Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Baraka za Yehova Zimenitajirisha

Baraka za Yehova Zimenitajirisha

NILIZALIWA mwaka wa 1927 kwenye mji mdogo wa Wakaw, Saskatchewan, Kanada. Baba na mama walikuwa na watoto saba; wavulana wanne na wasichana watatu, kwa hiyo nilijifunza kuishi na watu tangu utotoni.

Familia yetu iliathiriwa na hali mbaya ya uchumi katika miaka ya 1930, iliyojulikana kama Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi. Hatukuwa matajiri, lakini hatukukosa chakula. Tulifuga kuku na ng’ombe, kwa hiyo tulikuwa na mayai mengi, maziwa, jibini, na siagi. Hivyo kila mmoja kwenye familia yetu alisaidia kutunza mifugo na kazi za nyumbani.

Tulifurahia mambo mengi mazuri. Kwa mfano, Baba alipoenda mjini kuuza mazao wakati wa msimu wa vuli, mara nyingi alirudi na boksi la matofaa yaliyotoka kuvunwa. Bado ninakumbuka harufu nzuri ya matofaa iliyoenea nyumbani kwetu!

FAMILIA YETU YAJIFUNZA KWELI

Nilikuwa na umri wa miaka sita wazazi wangu walipojifunza kweli. Mwana wao wa kwanza, Johnny, alikufa muda mfupi tu baada ya kuzaliwa. Wakiwa wamefadhaika, wazazi wangu walimuuliza kasisi, “Johnny ameenda wapi?” Kasisi alisema kwamba mtoto huyo hakuwa amebatizwa, hivyo hakwenda mbinguni. Badala yake, alikuwa toharani. Pia kasisi alisema kwamba ikiwa wazazi wangu wangempa pesa, angesali ili Johnny atoke toharani na kwenda mbinguni. Ungekuwa wewe, ungehisije? Baba na Mama walikata tamaa sana kiasi kwamba hawakuzungumza tena na kasisi huyo. Lakini, bado walijiuliza Johnny alienda wapi.

Siku moja Mama alipata kitabu kinachoitwa Wafu Wako Wapi? ambacho kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova. Alikisoma kwa makini sana. Baba aliporudi nyumbani, alimwambia hivi kwa msisimko: “Ninajua Johnny yuko wapi! Amelala sasa, lakini siku moja ataamka.” Jioni hiyo Baba alikisoma kitabu chote. Mama na Baba walifarijika sana kujua kuwa Biblia inasema kwamba wafu wamelala na wakati ujao kutakuwa na ufufuo.—Mhu. 9:5, 10; Mdo. 24:15.

Mambo waliyojifunza yalibadili kabisa maisha yetu, kwa kuwa tulipata faraja na furaha. Mama na Baba walianza kujifunza Biblia na Mashahidi na kuhudhuria mikutano katika kutaniko dogo huko Wakaw, ambalo lilikuwa na washiriki wengi wenye asili ya Ukrainia. Baada ya muda mfupi, Mama na Baba wakaanza kuhubiri.

Muda mfupi baadaye tulihamia British Columbia, na tulipofika huko ndugu na dada walitukaribisha kwa uchangamfu. Tulifurahia sana kutayarisha Mnara wa Mlinzi kwa ajili ya mikutano ya Jumapili tukiwa familia. Sote tulimpenda sana Yehova na kweli ya Biblia. Niliona jinsi Yehova alivyotubariki.

Tulipokuwa watoto, haikuwa rahisi kwetu kuwaeleza wengine mambo tunayoamini. Hata hivyo, jambo lililotusaidia ni kwamba kila mwezi tulitayarisha utangulizi utakaotumiwa katika utumishi wa shambani, na tulitoa onyesho katika Mkutano wa Utumishi kuhusu jinsi tunavyoweza kutumia utangulizi huo. Ingawa tulikuwa na aibu, njia hiyo ilitusaidia sana kujifunza kuzungumza na wengine kuhusu Biblia. Mazoezi ya kuhubiri tuliyopata wakati huo yamenisaidia sana!

Jambo moja tulilofurahia utotoni ni kuwakaribisha watumishi wa wakati wote nyumbani. Kwa mfano, tulifurahia sana kumkaribisha mwangalizi wa mzunguko, Jack Nathan, alipotembelea kutaniko letu. * Alitusimulia mambo mengi mazuri, na pongezi zake zilichochea tamaa yetu ya kumtumikia Yehova kwa uaminifu.

Wakati huo niliwaza hivi, “Nitakapokuwa mkubwa, ninataka niwe kama Ndugu Nathan.” Baadaye nilitambua kwamba mfano wake mzuri ulinitayarisha kwa ajili ya utumishi wa wakati wote. Nilipofikia umri wa miaka 15, niliazimia kumtumikia Yehova. Mwaka wa 1942, mimi na Eva tulibatizwa.

MAJARIBU YA IMANI

Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu uzalendo ulipokuwa umepamba moto, Bi. Scott, mwalimu aliyechukia msimamo wetu, aliwafukuza shule wadogo zangu watatu. Kwa nini? Kwa sababu walikataa kusalimu bendera. Kisha Bi. Scott aliwasiliana na mwalimu wangu na kumchochea anifukuze shule. Lakini mwalimu wangu alimwambia, “Tunaishi katika nchi huru, na tuna haki ya kukataa kushiriki kwenye shughuli zozote za kizalendo.” Ijapokuwa Bi. Scott alimshinikiza sana, mwalimu wangu alimwambia hivi kwa uthabiti: “Huo ni uamuzi wangu.”

Bi. Scott alimjibu hivi: “Hapana, huo si uamuzi wako. Nitakushtaki usipomfukuza shule Melita.” Mwalimu aliwaeleza wazazi wangu kuwa alilazimika kunifukuza shule hata ingawa aliamini kwamba haikuwa sawa kufanya hivyo, kwa kuwa aliogopa kupoteza kazi yake. Hata hivyo, tulifanikiwa kupata vifaa vilivyotusaidia kuendelea na masomo yetu tukiwa nyumbani. Baada ya muda, tulihamia eneo lililokuwa umbali wa kilometa 32 kutoka mahali tulipoishi, ambapo tulikubaliwa kujiunga na shule nyingine.

Machapisho yetu yalipigwa marufuku wakati wa vita, lakini tulitumia Biblia kuhubiri nyumba kwa nyumba. Matokeo ni kwamba tuliboresha ustadi wetu wa kutumia Maandiko tulipokuwa tukihubiri habari njema za Ufalme. Jambo hilo lilitusaidia kukua kiroho na tulijionea jinsi Yehova alivyotutegemeza.

NAANZA UTUMISHI WA WAKATI WOTE

Nilikuwa na kipawa cha kutengeneza nywele na hata nilipata tuzo kadhaa

Mara baada ya mimi na Eva kumaliza masomo, tulianza upainia. Mwanzoni nilifanya kazi ya kuuza duka ili kujiruzuku. Baadaye, nilisoma kozi ya miezi sita ya kutengeneza nywele, jambo ambalo nilipenda sana kufanya nilipokuwa nyumbani. Nilifanya kazi saluni siku mbili kwa juma, na mara mbili kwa mwezi niliwafundisha watu kutengeneza nywele. Hivyo niliweza kujiruzuku na kuendelea na utumishi wa wakati wote.

Mwaka wa 1955, nilipanga kuhudhuria kusanyiko lenye kichwa “Ufalme Wenye Ushindi” jijini New York City, Marekani, na Nuremberg, Ujerumani. Hata hivyo, kabla sijaenda New York nilikutana na Ndugu Nathan Knorr kutoka makao makuu. Yeye na mke wake walikuja kuhudhuria kusanyiko jijini Vancouver, Kanada. Wakati huo, niliombwa nimtengeneze nywele Dada Knorr. Ndugu Knorr alipenda jinsi nilivyotengeneza nywele za mke wake na akataka kukutana nami. Tulipokuwa tukizungumza, nilimweleza kuwa ninatarajia kwenda New York kabla ya kuelekea Ujerumani. Alinialika nifanye kazi Betheli ya Brooklyn kwa siku tisa.

Safari hiyo ilibadili maisha yangu. Nikiwa New York, nilikutana na ndugu aliyeitwa Theodore (Ted) Jaracz. Muda mfupi baada ya kukutana naye, nilishangaa aliponiuliza, “Je, wewe ni painia?” Nilimjibu, “Hapana.” Rafiki yangu LaVonne alisikia swali hilo naye akaingilia mazungumzo yetu na kusema, “Ndiyo, yeye ni painia.” Akiwa ametatizika, Ted akamuuliza LaVonne, “Ni nani anayejua ukweli, wewe au yeye?” Nilimweleza kwamba niliwahi kuwa painia na ninakusudia kuanza tena punde tu nitakaporudi nyumbani.

NAKUTANA NA MWANAUME WA KIROHO

Ted alizaliwa Kentucky, Marekani mwaka wa 1925, na alibatizwa akiwa na umri wa miaka 15. Ingawa hakuna yeyote katika familia yao aliyekubali kweli, Ted alianza upainia baada ya miaka miwili. Aliendelea na utumishi wa wakati wote kwa miaka 67 hivi.

Mnamo Julai 1946, akiwa na umri wa miaka 20, Ted alihitimu darasa la saba la Shule ya Gileadi. Baada ya kuhitimu, alitumikia akiwa mwangalizi anayesafiri huko Cleveland, Ohio. Miaka minne hivi baadaye, alipewa mgawo wa kutumikia akiwa mtumishi wa tawi nchini Australia.

Ted alihudhuria kusanyiko huko Nuremberg, Ujerumani, na tulitumia wakati pamoja. Tukaanza kupendana. Nilifurahi kwa sababu lengo lake kuu maishani lilikuwa kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. Alitimiza majukumu yake kwa moyo wote na kwa umakini, lakini alikuwa mwenye fadhili na alishirikiana vizuri na watu. Alitanguliza masilahi ya wengine badala ya faida zake. Baada ya kusanyiko hilo, Ted alirudi Australia na mimi nilirudi Vancouver. Lakini tuliendelea kuwasiliana kwa barua.

Baada ya kutumikia kwa miaka mitano hivi huko Australia, Ted alirudi Marekani na kisha akahamia Vancouver ili kufanya upainia. Nilifurahi sana kwa kuwa familia yangu ilimpenda. Kaka yangu, Michael, alikuwa akinichunga sana, na mara nyingi hakufurahia kuona vijana wakivutiwa nami. Hata hivyo, kwa muda mfupi Michael alimpenda sana Ted. Alisema hivi: “Melita, umepata mwanaume mzuri. Umtendee vizuri na uwe mwangalifu usimpoteze.”

Baada ya kufunga ndoa mwaka wa 1956, tulifanya utumishi wa wakati wote kwa miaka mingi sana

Mimi pia nilimpenda sana Ted. Tulifunga ndoa Desemba 10, 1956. Tulifanya upainia pamoja jijini Vancouver, kisha California, na baadaye tulipewa mgawo wa kuyatembelea makutaniko katika eneo la Missouri na Arkansas. Kwa miaka 18 hivi, tuliishi katika nyumba tofauti kila juma tulipoyatembelea makutaniko mbalimbali nchini Marekani. Tulijionea mambo mengi mazuri katika huduma, na tulishirikiana vizuri na ndugu na dada. Ingawa haikuwa rahisi kuhama kutoka eneo moja hadi lingine kila juma, tulifurahia sana kuyatembelea makutaniko.

Nilimheshimu sana Ted kwa sababu sikuzote alithamini uhusiano wake na Yehova. Alipenda sana kumtumikia Muumba wa ulimwengu wote. Tulipenda kusoma na kujifunza Biblia pamoja. Usiku, kabla ya kulala, tulipiga magoti pembeni ya kitanda, na tulisali pamoja. Kisha kila mmoja alitoa sala yake. Sikuzote nilijua ikiwa kuna jambo linamsumbua Ted, kwani angetoka kitandani, angepiga magoti tena, na kusali kimyakimya kwa muda mrefu. Mazoea yake ya kusali kwa Yehova kuhusu mambo makubwa na madogo yalifanya nimheshimu sana.

Miaka kadhaa baada ya kuoana, Ted alinieleza kuwa angeanza kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho. Aliniambia hivi: “Nimesali sana ili niwe na uhakika kwamba ninafanya jambo ambalo Yehova anataka nifanye.” Sikushangaa sana kujua kwamba ametiwa mafuta kwa roho ya Mungu ili akaishi mbinguni. Ilikuwa heshima kubwa sana kwangu kumuunga mkono ndugu ya Yesu.—Mt. 25:35-40.

MGAWO MPYA

Mwaka wa 1974, Ted alipata mwaliko wa kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Baada ya muda, tulialikwa Betheli ya Brooklyn. Ted alipokuwa akitimiza majukumu yake katika Baraza Linaloongoza, mimi nilifanya kazi ya usafi au kutengeneza nywele.

Majukumu ya Ted yalihusisha kutembelea ofisi mbalimbali za tawi. Alivutiwa hasa na kazi ya kuhubiri katika nchi ambazo kazi yetu ilipigwa marufuku, kama vile nchi za Ulaya Mashariki zilizokuwa chini ya Muungano wa Sovieti. Wakati fulani, tulipokuwa likizo nchini Sweden, Ted alisema: “Melita, kazi ya kuhubiri imepigwa marufuku nchini Poland, na ningependa kuwasaidia akina ndugu nchini humo.” Kwa hiyo tulitafuta viza na kwenda Poland. Ted alikutana na ndugu waliosimamia kazi yetu, nao wakaenda eneo la mbali ili mtu yeyote asisikie mazungumzo yao. Ndugu hao walifanya mkutano kwa siku nne, lakini nilifurahia sana kumwona Ted akiwa na shangwe kwa sababu ya kuisaidia familia yake ya kiroho.

Tulitembelea tena Poland Novemba 1977. Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwa washiriki wa Baraza Linaloongoza, F. W. Franz, Daniel Sydlik, na Ted kufanya ziara rasmi nchini humo. Bado kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku, hata hivyo washiriki hao wa Baraza Linaloongoza walifanikiwa kuzungumza na waangalizi, mapainia, na Mashahidi waliotumikia kwa muda mrefu katika majiji mbalimbali.

Ted na wengine wakiwa katika Wizara ya Sheria jijini Moscow baada ya kazi yetu kusajiliwa kisheria

Milton Henschel na Ted walipotembelea Poland mwaka uliofuata, walikutana na maofisa wa serikali ambao hawakupinga sana kazi yetu. Mwaka wa 1982, serikali ya Poland iliwaruhusu ndugu zetu wafanye kusanyiko la siku moja. Mwaka uliofuata, makusanyiko makubwa yalifanywa, na mengi yalifanywa katika majumba ya kukodi. Mwaka wa 1985, marufuku ilipokuwa ikiendelea, tuliruhusiwa kufanya makusanyiko manne kwenye viwanja vikubwa. Mnamo Mei 1989, mipango ya kufanya makusanyiko makubwa zaidi ilipokuwa ikiendelea, serikali ya Poland iliondoa marufuku na Mashahidi wa Yehova wakatambuliwa kisheria. Ted alifurahia sana jambo hilo.

Kusanyiko la wilaya nchini Poland

KUKABILIANA NA MATATIZO YA AFYA

Mwaka 2007, tulikuwa njiani kwenda Afrika Kusini ili kuhudhuria wakfu wa ofisi ya tawi. Tukiwa Uingereza, Ted alipata tatizo la shinikizo la damu, hivyo daktari alimshauri aahirishe safari yake. Ted alipopata nafuu, tulirudi Marekani. Lakini majuma machache baadaye, alipatwa na kiharusi kilichomfanya apooze upande wa kulia.

Ted hakupona haraka, na mwanzoni hangeweza kwenda ofisini. Hata hivyo, tulishukuru sana kwa sababu hakupoteza uwezo wake wa kuzungumza. Licha ya tatizo hilo, Ted alijitahidi sana kufanya kazi zake kama kawaida, hata alishiriki mikutano ya kila juma ya Baraza Linaloongoza kupitia simu akiwa chumbani.

Ted alithamini sana matunzo aliyopata Betheli alipokuwa akiugua. Alianza kupata nafuu hatua kwa hatua. Aliweza kutimiza baadhi ya migawo yake ya kitheokrasi, na sikuzote alikuwa mchangamfu.

Miaka mitatu baadaye, alipata tena kiharusi naye akafa siku ya Jumatano, Juni 9, 2010. Ingawa sikuzote nilijua kwamba Ted angemaliza mwendo wake wa kidunia, siwezi kueleza uchungu niliohisi alipokufa na jinsi ninavyomkosa sana. Hata hivyo, kila siku ninamshukuru Yehova kwa mambo yote niliyoweza kufanya ili kumsaidia Ted. Tulifurahia utumishi wa wakati wote tukiwa pamoja kwa zaidi ya miaka 53. Ninamshukuru Yehova kwa jinsi Ted alivyonisaidia nimkaribie zaidi Baba yangu wa mbinguni. Sasa nina uhakika kwamba anafurahia sana mgawo wake mpya.

CHANGAMOTO MPYA MAISHANI MWANGU

Nilifurahia sana kufanya kazi na kuwazoeza wengine katika saluni ya Betheli

Si rahisi kukabiliana na changamoto za sasa baada ya kuishi miaka mingi na yenye furaha pamoja na mume wangu. Mimi na Ted tulipenda sana kukutana na wageni hapa Betheli na katika Jumba la Ufalme. Kwa kuwa sasa mpenzi wangu Ted hayupo na sina nguvu kama zamani, siwezi kushirikiana na watu wengi. Hata hivyo, bado ninafurahia kuwa pamoja na ndugu na dada zangu wapendwa hapa Betheli na kutanikoni. Ratiba ya Betheli si rahisi, lakini ni shangwe kubwa sana kumtumikia Mungu kwa njia hii. Bado ninapenda sana kazi ya kuhubiri. Ingawa ninachoka na siwezi kusimama kwa muda mrefu, ninafurahia sana kuhubiri barabarani na kuwafundisha watu Biblia.

Kuona mambo mabaya yanayotukia ulimwenguni, kumenifanya nithamini sana baraka ya kumtumikia Yehova pamoja mume mzuri sana! Kwa kweli, baraka za Yehova zimenitajirisha.—Met. 10:22.

^ fu. 13 Simulizi la maisha la Jack Nathan lilichapishwa kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1990, ukurasa wa 10-14.