Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, ni jambo linalofaa kwa Shahidi wa Yehova kuhudhuria arusi ya mtu wa ukoo au rafiki ambaye si Shahidi?

Arusi ni pindi zenye shangwe, na inaeleweka kwamba Mkristo angependa kushiriki shangwe hiyo. Bila shaka, vijana ambao wanaalikwa kuhudhuria pindi hizo wanapaswa kuwatii wazazi wao au walezi wao, ambao wana haki ya kutoa uamuzi wa mwisho. (Waefeso 6:1-3) Lakini namna gani ikiwa mwanamume ambaye si Shahidi wa Yehova anamwomba mke wake ambaye ni Shahidi aende pamoja naye kuhudhuria arusi kanisani? Huenda dhamiri ya mke huyo ikamruhusu kwenda ili kuwa tu mtazamaji anayeazimia kutoshiriki matendo yoyote yale ya kidini yanayohusiana na pindi hiyo.

Hivyo basi, kuhudhuria au kutohudhuria arusi fulani ni uamuzi wa mtu binafsi. Hata hivyo, kila Mkristo anapaswa kujua kwamba atatoa hesabu kwa Yehova, na ni lazima afikirie kanuni mbalimbali za Kimaandiko anapofanya uamuzi kuhusu kuhudhuria arusi ya mtu ambaye si Shahidi.

Jambo la maana zaidi ambalo Mkristo anapaswa kufikiria ni tamaa yake ya kupata kibali cha Mungu. Yesu alisema hivi: “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika shughuli mbalimbali za dini nyingine, kama vile sala, desturi za ibada, au sherehe ambazo hazipatani na kweli ya Biblia. —2 Wakorintho 6:14-17.

Pia, Mkristo anatambua kwamba uamuzi wake unaweza kuwa na matokeo mazuri au mabaya juu wengine. Ukiamua kuhudhuria, je, watu wako wa ukoo wataudhika usiposhiriki kikamili katika sherehe za arusi? Tunahitaji pia kufikiria uvutano ambao uamuzi wetu utakuwa nao juu ya waamini wenzetu. (Waroma 14:13) Hata ikiwa wewe au watu wa familia yako mnakata kauli kwamba si kosa kuhudhuria arusi ya mtu ambaye si Shahidi, je, uamuzi huo utakuwa na matokeo mabaya juu ya ndugu na dada zako wa kiroho? Je, kufanya hivyo kunaweza kuumiza dhamiri ya wengine?

Sherehe za arusi zinazohusisha watu wa ukoo ambao si Mashahidi zinaweza kutokeza hali zenye kutatanisha. Namna gani ikiwa wanakuomba ushiriki katika msafara wa arusi? Au namna gani ikiwa mwenzi wako si Shahidi na anataka kushiriki kikamili katika shughuli zote za arusi? Ikiwa arusi hiyo itakuwa ndoa ya kiserikali itakayofungishwa na hakimu au ofisa wa serikali, huenda kuhudhuria arusi hiyo hakutahusisha mambo mengi zaidi ya kushuhudia utaratibu wa kisheria.

Hata hivyo, arusi zinazofanywa katika jengo la kidini au zinazoendeshwa na kasisi zinatokeza maswali mengi zaidi. Ili kutii dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia na kuepuka kutenda kinyume na imani yako ya kidini au kufanya jambo ambalo linaweza kuwaudhi wengine kwenye arusi, huenda ukaamua kutohudhuria arusi hiyo. (Methali 22:3) Unaweza kuepuka kufadhaika sana na pia kuizuia familia yako isifadhaike sana kwa kuwaeleza mapema imani yako inayotegemea Biblia, kwa kuwaonyesha ni kwa kadiri gani uko tayari kushirikiana nao au labda kwa kupendekeza njia nyingine.

Baada ya kuchanganua mambo yote kwa uangalifu, huenda Wakristo fulani wakaamua kwamba si kosa kuhudhuria arusi ya mtu ambaye si Shahidi na kuwa tu mtazamaji asiyeshiriki. Lakini ikiwa Mkristo anaona kwamba kwa kuhudhuria huenda akashawishika kutenda kinyume na kanuni za kimungu, anaweza kukata kauli kwamba ingefaa zaidi asihudhurie arusi hiyo. Akiamua kutohudhuria arusi yenyewe, lakini kwa sababu amealikwa, aamue kwenda kwenye karamu zitakazofanywa baadaye, anapaswa kuazimia ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’ (1 Wakorintho 10:31) Kwa kufanya maamuzi kama hayo, “kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe” wa daraka. (Wagalatia 6:5) Kwa hiyo, hata uamuzi wako uwe nini, kumbuka kwamba ni jambo la maana sana kuwa na dhamiri njema mbele za Yehova Mungu.