Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufanikiwa Ukiwa Mama

Kufanikiwa Ukiwa Mama

Kufanikiwa Ukiwa Mama

LEO ulimwenguni pote, wanawake wengi wanafanya kazi ya kujiruzuku. Katika nchi zenye utajiri, wanawake wengi wanafanya kazi ya kuajiriwa kama wanaume. Katika nchi zinazoendelea, mara nyingi wanawake wanajikakamua kwa muda wa saa nyingi wakilima ili kusaidia kupata riziki ya familia zao.

Wanawake wengi wanafanya kazi ili kupata pesa wanazohitaji na pia wanajitahidi kutunza nyumba na familia zao. Wanawake hao hawapati tu pesa za kununua chakula, mavazi, na nyumba, lakini pia wanapika chakula, wanafua nguo, na kusafisha nyumba.

Zaidi ya hayo, mama Wakristo wanajitahidi kuwafundisha watoto wao viwango vya kiroho. “Kwa kweli, ni vigumu sana kuwa na usawaziko kati ya kazi na madaraka ya familia, hasa ikiwa una watoto wachanga,” anakiri Cristina, mama wa wasichana wawili. “Si rahisi kuwapa watoto uangalifu wote ambao wanahitaji.”

Ni nini kinachowachochea akina mama kufanya kazi ya kujiruzuku? Ni matatizo gani wanayokabili? Na je, ni lazima mama afanye kazi ya kimwili ili afanikiwe?

Kwa Nini Akina Mama Wanafanya Kazi

Mama wengi wanalazimika kufanya kazi ya wakati wote. Wengine hawana wenzi wa ndoa wa kuwasaidia kupata riziki. Wenzi wengine wa ndoa wanaona kwamba mshahara wa mtu mmoja hautoshi kabisa kugharimia mahitaji ya msingi ya familia.

Kwa kweli, si mama wote wanaofanya kazi kwa sababu za kiuchumi. Wengi wao wanafanya kazi ili waheshimiwe zaidi. Wengine huenda wanafanya kazi ili kujitegemea kifedha kwa kadiri fulani au ili kuishi maisha ya starehe. Wengi wanafanya kazi vizuri na wanaifurahia.

Huenda uvutano wa wengine ukawa sababu nyingine inayofanya akina mama wahisi wanalazimika kufanya kazi ya kimwili. Hata ingawa watu wengi wanatambua kwamba akina mama wanaofanya kazi kwa kawaida wanakabiliana na mifadhaiko na uchovu, wale ambao wameamua kutofanya kazi ya kimwili mara nyingi wanaeleweka vibaya, na hata wanadhihakiwa. Mwanamke mmoja anasema hivi: “Si rahisi kuwaeleza wengine kwamba wewe ni ‘mke wa nyumbani tu.’” Anaongeza hivi: “Watu fulani wanaonyesha kwa maneno au kwa ishara za uso kwamba unajiharibia maisha.” Rebeca, mama aliye na binti mwenye umri wa miaka miwili, anasema: “Ingawa jamii yetu inatambua kwamba wanawake wanapaswa kuwatunza watoto wao, ninahisi kwamba inawaona akina mama ambao hawafanyi kazi ya kimwili kuwa watu wa hali ya chini.”

Hadithi na Mambo ya Hakika

Katika maeneo fulani ulimwenguni, vyombo vya habari vinaonyesha kwamba “mwanamke aliye kielelezo” ni yule anayefanikiwa katika kazi yake, anayelipwa mshahara mkubwa, anayevalia vizuri, na anayejiamini kabisa. Anapofika nyumbani, ana uwezo wa kutatua matatizo ya watoto wake, kurekebisha makosa ya mume wake, na kushughulikia matatizo yoyote ya nyumbani. Ni wazi kwamba ni wanawake wachache  sana ambao wanaweza kutimiza viwango hivyo.

Kwa kweli, kazi nyingi ambazo wanawake wanapata ni za kuchosha na za mshahara mdogo. Huenda akina mama wafanyakazi wakakata tamaa wanapoona kwamba kazi yao haiwawezeshi kutumia kikamili uwezo wao mbalimbali. Kitabu kimoja (Social Psychology) kinasema hivi: “Ingawa kumekuwa na maendeleo ya [wanaume na wanawake] kutendewa kwa usawa, bado wanaume wanalipwa mshahara mkubwa zaidi na wana vyeo vikubwa zaidi. Kwa hiyo, wanawake wanaojaribu kupata heshima kutokana na cheo chao kazini wanakabili hatari ya pekee.” Gazeti moja la Kihispania (El País) linasema: “Imekadiriwa kwamba wanawake wanaweza kupata mfadhaiko unaosababishwa na mahangaiko mara tatu zaidi ya wanaume kwa kuwa wanawake wengi wana kazi mbili—kazini na nyumbani.”

Jinsi Waume Wanavyoweza Kusaidia

Bila shaka, mama Mkristo ndiye anayepaswa kuamua ikiwa atafanya au hatafanya kazi ya kimwili. Hata hivyo, ikiwa ameolewa, yeye na mume wake wanapaswa kufanya uamuzi huo baada tu ya kuzungumzia jambo hilo na kuchunguza kwa uangalifu mambo yote yanayohusika.—Methali 14:15.

Namna gani ikiwa wenzi wa ndoa wanaamua kwamba kwa sababu ya hali za kiuchumi, wote wawili wanalazimika kufanya kazi ya wakati wote? Ikiwa ndivyo, mume mwenye hekima atafikiria kwa uangalifu himizo hili la Biblia: “Ninyi waume mnapaswa kuonyesha uelewaji katika maisha yenu ya ndoa: watendeeni wake zenu kwa heshima, si kwa sababu tu wao ni dhaifu zaidi kimwili, bali pia kwa sababu zawadi ya Mungu ya uhai ni kitu mnachoshiriki pamoja.” (1 Petro 3:7, The Revised English Bible) Mume anamwonyesha mke wake heshima kwa kufikiria sana udhaifu wake wa kimwili na wa kihisia. Ikiwezekana, atamsaidia mke wake kufanya kazi za nyumbani. Kama Yesu, mume atakuwa tayari kufanya kwa unyenyekevu kazi za nyumbani, na hatakataa kufanya kazi hizo eti kwa sababu zinamshushia heshima. (Yohana 13:12-15) Badala yake, ataona kazi hizo kuwa nafasi ya kuonyesha kwamba anampenda mke wake mwenye bidii. Mke wake atathamini sana msaada huo.—Waefeso 5:25, 28, 29.

Bila shaka, ikiwa wenzi wote wawili wanafanya kazi ya kimwili, ni jambo la maana sana washirikiane nyumbani. Jambo hilo linakaziwa na ripoti ya gazeti moja la Hispania (ABC). Ikieleza kuhusu uchunguzi uliofanywa na Taasisi ya Masuala ya Familia, ripoti hiyo ilisema kwamba talaka zinaongezeka nchini Hispania kwa sababu ya “kuporomoka kwa viwango vya dini na vya maadili,” na pia kwa sababu ya mambo mengine mawili, yaani, “wanawake kufanya kazi ya kimwili na wanaume kukataa kuwasaidia kazi za nyumbani.”

Wajibu Muhimu wa Mama Mkristo

Ingawa Yehova anawapa akina baba daraka la msingi la kuwazoeza watoto wao, mama Wakristo wanajua kwamba wao pia wana wajibu wa maana, hasa mtoto akiwa mchanga. (Methali 1:8; Waefeso 6:4) Yehova alikuwa akizungumza na akina mama na baba alipowapa Waisraeli agizo la kukazia Sheria yake ndani ya watoto wao. Alijua kwamba jambo hilo lingehitaji wakati na subira, hasa katika miaka ya mapema ya mtoto. Kwa sababu hiyo, Mungu aliwaambia wazazi kwamba walipaswa kuwazoeza watoto wao nyumbani, barabarani, wanapoamka, na wanapolala.—Kumbukumbu la Torati 6:4-7.

Neno la Mungu linakazia wajibu muhimu na wenye heshima wa akina mama linapowaamuru watoto hivi: “Usiiache sheria ya mama yako.” (Methali 6:20) Bila shaka, mwanamke aliyeolewa atazungumza kwanza na mume wake kabla ya kuwapa watoto sheria yoyote. Hata hivyo, kama andiko hilo linavyoonyesha, mama wana haki ya kuweka sheria. Na watoto wanaotii sheria za kiroho na za maadili ambazo wanafundishwa na mama anayemwogopa Mungu watafaidika sana. (Methali 6:21, 22) Teresa, mama aliye na wavulana wawili, alieleza kwa nini hatafuti kazi ya kuajiriwa. Alisema hivi: “Kuwalea watoto wangu ili wamtumikie Mungu ndiyo kazi ya maana zaidi niliyo nayo. Ninataka kufanya kazi hiyo vizuri iwezekanavyo.”

Akina Mama Waliowasaidia Watoto Wao

Bila shaka, Mfalme Lemueli wa Israeli alifaidika sana kutokana na jitihada za mama yake. “Ujumbe mzito” ambao mama yake alimpa “ili kumrekebisha” umeandikwa katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (Methali 31:1; 2 Timotheo 3:16) Maelezo ya mama huyo kuhusu mke mwenye uwezo bado yanawasaidia vijana wa kiume kuchagua kwa hekima mwenzi wa ndoa. Na maonyo yake kuhusu upotovu wa maadili na kunywa kupita kiasi bado ni muhimu leo kama yalivyokuwa yalipoandikwa.—Methali 31:3-5, 10-31.

Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alisifu kazi nzuri iliyotimizwa na mama mmoja aliyeitwa Eunike ya kumfundisha mwana wake Timotheo. Kwa kuwa huenda mume wake ambaye hakuwa mwamini aliabudu miungu ya Wagiriki, Eunike alihitaji kumshawishi Timotheo ayaamini “maandishi matakatifu.” Eunike alianza wakati gani kumfundisha Timotheo Maandiko? Maandiko yaliyoongozwa na roho yanasema kwamba alianza “tangu utoto,” kwa maneno mengine, tangu Timotheo alipokuwa mchanga. (2 Timotheo 1:5; 3:14, 15) Ni wazi kwamba imani na kielelezo chake, na pia mafundisho yake, yalimtayarisha Timotheo kwa ajili ya utumishi wa umishonari.—Wafilipi 2:19-22.

Pia, Biblia inazungumza kuhusu akina mama ambao ukarimu wao kuelekea watumishi washikamanifu wa Mungu uliwawezesha watoto wao kupata vielelezo vizuri maishani. Kwa mfano, mwanamke Mshunamu alimkaribisha kwa ukawaida nabii Elisha nyumbani mwake. Baadaye, mwana wake alifufuliwa na Elisha. (2 Wafalme 4:8-10, 32-37) Fikiria pia mfano wa Maria, mama ya Marko, mwandikaji wa Biblia. Inaelekea alitoa nyumba yake huko Yerusalemu ili itumiwe kwa ajili ya mikutano ya wanafunzi wa mapema. (Matendo 12:12) Bila shaka, Marko alifaidika kwa kushirikiana na mitume na Wakristo wengine ambao walikuja kwa ukawaida nyumbani kwao.

Kwa wazi, Yehova anathamini sana kazi ya wanawake waaminifu ambao wanakazia kanuni zake ndani ya mioyo ya watoto wao. Anawapenda wanawake hao kwa sababu ya ushikamanifu wao na jitihada zao za kusitawisha mazingira ya kiroho katika nyumba zao.—2 Samweli 22:26; Methali 14:1.

Uamuzi Ulio Bora Zaidi

Kama mifano ya Kimaandiko tuliyozungumzia inavyoonyesha, kutimiza vizuri mahitaji ya familia kimwili, kiroho, na kihisia kunaleta baraka za pekee. Lakini si rahisi kufanya hivyo. Mara nyingi, kazi ya mama nyumbani inaonekana ngumu kuliko cheo chochote kikubwa kazini.

Ni kweli kwamba ikiwa mama, baada ya kutafuta mwongozo wa mume wake, anaamua kuacha kazi au kufanya kazi ya muda, huenda familia ikalazimika kupunguza kiwango cha maisha na huenda akadhihakiwa na wale ambao hawamwelewi. Lakini kujinyima kwake kunaweza kuleta baraka nyingi zaidi. Paqui ana watoto watatu na anafanya kazi ya muda. Anasema hivi: “Ninapenda kuwepo watoto wangu wanaporudi nyumbani kutoka shuleni ili wapate mtu wa kuzungumza nao.” Watoto wake wanafaidika kwa njia gani? “Ninawasaidia kufanya kazi zao za shule, na matatizo yanapotokea, ninaweza kuyashughulikia mara moja,” anasema. “Wakati tunaotumia pamoja kila siku unatusaidia kudumisha mawasiliano mazuri. Ninathamini sana wakati ninaotumia pamoja na watoto wangu hivi kwamba nilikataa kazi niliyopewa ya wakati wote.”

Mama wengi Wakristo wametambua kwamba wakiacha kazi au wakifanya kazi ya muda, washiriki wote wa familia wanafaidika. “Nilipoacha kazi ya kimwili, ilionekana kwamba matatizo ya familia yetu yalipungua,” anaeleza Cristina aliyetajwa mwanzoni. “Nilikuwa na wakati wa kuzungumza na watoto wangu na kumsaidia mume wangu katika njia nyingi. Nilianza kufurahia kuwafundisha mabinti wangu, na kuwaona wakijifunza na kufanya maendeleo.” Cristina anakumbuka hasa tukio fulani. “Mtoto wangu wa kwanza alijifunza kutembea kwenye kituo cha kutunzia watoto,” anakumbuka Cristina, “lakini mtoto wangu wa pili nilimfundishia nyumbani kutembea. Alianza kupiga hatua zake za kwanza na kuanguka mikononi mwangu. Pindi hiyo iliniletea uradhi mwingi sana!”

Jambo lingine la kufikiria ni kwamba mama anapokubali kupunguza kazi yake ya kimwili huenda matatizo ya kiuchumi yasiwe mengi kama anavyotarajia. Cristina anaeleza hivi: “Gharama za kuwatunza watoto na za usafiri zilimeza sehemu kubwa ya mshahara wangu. Tulipochunguza kwa makini hali yetu, tulitambua kwamba kazi yangu haikuwa ikituletea pesa nyingi za ziada.”

Baada ya kuchunguza hali yao, wenzi wengine wa ndoa wanaamua kwamba faida za mke kubaki nyumbani ili kuitunza familia kwa wakati wote ni nyingi zaidi kuliko kujinyima kifedha kwa kadiri yoyote ile. “Ninafurahi kwamba mke wangu anaweza kukaa nyumbani ili kuwatunza watoto wetu wawili,” anasema Paul, mume wa Cristina. “Tulikuwa na mfadhaiko mkubwa sana mke wangu alipokuwa akifanya kazi.” Uamuzi huo umekuwa na matokeo gani juu ya mabinti wao wawili? Paul anasema hivi: “Wanajihisi salama zaidi na pia wanalindwa sana kutokana na uvutano mbaya katika miaka yao ya mapema.” Kwa nini wenzi hao wa ndoa wanahisi kwamba ni jambo la maana sana kwao kutumia wakati mwingi iwezekanavyo pamoja na mabinti wao? Paul anajibu: “Nina hakika kwamba sisi wazazi tusipoelekeza mioyo na akili za watoto wetu, mtu  mwingine  atafanya hivyo.”

Kwa wazi, wenzi wote wa ndoa wanapaswa kuchunguza hali zao, na hakuna mtu anayepaswa kuchambua uamuzi ambao huenda wengine wakafanya. (Waroma 14:4; 1 Wathesalonike 4:11) Hata hivyo, inafaa kufikiria faida nyingi ambazo familia inapata mama asipofanya kazi ya kuajiriwa ya wakati wote. Akizungumzia kwa ufupi  hisia zake  kuhusu  habari  hii,  Teresa,  aliyetajwa mapema, anasema hivi: “Hakuna jambo linalomfanya mtu ahisi amefanikiwa kuliko kutumia wakati mwingi iwezekanavyo kuwatunza na kuwafundisha watoto wake mwenyewe.”—Zaburi 127:3.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mama Wakristo wanashiriki katika kazi ya maana sana ya kuwazoeza watoto wao