yenye kupingana. Badala yake, tutategemea kabisa mashauri ya Biblia. Kwa nini? Kwa sababu “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Timotheo 3:16, 17.

Ni kweli kwamba ili kufuata mashauri ya Biblia tunapaswa kujitahidi na kujitia nidhamu. Nyakati nyingine huenda mwongozo wake ukatulazimu kutenda kwa njia ambazo zinaonekana hazipatani na mwelekeo wetu. (Mwanzo 8:21) Hata hivyo, tukikubali kwamba tuliumbwa na Baba wa mbinguni mwenye upendo, ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba anajua njia bora zaidi ambayo tunapaswa kufuata. (Isaya 55:9) Neno lake linatuhakikishia hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” (Methali 3:5, 6) Tukitumia shauri hilo, mahangaiko mengi tunayopata tunapokabili matatizo na maamuzi yatakwisha.

Tunapobaguliwa, hatutalemewa na hisia za kujiona hatufai, na kufikiri kwamba kwa njia fulani hatuna thamani kama watu wa rangi au jamii nyingine. Badala yake, tutajiheshimu kwa usawaziko. Kwa nini? Kwa sababu Baba yetu, Yehova Mungu, “hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” —Matendo 10:34, 35.

Tukijua hivyo, hatutaruhusu ubaguzi utufanye tuwe na mtazamo mbaya kuelekea watu wengine. Tutaelewa kwamba hatuna sababu yoyote halali ya kujiona kuwa bora kuliko watu wa jamii nyingine, kwa kuwa Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima.”—Matendo 17:26.

Bila shaka, kujua kwamba tuliumbwa na kwamba Muumba wetu anatujali ni msingi wa kupata amani ya kweli ya akili. Lakini tunahitaji kufanya mengi zaidi ili tudumishe amani ya ndani.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Je, wanadamu walitokana na mageuzi?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kujua kwamba Muumba wetu anatujali kunaweza kutuletea amani ya akili