Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitia-Moyo “Kutoka Katika Kinywa cha Watoto”

Kitia-Moyo “Kutoka Katika Kinywa cha Watoto”

Mnamo Desemba 2009, Mahakama Kuu ya Urusi iliunga mkono uamuzi uliofutilia mbali shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova huko Taganrog, Urusi, na kuwapokonya Jumba lao la Ufalme, na kisha kutangaza kwamba machapisho yetu 34 yana msimamo mkali wa kidini. Habari hiyo ya kushangaza iliwekwa kwenye Tovuti rasmi ya Mashahidi wa Yehova pamoja na picha za Mashahidi walioathiriwa na uamuzi huo, kutia ndani watoto wadogo.

Miezi michache baadaye, Kituo cha Usimamizi cha Mashahidi wa Yehova nchini Urusi kilipokea kifurushi na barua kutoka kwa familia ya Mashahidi huko Queensland, Australia. Familia hiyo ilikuwa imeona ripoti ya uamuzi wa Mahakama hiyo. Barua hiyo ilisema hivi: “Ndugu Wapendwa, watoto Wetu, Cody na Larissa, waliguswa hisia sana na imani na majaribu ya rafiki zetu nchini Urusi. Wameandika kadi na barua, na tumetengeneza kifurushi kidogo kilicho na zawadi ambazo tungependa kuzituma kwa watoto walio huko Taganrog, ili tu tuwajulishe kwamba kuna watoto wengine kutoka eneo la mbali sana ambao pia wanamtumikia Yehova kwa uaminifu na wanawafikiria. Wanawatumia wote kumbatio kubwa na upendo wao.”

Walipopokea zawadi hizo, watoto wa huko Taganrog waliandika barua za shukrani zenye michoro na kuzituma kwa ile familia iliyoko Australia. Akiwa ameguswa sana na maneno yenye kutia moyo “kutoka katika kinywa cha watoto,” Shahidi mmoja anayetumikia katika ofisi ya tawi ya Urusi aliwaandikia Cody na Larissa hivi: “Mnaweza kuwazia jinsi inavyoudhi watoto na watu wazima kuadhibiwa bila kufanya kosa lolote. Ndugu na dada zetu huko Taganrog hawakufanya kosa lolote, lakini Jumba lao la Ufalme limechukuliwa. Jambo hilo limewahuzunisha sana. Watatiwa moyo sana wakijua kwamba mtu fulani kutoka upande mwingine wa ulimwengu anawafikiria. Asanteni kwa fadhili na ukarimu wenu!”​—Zab. 8:2.

Kwa kweli sisi ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote, na upendo uliopo kati yetu unatusaidia sote kukabiliana na majaribu na magumu maishani. Mahakama zinapoendelea kujadiliana ikiwa machapisho ya Mashahidi wa Yehova huchochea chuki au la, watoto wetu wanaonyesha kimyakimya kwamba wanahangaikiana, wakishinda mipaka ya kitaifa na kijamii na kudhihirisha ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”​—Yoh. 13:35.