Mjane wa Sarefathi Alithawabishwa kwa Sababu ya Imani Yake

Mjane wa Sarefathi Alithawabishwa kwa Sababu ya Imani Yake

MJANE maskini anamkumbatia mwana wake wa pekee. Haamini macho yake. Muda mfupi tu uliopita, alikuwa amembeba mwana wake aliyekufa. Sasa, mwanamke huyo anamtazama mwana wake aliyefufuliwa na kusisimka anapomwona akitabasamu. Mgeni wake anamwambia hivi: “Tazama, mwana wako yuko hai.”

Ufufuo huo ulitukia miaka 3,000 hivi iliyopita. Unaweza kusoma simulizi hilo katika kitabu cha 1 Wafalme sura ya 17. Eliya, nabii wa Mungu ndiye mgeni wake. Ni nani mama ya mtoto huyo aliyekufa? Ni mjane anayeishi katika mji wa Sarefathi ambaye jina lake halitajwi. Ufufuo wa mwana wake ni mojawapo ya matukio yaliyoimarisha sana imani yake. Tutajifunza mambo muhimu sana kwa kuchunguza simulizi hilo.

ELIYA AMPATA MJANE MWENYE IMANI

Yehova alikusudia kuleta ukame wa muda mrefu katika ufalme wa Ahabu, mfalme mwovu wa Israeli. Baada ya Eliya kutangaza kwamba kungekuwa na ukame, Mungu alimficha ili Ahabu asimwangamize na pia alimlisha kimuujiza nabii huyo kwa kumpa mkate na nyama zilizoletwa na kunguru. Kisha, Yehova alimwambia Eliya hivi: “Ondoka, nenda Sarefathi, wa Sidoni, nawe ukae huko. Tazama! Nitamwamuru mwanamke fulani huko, mjane, akupe chakula.” —1 Fal. 17:1-9.

Eliya alipofika Sarefathi, alimwona mjane maskini akikusanya kuni. Je, huyo ndiye mwanamke ambaye angemwandalia nabii huyo chakula? Angefanyaje hivyo akiwa maskini sana? Licha ya shaka yoyote ambayo huenda Eliya alikuwa nayo, alianza kuzungumza na mwanamke huyo. Akamwambia hivi: “Tafadhali, niletee maji kidogo katika chombo ninywe.” Mwanamke huyo alipokuwa akienda kuyaleta, Eliya akamwambia: “Tafadhali, niletee kipande cha mkate.” (1 Fal. 17:10, 11) Haikuwa vigumu kwa mjane huyo kumpa mgeni kinywaji, lakini haikuwa rahisi kumpa mkate.

 Mwanamke huyo akasema hivi: “Kama anavyoishi Yehova Mungu wako, mimi sina keki yoyote ya mviringo, isipokuwa mkono mmoja tu wa unga katika mtungi mkubwa na mafuta kidogo katika mtungi mdogo; na tazama, ninakusanya kuni chache, nami nitaenda kutayarisha kitu kwa ajili yangu na mwanangu, nasi tutakula chakula hicho na kufa.” (1 Fal. 17:12) Mazungumzo hayo yanafunua nini? Hebu tuone.

Mjane huyo alijua kwamba Eliya ni Mwisraeli aliyemwogopa Mungu. Maneno haya aliyosema yanaonyesha hivyo: “Kama anavyoishi Yehova Mungu wako.” Inaonekana kwamba alimjua Yehova, Mungu wa Israeli kwa kadiri fulani ingawa hakumwita ‘Mungu wake.’ Aliishi Sarefathi, mji “wa” Sidoni au uliotegemea jiji la Sidoni huko Foinike. Inaelekea kwamba wakaaji wa Sarefathi waliabudu Baali. Hata hivyo, Yehova aliona sifa fulani ya pekee ya mjane huyo.

Mjane maskini wa Sarefathi alionyesha imani licha ya kwamba aliishi miongoni mwa watu walioabudu sanamu. Yehova alimtuma Eliya kwa mjane huyo ili wote wawili waokolewe. Tunajifunza jambo muhimu kutokana na hilo.

Baadhi ya wakaaji wa Sarefathi walioabudu Baali hawakuwa na moyo mwovu. Yehova alipomtuma Eliya kwa mjane huyo, alionyesha kwamba Anaona watu wenye nia njema ambao hawajaanza Kumtumikia. Kwa kweli, “katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa [Mungu] na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Mdo. 10:35.

Ni watu wangapi wanaoishi katika eneo lenu walio kama yule mjane wa Sarefathi? Ingawa huenda wamezungukwa na wafuasi wa dini ya uwongo, labda wanatamani kitu bora zaidi. Huenda wanamjua Yehova kwa kadiri fulani au labda hawamjui, hivyo wanahitaji msaada ili waikubali ibada safi. Je, unawatafuta na kuwasaidia watu hao?

“UNITAYARISHIE KWANZA KEKI NDOGO YA MVIRINGO”

Fikiria kwa makini jambo ambalo Eliya alimwomba mjane huyo afanye. Mjane huyo alikuwa amemwambia kwamba angetayarisha chakula cha mwisho kwa ajili yake na mwanaye, kisha wangekula chakula hicho na kufa. Lakini Eliya alisemaje? “Usiogope. Nenda, fanya kulingana na neno lako. Ila tu unitayarishie kwanza keki ndogo ya mviringo kutokana na kile kilichopo, nawe uniletee hiyo, na unaweza kutayarisha kitu kwa ajili yako na mwana wako baadaye. Kwa maana Yehova Mungu wa Israeli, amesema hivi, ‘Ule mtungi mkubwa wa unga hautamalizika, na ule mtungi mdogo wa mafuta hautapungua mpaka siku Yehova atakapoleta mvua juu ya uso wa nchi.’”—1 Fal. 17:11-14.

Huenda wengine wangesema, ‘Siwezi kamwe kumpa chakula chetu cha mwisho.’ Lakini mjane huyo hakusema hivyo. Ingawa hakujua mambo mengi kumhusu Yehova, alimwamini Eliya na kufanya jambo aliloambiwa. Hilo lilikuwa jaribu kubwa sana la imani, na mjane huyo alifanya uamuzi wa hekima kwelikweli.

Imani ya mjane huyo katika Yehova, Mungu wa Eliya, ilimwokoa yeye na mwana wake

Mungu hakumwacha mjane huyo maskini. Kama Eliya alivyoahidi, Yehova aliongeza unga na mafuta kidogo waliyokuwa nayo hivi kwamba Eliya, yule mjane, na mwana wake waliendelea kupata chakula hadi ukame ulipoisha. Kwa kweli, “ule mtungi mkubwa wa unga haukumalizika, wala ule mtungi mdogo wa mafuta haukupungua, kulingana na neno la Yehova alilokuwa amesema kupitia Eliya.” (1 Fal. 17:16; 18:1) Ikiwa mwanamke huyo angetenda kwa  njia tofauti, huenda keki aliyooka kwa mafuta na unga kidogo aliokuwa nao ingekuwa mlo wake wa mwisho. Badala yake, alitenda kwa imani, akamtegemea Yehova, na kumpa Eliya chakula.

Hilo linatufundisha kwamba Mungu huwabariki wale wanaotenda kwa imani. Unapokabili jaribu la utimilifu, Yehova atakusaidia ukionyesha imani. Yeye atakusaidia unapokabili jaribu kwa kuwa Mwandalizi, Mlinzi, na Rafiki yako.—Kut. 3:13-15.

Katika mwaka wa 1898, gazeti la Zion’s Watch Tower lilitaja jambo hili tunalojifunza kutokana na simulizi la mjane huyo: “Kama mwanamke huyo angetii kwa imani, basi angestahili kusaidiwa na Bwana kupitia Nabii huyo; ikiwa hangeonyesha imani, huenda mjane mwingine mwenye imani angepatikana. Ndivyo ilivyo kwetu pia,—wakati fulani katika safari yetu maishani Bwana huruhusu hali zinazojaribu imani yetu. Tukionyesha imani tutapata baraka; tusipoonyesha imani, tutakosa baraka hizo.”

Tunapokabili majaribu, tunahitaji kutafuta mwongozo wa Mungu kutoka katika Maandiko na machapisho yetu yanayotegemea Biblia. Kisha tunapaswa kutenda kupatana na mwongozo wa Yehova hata ikiwa ni vigumu sana kwetu kukubali mwongozo huo. Kwa kweli tutabarikiwa tukitenda kupatana na methali hii yenye hekima: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Met. 3:5, 6.

‘JE, UMEKUJA KUMUUA MWANANGU?’

Imani ya mjane huyo ingejaribiwa tena. Simulizi la Biblia linasema hivi: “Na ikawa kwamba baada ya mambo hayo mwana wa yule mwanamke, bimkubwa wa ile nyumba, akawa mgonjwa, na ugonjwa wake ukawa mkali sana hivi kwamba hapakuwa na pumzi iliyobaki ndani yake.” Akijaribu kutafuta chanzo cha msiba huo, mama huyo aliyekuwa akiomboleza alimwambia Eliya hivi: “Nina nini nawe, Ee mtu wa Mungu wa kweli? Umekuja kwangu ili kurudisha kumbukumbu la kosa langu na kumuua mwanangu.” (1 Fal. 17:17, 18) Maneno hayo ya uchungu yanamaanisha nini?

Je, huenda dhamiri ya mwanamke huyo ilimsumbua kwa sababu ya dhambi aliyofanya zamani? Je, alifikiri kwamba Mungu alikuwa akilipiza kisasi kwa kumuua mwana wake na kwamba Eliya alikuwa mjumbe aliyetumwa na Mungu kuleta kifo? Biblia haituelezi, hata hivyo, jambo moja liko wazi: Mjane huyo hakumlaumu Mungu kwa sababu ya ukosefu wowote wa uadilifu.

Huenda Eliya alishtushwa na kifo cha mwana wa mjane huyo na dai la mjane huyo kwamba nabii huyo ndiye aliyesababisha kifo cha mwana wake. Baada ya kumpeleka mwana huyo juu katika chumba cha darini, Eliya akapaaza sauti na kusema hivi: “Ee Yehova Mungu wangu, je, tena unaleta mabaya juu ya mjane ninayekaa naye kwa kumuua mwana wake?” Nabii huyo hangeweza kuvumilia jina la Mungu liendelee kulaumiwa ikiwa mwanamke huyo mwenye fadhili na mkarimu angeendelea kuteseka. Eliya akasihi hivi: “Ee Yehova, Mungu wangu, tafadhali, irudishe nafsi ya mtoto huyu ndani yake.”—1 Fal. 17:20, 21.

“TAZAMA, MWANA WAKO YUKO HAI”

Yehova alikuwa akisikiliza. Mjane huyo alitenda kwa imani kwa kumpa chakula nabii Wake. Inaonekana kwamba Mungu aliruhusu mvulana huyo afe kutokana na ugonjwa kwa sababu alijua kwamba angemfufua. Ufufuo huo wa kwanza kutajwa katika Maandiko ungeleta tumaini kwa vizazi vya wakati ujao. Yehova alimfufua mwana huyo baada ya kusihiwa na Eliya. Hebu wazia shangwe ya mjane huyo Eliya aliposema hivi: “Tazama, mwana wako yuko hai”!3 Kisha mjane huyo akamwambia hivi Eliya: “Kwa kweli sasa najua kwamba wewe ni mtu wa Mungu na kwamba neno la Yehova kinywani mwako ni la kweli.”—1 Fal. 17:22-24.

Simulizi la 1 Wafalme sura ya 17 halisemi mengi zaidi kumhusu mwanamke huyo. Hata hivyo, tukizingatia jinsi Yesu alivyomsifu, inaonekana kwamba aliendelea kuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova hadi alipokufa. (Luka 4: 25, 26) Simulizi hilo linatufunza kwamba Mungu anawabariki wale wanaowatendea mema watumishi wake. (Mt. 25: 34-40) Linathibitisha kwamba Mungu huwaandalia walio waaminifu mahitaji yao, hata wanapokabili hali ngumu sana. (Mt. 6: 25-34) Simulizi hilo linatuthibitishia pia kwamba Yehova anatamani na anaweza kuwafufua wafu. (Mdo. 24:15) Kwa kweli, hizo ni sababu nzuri sana za kumkumbuka mjane wa Sarefathi.