Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Una Kusudi Gani Maishani?

Una Kusudi Gani Maishani?

Una Kusudi Gani Maishani?

KENNY alikuwa mfanyakazi wa kampuni moja kubwa ya kuuza vitu. Alikuwa na gari la kifahari na nyumba ya ghorofa katika eneo la matajiri katika jiji fulani kubwa. Akiwa na uzoefu wa kuruka angani kwa mwavuli, alifurahia sana msisimuko wa kuruka angani kwa mwavuli umbali wa maelfu ya kilomita juu ya ardhi. Je, aliishi maisha yenye kuridhisha? Kulingana na gazeti moja (The Wall Street Journal) Kenny alisema hivi: “Sasa nina umri wa miaka 45, sina tumaini lolote la wakati ujao . . . Maisha yangu hayana kusudi lolote.”

Elyn alifanya mazoezi kwa bidii ili awe hodari katika mchezo wa kuteleza kwenye barafu. Mwishowe, alikuja kuwa mchezaji hodari. Elyn alipata umaarufu aliotaka. Hata hivyo, alilalamika hivi: “Furaha yote ambayo niliahidiwa iko wapi? Nilijisikia mpweke sana. Mwishowe nitazeeka, na ingawa nilikuwa na usalama wa kifedha, maisha yatakuwa ya ubatili ikiwa kusudi la maisha ni hilo tu.”

Hideo aliyejulikana kuwa mchoraji stadi, alitumia maisha yake kufanya kazi hiyo. Hakuuza picha zake za sanaa; alifikiri kwamba kufanya hivyo kungepunguza sifa yake akiwa mchoraji. Mwishoni mwa maisha yake ya miaka 98, alipeleka picha zake nyingi kwenye jumba moja la makumbusho kama mchango. Alitumia maisha yake kufuatia sanaa. Lakini, hakutosheka, kwa kuwa aliona kwamba hangeweza kamwe kuwa msanii bora kabisa.

Watu fulani wanajitolea sana kuwasaidia wengine. Kwa mfano, mfikirie msimamizi mmoja wa sinema huko Hollywood. Akiwa mkurugenzi-msaidizi katika moja ya makampuni makubwa zaidi ya sinema nchini Marekani, alishirikiana na watu mashuhuri na aliishi katika eneo la kifahari. Alipoenda kupumzika nchini Kambodia, msichana fulani alimfikia alipokuwa akila katika mkahawa mmoja huko Phnom Penh na kumwomba pesa. Alimpa dola moja na soda. Msichana huyo alifurahi. Hata hivyo, alirudi tena usiku uliofuata na kuendelea kuomba pesa. Mkurugenzi huyo aliona kwamba msichana huyo hakuhitaji tu msaada wa aina hiyo.

Mwaka mmoja baadaye, mkurugenzi huyo aliamua kubadili kazi yake. Aliacha kufanya kazi katika kampuni ya sinema na kuanza kuwasaidia maskini nchini Kambodia. Alianzisha shule ya kuwatunza, kuwalisha, na kuwaelimisha maskini. Hata hivyo, hisia zake zinabadilika-badilika, nyakati fulani anafurahi na kuridhika na yale anayotimiza na nyakati nyingine anavunjika moyo na kufadhaika kwa sababu ya matatizo yanayoongezeka ambayo analazimika kukabiliana nayo.

Watu wote wanne ambao wametajwa walifikiri kwamba walijua walichotaka kutimiza maishani. Hata hivyo, mwishowe hawakuridhika walipotimiza miradi ambayo walikuwa wamejitahidi sana kutimiza. Una kusudi gani maishani? Unatanguliza nini katika maisha yako? Je, una hakika kwamba baadaye hutajuta kwa sababu ya jinsi unavyotumia maisha yako?