Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimepata Mambo Mengi Mazuri

Nimepata Mambo Mengi Mazuri

Nimepata Mambo Mengi Mazuri

Limesimuliwa na Arthur Bonno

ULIKUWA mwaka wa 1951. Mimi na mke wangu Edith, tulikuwa katika kusanyiko la wilaya tuliposikia tangazo kwamba kungekuwa na mkutano wa wale ambao wangependa kuingia katika utumishi wa umishonari.

Nilisema hivi kwa msisimko: “Twende tukasikilize!”

Edith akajibu hivi: “Art, huo si mkutano wetu!”

“Twende Edie, tutasikiliza tu.”

Baada ya mkutano huo, fomu za maombi ya Shule ya Gileadi zilitolewa.

Nikamhimiza hivi: “Acha tuzijaze.”

“Lakini Art, namna gani kuhusu familia zetu?”

Karibu mwaka mmoja na nusu baada ya kusanyiko hilo, tulihudhuria Shule ya Gileadi na tukapewa mgawo wa kutumika huko Ekuado, Amerika Kusini.

Kama unavyoweza kuona katika mazungumzo kati yangu na mke wangu katika kusanyiko hilo, nilikuwa mtu wa kusukuma mambo na nilikuwa na mtazamo wa kwamba tulikuwa na uwezo wa kufanya jambo lolote. Hata hivyo, Edith alikuwa mpole na mwenye kiasi. Alipokuwa akikua katika mji mdogo wa Elizabeth, huko Pennsylvania, Marekani, hakuwa amewahi kamwe kwenda mbali na nyumbani au kukutana na mtu ambaye si mwenyeji. Ilikuwa vigumu kwake kuacha familia yao. Hata hivyo, alikubali kwa moyo wote mgawo wa kutumika katika nchi ya kigeni. Tulifika Ekuado mwaka wa 1954 na tangu wakati huo tumekuwa tukitumika tukiwa wamishonari katika nchi hii. Katika miaka ambayo tumekuwa huku, tumepata mambo mengi mazuri. Je, ungependa kusikia baadhi ya mambo hayo?

Kumbukumbu Zenye Kufurahisha

Mgawo wetu wa kwanza ulikuwa kwenye jiji kuu, Quito, lililo mita 2,850 hivi juu kwenye Milima ya Andes. Tulitumia siku mbili kufika kwenye jiji hilo tukisafiri kwa gari-moshi na lori kutoka kwa jiji la pwani la Guayaquil—safari ambayo siku hizi inachukua dakika 30 kwa ndege! Tulitumikia huko Quito kwa miaka minne ambayo hatuwezi kusahau. Kisha, jambo lingine zuri likafanyika mwaka wa 1958: Tulipewa mgawo wa kufanya kazi ya mzunguko.

Wakati huo, kulikuwa na mizunguko miwili tu midogo katika nchi yote. Kwa hiyo, zaidi ya kutembelea makutaniko, tulitumia majuma mengi katika mwaka tukihubiri katika miji midogo ya Wahindi ambayo haikuwa na Mashahidi. Kwa kawaida wageni waliotembelea miji hiyo (pueblos) waliishi katika vyumba vidogo visivyo na madirisha vyenye kitanda kimoja bila kitu kingine chochote. Tulibeba sanduku la mbao ambalo lilikuwa na jiko linalotumia mafuta ya taa, lilikuwa pia na sufuria, sahani, beseni, mashuka, chandarua cha mbu, nguo, magazeti ya zamani, na vitu vingine. Tulitumia magazeti hayo kuziba mashimo kwenye ukuta ili iwe vigumu kwa panya kuingia.

Ingawa vyumba hivyo vilikuwa vichafu na vyenye giza, tunakumbuka vizuri mazungumzo tuliyokuwa nayo wakati wa usiku tukiwa tumeketi kwenye kitanda, tukila chakula chepesi tulichokuwa tumekipika kwa jiko letu la mafuta. Kwa sababu kiasili mimi ni mtu mwenye msisimko, mara nyingi nilizungumza kabla ya kufikiri, nyakati nyingine mke wangu angetumia pindi hizo zenye utulivu kunitajia njia za busara ambazo ningetumia ili kujieleza vizuri kwa ndugu tuliowatembelea. Nilimsikiliza na hivyo ziara zangu zikawa zenye kutia moyo zaidi. Pia, nilipozungumza vibaya kuhusu mtu fulani bila kufikiri, mke wangu alikataa kushiriki katika mazungumzo hayo. Hivyo, nilijifunza kuwa na mtazamo unaofaa kuwaelekea ndugu zangu. Ingawa hivyo, mara nyingi mazungumzo yetu wakati wa usiku yalihusu mambo ambayo tulikuwa tumejifunza katika gazeti la Mnara wa Mlinzi na mambo ambayo tulikuwa tumejionea katika utumishi wa shambani siku hiyo. Kwa kweli, tulijionea mambo yenye kusisimua kama nini!

Jinsi Tulivyompata Carlos

Katika mji wa Jipijapa, magharibi mwa Ekuado, tulipewa jina la mtu anayependezwa—jina peke yake, Carlos Mejía, lakini hatukuambiwa mahali anapoishi. Tulipoondoka kwenye chumba chetu cha kukodi asubuhi hiyo, hatukujua tungeanzia wapi kumtafuta, kwa hiyo tulianza tu kutembea. Tulilazimika kuruka mashimo mengi yenye matope kwenye barabara za udongo kwa sababu ya mvua kubwa iliyokuwa imenyesha usiku uliotangulia. Nilikuwa nikitembea mbele ya mke wangu wakati niliposikia kwa ghafula mtu akilia nyuma yangu kwa sauti na kuniomba msaada, “Art!” Niligeuka na kumwona Edie akiwa ametumbukia ndani ya matope meusi yaliyofika kwenye magoti yake. Jambo hilo lilikuwa la kuchekesha sana hivi kwamba ningecheka lakini sikucheka kwa sababu machozi yalikuwa yakimlenga-lenga.

Nilifanikiwa kumvuta Edie kutoka ndani ya shimo hilo, lakini viatu vyake vilibaki ndani ya matope hayo. Kando yetu kulikuwa na mvulana na msichana ambao walikuwa wakitutazama, hivyo nikawaambia: “Nitawapa pesa ikiwa mtatoa viatu vilivyo ndani ya matope.” Papo hapo wakavitoa viatu hivyo, lakini Edie alihitaji mahali pa kusafisha miguu yake. Mama ya watoto hao alikuwa akitazama kilichokuwa kikiendelea na akatukaribisha ndani ya nyumba yake, ambako alimsaidia mke wangu kusafisha miguu yake huku watoto wakisafisha vile viatu vichafu. Kabla hatujaondoka, jambo zuri lilitokea. Nilimuuliza mwanamke huyo ikiwa alijua mahali ambapo tungempata mwanamume anayeitwa Carlos Mejía. Alisema hivi kwa mshangao: “Yeye ni mume wangu.” Baada ya muda tulianzisha funzo la Biblia, na mwishowe washiriki wote wa familia hiyo wakabatizwa. Miaka mingi baadaye, Carlos, mke wake, na wawili kati ya watoto wao wakawa mapainia wa pekee.

Safari Ngumu—Ukarimu Wenye Kugusa Moyo

Tulipambana na hali ngumu katika kazi ya kusafiri. Tulisafiri kwa mabasi, magari-moshi, malori, mitumbwi au boti, na ndege ndogo. Wakati mmoja tulienda kuhubiri kwenye vijiji vya wavuvi vilivyo karibu na mpaka wa Kolombia pamoja na John McLenachan, aliyekuwa mwangalizi wa wilaya, na mke wake, Dorothy. Tulisafiri kwa mtumbwi wenye injini. Samaki wanaoitwa papa waliokuwa wakubwa kama mtumbwi wetu walikuwa wakiogelea kando yetu! Hata mwendeshaji-mtumbwi hodari tuliyekuwa naye alishtuka alipoona ukubwa wa papa hao na akaelekeza haraka mtumbwi karibu na ufuo.

Hata hivyo, tulipata matokeo mazuri sana hata ingawa tulikabili magumu katika kazi ya mzunguko. Tuliwafahamu ndugu wazuri sana, wenye ukarimu. Mara nyingi familia ambazo tuliishi nazo zilisisitiza kwamba tule chakula mara tatu kwa siku huku wao wakila mlo mmoja tu. Au walitukaribisha tulale kwenye kitanda kimoja tu katika nyumba yao, huku wao wakilala kwenye sakafu. Mara nyingi mke wangu aliniambia, “Ndugu na dada hawa wapendwa wananisaidia kuona kwamba kwa kweli tunahitaji vitu vichache maishani.”

“Hatutakataa”

Mwaka wa 1960, jambo lingine zuri lilifanyika, tulialikwa kutumika kwenye ofisi ya tawi huko Guayaquil. Nilifanya kazi ya usimamizi kwenye ofisi, huku Edith akihubiri pamoja na kutaniko lililokuwa karibu na ofisi ya tawi. Sikufikiri kamwe kwamba ninaweza kufanya kazi ofisini na nilihisi sistahili, lakini andiko la Waebrania 13:21 linasema kwamba Mungu anatupatia “vifaa vyema vya kila namna ili kufanya mapenzi yake.” Miaka miwili baadaye, nilialikwa kuhudhuria mazoezi ya miezi kumi ya Gileadi ambayo yangefanywa katika Betheli ya Brooklyn, New York. Wakati huo, wake walitazamiwa kubaki katika migawo yao. Mke wangu alipokea barua kutoka Brooklyn. Aliombwa afikirie kwa makini ikiwa angekubali kuishi bila mume wake kwa miezi kumi.

Edith alijibu hivi barua hiyo: “Nina hakika kwamba hili halitakuwa jambo rahisi hata kidogo, lakini tunajua kwamba bila shaka Yehova atatusaidia kushinda hali yoyote ngumu ambayo inaweza kutokea. . . . Hatutakataa mapendeleo yoyote ambayo tutapewa au nafasi yoyote ambayo itatuwezesha kustahili zaidi kutimiza madaraka yetu.” Nilipokuwa Brooklyn, nilipokea barua kutoka kwa mke wangu kila juma.

Kutumika Pamoja na Waamini Wenzetu Waaminifu

Mwaka wa 1966, kwa sababu ya matatizo ya kiafya, mimi na Edith tulirudi Quito, ambako tulianza tena utumishi wetu wa umishonari na kuhubiri pamoja na ndugu na dada wenyeji. Waliweka mfano mzuri kama nini katika kushika utimilifu!

Dada mmoja mwaminifu alikuwa na mume ambaye hakuwa mwamini na ambaye alimpiga mara nyingi. Siku moja saa kumi na mbili asubuhi, tulipigiwa simu na kuambiwa kwamba alikuwa amepigwa tena. Nilienda haraka kwenye nyumba ya dada huyo. Nilipomwona, sikuamini macho yangu. Alikuwa amelala kitandani, akiwa amevimba na akiwa ameumizwa mwili wote. Mume wake alikuwa amempiga kwa mti wa ufagio mpaka ukavunjika mara mbili. Baadaye siku hiyo, nilimpata mume huyo nyumbani na nikamwambia kwamba alikuwa ametenda jambo la kipumbavu. Aliomba msamaha kwelikweli.

Mwanzoni mwa miaka ya 1970, hali yangu ya afya ilikuwa nzuri zaidi na tukarudia kazi ya mzunguko. Mji wa Ibarra ulikuwa katika mzunguko wetu. Tulipotembelea mji huo mwishoni mwa miaka ya 1950 kulikuwa na Mashahidi wawili tu, yaani, mmishonari mmoja na ndugu mmoja mwenyeji. Kwa hiyo, tulitamani sana kukutana na watu wengi wapya ambao walikuwa wamejiunga na kutaniko hilo.

Katika mkutano wetu wa kwanza huko, Ndugu Rodrigo Vaca alisimama jukwaani na akaongoza sehemu ambayo ilihusisha mazungumzo pamoja na wasikilizaji. Kila alipouliza swali, wasikilizaji walisema kwa sauti “Yo, yo!” (“Mimi, mimi!”) badala ya kuinua mikono yao. Mimi na Edith tuliangaliana kwa mshangao. Nilijiuliza, ‘Ni nini kinachoendelea hapa?’ Baadaye tuliambiwa kwamba Ndugu Vaca ni kipofu lakini anatambua sauti za washiriki wa kutaniko wanaposema kwa sauti. Yeye ni mchungaji ambaye kwa kweli anawajua kondoo wake! Hilo lilitukumbusha maelezo ya Yesu katika andiko la Yohana 10:3, 4, 14 kuhusu jinsi Mchungaji Mwema anavyowajua vizuri sana kondoo na jinsi wanavyomjua. Leo, mji wa Ibarra una makutaniko sita yanayozungumza Kihispania, kutaniko moja la lugha ya Quichua, na kutaniko moja la lugha ya ishara. Ndugu Vaca anaendelea kutumika kwa uaminifu akiwa mzee na painia wa pekee. *

Tunashukuru kwa Ajili ya Wema wa Yehova

Mwaka wa 1974 Yehova alituonyesha wema tena tulipoalikwa kurudi Betheli, ambako nilipewa tena kazi ya usimamizi na baadaye nikawekwa rasmi kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi. Mwanzoni Edith alifanya kazi jikoni, na baadaye akaanza kufanya kazi katika ofisi, ambako anaendelea kutumika leo akiwa karani wa kushughulikia barua.

Kwa miaka mingi, tumepata shangwe ya kuwakaribisha mamia ya wamishonari waliozoezwa Gileadi, ambao wanasaidia ndugu na dada katika makutaniko wawe wakomavu na wenye bidii. Tunatiwa moyo pia na maelfu ya ndugu na dada ambao wamekuja kutoka nchi zaidi ya 30 ili kutumika nchini. Tunachochewa kama nini na roho yao ya kujidhabihu! Wengine wao waliuza nyumba na biashara ili waje huku kutumika mahali ambapo pana uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Walinunua magari ili kuhubiri katika maeneo yaliyo mbali, wakaanzisha makutaniko mapya, na wakasaidia kujenga Majumba ya Ufalme. Dada wengi waseja wametoka nchi za kwao ili wafanye upainia huku, na ni wafanyakazi wenye bidii na uwezo kama nini!

Kwa kweli, nimepata mambo mengi mazuri katika miaka ambayo nimemtumikia Mungu. Jambo la kwanza kabisa kati ya hayo ni uhusiano wangu pamoja na Yehova. Pia, ninashukuru kwamba Yehova alinipa “msaidizi.” (Mwa. 2:18) Ninapokumbuka miaka zaidi ya 69 ambayo tumekuwa pamoja tukiwa mume na mke, ninafikiria andiko la Methali 18:22, ambalo linasema: “Je, mtu amepata mke mwema? Amepata kitu chema.” Nimefurahia sana kuwa pamoja na Edith. Amenisaidia kwa njia nyingi sana. Alithibitika pia kuwa binti mzuri kwa mama yake. Tangu tulipofika Ekuado, mke wangu alimtumia mama yake barua kila juma mpaka 1990, mama yake alipokufa akiwa na umri wa miaka 97.

Sasa nina umri wa miaka 90 na Edith ana umri wa miaka 89. Tunathamini shangwe ambayo tumepata kwa kuwasaidia watu 70 kumjua Yehova. Bila shaka, tunafurahi kwamba tulijaza zile fomu za Shule ya Gileadi zaidi ya miaka 60 iliyopita. Tumefurahia mambo mengi mazuri katika maisha kwa sababu ya uamuzi huo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 29 Simulizi la maisha ya Ndugu Vaca linapatikana katika gazeti Amkeni! la Januari 8, 1985 (8/1/1985).

[Picha katika ukurasa wa 29]

Tukiwa Yankee Stadium, huko New York pamoja na wamishonari ambao tulihudhuria darasa moja, 1958

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kutembelea familia ya Mashahidi tulipokuwa tunafanya kazi ya mzunguko, 1959

[Picha katika ukurasa wa 32]

Tukiwa katika ofisi ya tawi ya Ekuado, 2002