Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia ya Kwanza Katika Kireno Hadithi ya Uvumilivu

Biblia ya Kwanza Katika Kireno Hadithi ya Uvumilivu

Biblia ya Kwanza Katika Kireno Hadithi ya Uvumilivu

“ANAYEVUMILIA ndiye atakayefanikiwa.” Maneno hayo yanaonekana kwenye ukurasa wa kwanza wa kijitabu cha kidini kilichoandikwa na João Ferreira de Almeida katika karne ya 17. Ni vigumu kueleza kwa njia inayofaa kuhusu mwanamume ambaye alijitoa kwa ajili ya kazi ya kutafsiri na kuchapisha Biblia katika Kireno.

Almeida alizaliwa mwaka wa 1628 huko Torre de Tavares, katika kijiji kimoja kilicho kaskazini mwa Ureno. Akiwa yatima, Almeida alikulia Lisbon, mji mkuu wa Ureno, ambako alilelewa na baba yake mdogo aliyekuwa kasisi. Kama inavyoaminiwa, alipokuwa akisomea ukasisi, Almeida alipata elimu bora, ambayo ilimsaidia kusitawisha uwezo wa ajabu wa kujua lugha nyingi akiwa na umri mdogo.

Hata hivyo, haielekei kwamba Almeida angetumia ustadi wake katika kazi ya kutafsiri Biblia ikiwa angebaki Ureno. Wakati Marekebisho Makubwa yalipokuwa yakienea kaskazini na katikati mwa Ulaya, na tafsiri za Biblia katika lugha za kienyeji kusambazwa, nchi ya Ureno ilibaki kabisa chini ya uvutano wa Baraza la Kuhukumu Wazushi la Katoliki. Kupatikana tu ukiwa na tafsiri ya Biblia ya lugha ya kienyeji kungefanya upelekwe mbele ya Baraza hilo. *

Ili kuepuka hali ya ukatili iliyokuwepo, Almeida alihamia Uholanzi alipokuwa na umri wa miaka 14. Muda mfupi baadaye, akiwa na umri huo, alisafiri kwenda Asia, kupitia Batavia (leo ni Jakarta), Indonesia. Wakati huo, Batavia kilikuwa kituo cha kuendesha shughuli za serikali ya Ureno ya Shirika la Uholanzi la India Mashariki katika Kusini-Mashariki mwa Asia.

Mtafsiri Kijana

Katika sehemu ya mwisho ya safari yake ya kwenda Asia, Almeida alipata kitu kilichobadili maisha yake. Alipokuwa akisafiri kwa meli kati ya Batavia na Malacca (leo ni Melaka), magharibi mwa Malaysia, alipata kijitabu cha Kiprotestanti cha Kihispania chenye kichwa Tofauti Katika Dini Zinazodai Kuwa za Kikristo (Diferencias de la Cristiandad). Zaidi ya kushambulia mafundisho ya dini za uwongo, kijitabu hicho kilikuwa na taarifa hii ambayo ilimvutia hasa kijana Almeida: “Kutumia lugha isiyoeleweka kanisani, hata ingawa ni kwa utukufu wa Mungu, hakumfaidi msikilizaji ambaye haelewi lugha hiyo.”—1 Wakorintho 14:9.

Kauli ya Almeida ilikuwa wazi: Suluhisho la kuweka wazi makosa ya dini ni kufanya Biblia ieleweke kwa watu wote. Alipofika Malacca alijiunga na dini ya Dutch Reformed, na papo hapo akaanza kutafsiri sehemu za Injili za Kihispania katika Kireno, akizisambaza kwa “wale waliotamani kwa unyoofu kujua kweli.” *

Miaka miwili baadaye, Almeida alikuwa tayari kwa ajili ya kazi kubwa zaidi, yaani, kutafsiri Maandiko yote ya Kigiriki ya Kikristo kutokana na Vulgate ya Kilatini. Kijana huyo mwenye umri wa miaka 16, alimaliza kazi hiyo kubwa kabla ya mwaka mmoja kwisha! Kwa ujasiri, alituma nakala moja ya tafsiri yake kwa gavana mkuu wa Uholanzi huko Batavia ili ichapishwe. Inaelekea, Kanisa la Reformed la Batavia lilituma maandishi ya Almeida huko Amsterdam, lakini mhudumu mzee ambaye alikabidhiwa maandishi hayo alikufa, na hivyo kazi ya Almeida ikapotea.

Alipoombwa atoe nakala ya tafsiri yake kwa ajili ya Kanisa la Reformed huko Ceylon (leo ni Sri Lanka) mwaka wa 1651, Almeida aligundua kwamba tafsiri ya kwanza iliyokuwa ndani ya hifadhi ya maandishi ya kanisa ilikuwa imetoweka. Bila kuvunjika moyo, alipata nakala moja, labda nakala ya awali, na mwaka uliofuata alikamilisha tafsiri iliyorekebishwa ya vitabu vya Injili na kitabu cha Matendo ya Mitume. Baraza la kanisa * huko Batavia lilimpa zawadi ya gilda 30 (pesa za Uholanzi). Hicho “kilikuwa kiasi kidogo sana cha pesa kikilinganishwa na kazi kubwa aliyofanya,” aliandika mmoja wa marafiki wa Almeida.

Ingawa hakutambuliwa, Almeida aliendelea na kazi yake, na mnamo 1654 akatoa tafsiri yake kamili ya Agano Jipya iliyofanyiwa marekebisho. Kwa mara nyingine tena, kuchapishwa kwa tafsiri hiyo kulifikiriwa, lakini hakuna jambo lolote la maana lililofanywa isipokuwa kutayarisha nakala chache zilizoandikwa kwa mkono za kutumiwa katika makanisa fulani.

Anahukumiwa na Baraza la Kuhukumu Wazushi

Katika miaka kumi iliyofuata, Almeida alijishughulisha sana na kazi ya uchungaji na ya umishonari kwa ajili ya Kanisa la Reformed. Aliwekwa rasmi kuwa mhudumu mwaka wa 1656, naye akatumika kwanza huko Ceylon, ambako aliponea chupuchupu kukanyagwa na tembo, na baadaye akatumika huko India, akiwa mmoja kati ya wamishonari wa kwanza wa Kiprostestanti kutembelea nchi hiyo.

Almeida alikuwa Mprotestanti aliyetumikia nchi ya kigeni. Kwa hiyo, watu wengi wanaozungumza Kireno ambao alitembelea walimwona kuwa mwasi-imani na msaliti. Alizozana mara kwa mara na wamishonari Wakatoliki kwa kuwa alishutumu moja kwa moja upotovu wa maadili miongoni mwa makasisi, na pia alifunua waziwazi mafundisho ya uwongo ya kanisa. Mizozo hiyo ilifikia kilele mwaka wa 1661 wakati Baraza la Kuhukumu Wazushi huko Goa, India, lilipomhukumia kifo Almeida kwa sababu ya uzushi wa kidini. Sanamu yake ilichomwa bila yeye kuwepo. Huenda gavana mkuu wa Uholanzi alimwita Almeida huko Batavia muda mfupi baadaye kwa sababu ya kuhofia jinsi Almeida alivyokuwa akishambulia kwa hoja nzito.

Almeida alikuwa mmishonari mwenye bidii, lakini hakusahau kamwe uhitaji wa Biblia ya Kireno. Kwa kweli, ilikuwa wazi kwamba makasisi na watu wa kawaida hawakuifahamu Biblia, na jambo hilo lilitia tu nguvu azimio lake. Katika utangulizi wa trakti moja ya kidini ya mwaka wa 1668, Almeida aliwajulisha hivi wasomaji wake: “Ninatumaini . . . hivi karibuni kwamba nitawapa Biblia nzima katika lugha yenu wenyewe, zawadi kubwa zaidi na hazina yenye thamani zaidi ambayo hakuna yeyote amewahi kuwapa.”

Almeida na Halmashauri ya Marekebisho ya Tafsiri

Mwaka wa 1676, Almeida alipeleka nakala yake ya mwisho ya Agano Jipya kwa baraza la kanisa huko Batavia ili ifanyiwe marekebisho. Tangu mwanzo, uhusiano kati ya mtafsiri huyo na wasahihishaji haukuwa mzuri. Mwandishi wa masimulizi ya maisha J. L. Swellengrebel anasema kwamba huenda watu waliofanya kazi pamoja na Almeida ambao walizungumza Kiholanzi walikuwa na matatizo ya kuelewa maana ya maneno fulani na jinsi yalivyoandikwa. Kulikuwa pia na ubishi kuhusu lugha ambayo alitumia. Je, ilifaa Biblia itumie Kireno cha watu wa kawaida au Kireno cha kitaalamu zaidi ambacho watu wengi hawangeelewa kwa urahisi? Mwishowe, bidii ya Almeida ya kukamilisha kazi hiyo ilisababisha mizozo kila mara.

Kazi ilisonga polepole, labda kwa sababu ya kutoelewana au kutopendezwa kwa wasahihishaji. Miaka minne baadaye, wasahihishaji walikuwa bado wanazozana kuhusu sura za kwanza za kitabu cha Luka. Akiwa amekata tamaa kwa sababu ya kukawia-kawia huko, Almeida alituma nakala moja ya maandishi yake Uholanzi ili ichapishwe bila wasahihishaji kujua.

Ingawa halmashauri ya kanisa ilijaribu kuzuia uchapishaji huo, tafsiri yake ya Agano Jipya ilichapishwa huko Amsterdam mwaka wa 1681, na nakala za kwanza zilifika Batavia mwaka uliofuata. Wazia jinsi Almeida alivyokata tamaa alipotambua kwamba tafsiri yake ilibadilishwa na wasahihishaji huko Uholanzi! Kwa kuwa wasahihishaji hawakujua Kireno, Almeida aligundua kwamba waliingiza “tafsiri zenye kupingana na zenye makosa ambazo zilificha maana ya Roho Takatifu.”

Wakuu wa serikali ya Uholanzi pia hawakufurahi, na hivyo wakaamuru kwamba nakala zote hizo zilizochapishwa ziharibiwe. Hata hivyo, Almeida aliwaomba wenye mamlaka wahifadhi nakala chache ili makosa mazito yasahihishwe kwa mkono. Nakala hizo zingetumiwa hadi wakati ambapo chapa iliyorekebishwa ingetayarishwa.

Wasahihishaji huko Batavia walikutana ili kuendelea na kazi yao ya kukagua Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na wakaanza kutayarisha vitabu vya Maandiko ya Kiebrania Almeida alipokuwa akivikamilisha. Ikihofia kwamba mtafsiri huyo atakasirika, halmashauri ya kanisa iliamua kuhifadhi mahali salama kanisani kurasa zilizotiwa sahihi za nakala ya mwisho. Almeida alipinga uamuzi wao.

Kufikia wakati huo, afya yake ilidhoofika kwa sababu ya miaka mingi ya kazi ngumu na ugumu wa maisha katika eneo lenye joto. Mwaka wa 1689, kwa sababu ya kuzorota kwa afya yake, Almeida aliachana na kazi za kanisa ili ajitoe kabisa kutafsiri Maandiko ya Kiebrania. Kwa kusikitisha, alikufa mwaka wa 1691 alipokuwa akitafsiri sura ya mwisho ya kitabu cha Ezekieli.

Chapa ya pili ya Agano Jipya iliyokamilishwa muda mfupi kabla ya kifo chake, ilichapishwa mwaka wa 1693. Kwa mara nyingine tena, inaelekea kwamba kazi yake iliharibiwa na wasahihishaji wasio na ujuzi. Katika kitabu chake kinachoitwa Biblia Huko Ureno (A Biblia em Portugal), G. L. Santos Ferreira anasema hivi: “Wasahihishaji . . . walifanya mabadiliko makubwa katika kazi bora ya Almeida, waligeuza-geuza na kuharibu umaridadi wote wa nakala ya awali ambao haukuharibiwa na wasahihishaji wa chapa ya kwanza.”

Biblia ya Kireno Yakamilishwa

Almeida alipokufa, bidii ya kurekebisha na kuchapisha Biblia ya Kireno huko Batavia ilitoweka. Shirika la London la Kueneza Ujuzi wa Kikristo ndilo lililogharimia toleo la tatu la Almeida la Agano Jipya mwaka wa 1711 kufuatia ombi la wamishonari kutoka Denmark waliokuwa wakifanya kazi huko Tranquebar, kusini mwa India.

Shirika hilo liliamua kujenga kiwanda cha uchapishaji huko Tranquebar. Hata hivyo, meli iliyobeba vifaa vya kuchapisha na shehena ya Biblia za Kireno ilitekwa nyara na maharamia Wafaransa ikiwa njiani kuelekea India, na wakaiacha katika bandari ya Rio de Janeiro, Brazili. Santos Ferreira anaandika hivi: “Kwa sababu fulani zisizoeleweka na katika hali ambazo wengi waliziona kuwa kama muujiza, masanduku ambayo yalikuwa na vifaa vya kuchapisha yalipatikana yakiwa salama kabisa ndani ya chumba cha chini cha mizigo na hivyo yakaendelea na safari yake katika meli hiyohiyo kuelekea Tranquebar.” Wamishonari kutoka Denmark walirekebisha kwa makini na kuchapisha tafsiri ya Almeida ya vitabu vya Biblia vilivyobaki. Buku la mwisho la Biblia ya Kireno lilichapishwa mwaka wa 1751, karibu miaka 110 baada ya Almeida kuanza kazi yake akiwa mtafsiri wa Biblia.

Urithi Unaodumu

Tangu alipokuwa kijana, Almeida alielewa uhitaji wa Biblia ya Kireno ili watu wa kawaida wafahamu kweli katika lugha yao wenyewe. Aliazimia kufuatia mradi huo katika maisha yake yote, ingawa kulikuwa na upinzani wa Kanisa Katoliki, ubaridi wa wenzake, matatizo ya kurekebisha tafsiri ambayo yalionekana kuwa yasiyo na mwisho, na kuzorota kwa afya yake. Uvumilivu wake ulithawabishwa.

Wazungumzaji wengi wa Kireno ambao Almeida alihubiria walikufa, lakini Biblia yake bado ipo. Katika karne ya 19, Chama cha Biblia cha Uingereza na Nchi za Kigeni na Chama cha Biblia cha American zilisambaza maelfu ya nakala za tafsiri ya Almeida huko Ureno na katika majiji ya pwani ya Brazili. Kwa sababu hiyo, Biblia zinazotegemea maandishi ya awali ya Almeida ni kati ya Biblia zinazopendwa sana leo na zenye kusambazwa zaidi katika nchi zinazozungumza Kireno.

Bila shaka, watu wengi wanapaswa kuwashukuru watafsiri wa mapema wa Biblia kama vile Almeida. Lakini tunapaswa kumshukuru hata zaidi Yehova, Mungu mwenye kuwasiliana, ambaye “mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Yeye ndiye amelihifadhi Neno lake na kulifanya lipatikane kwa faida yetu. Acheni basi sikuzote tuithamini sana na kujifunza kwa bidii ‘hazina hii yenye thamani zaidi’ kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Mwishoni mwa karne ya 16, Kanisa Katoliki lilikataza vikali matumizi ya Biblia za lugha za kienyeji ilipotoa Fahirisi ya Vitabu Vilivyokatazwa. Kulingana na kitabu kimoja (The New Encyclopædia Britannica), fahirisi hiyo “ilisimamisha kabisa kazi ya Wakatoliki ya kutafsiri kwa miaka 200 iliyofuata.”

^ fu. 8 Tafsiri za zamani za Biblia ya Almeida zinamwita Padri (Baba) Almeida, hiyo ndiyo sababu inayowafanya watu fulani waamini kwamba Almeida alikuwa kasisi Mkatoliki. Hata hivyo, wahariri Waholanzi wa Biblia ya Almeida walitumia neno hilo kimakosa, wakiwazia kuwa hicho ndicho cheo kilichotumiwa na kasisi au mhudumu.

^ fu. 10 Halmashauri inayosimamia Kanisa la Reformed.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

JINA LA MUNGU

Mfano mzuri wa utimilifu wa Almeida akiwa mtafsiri ni jinsi anavyotumia jina la Mungu ili kutafsiri Tetragramatoni ya Kiebrania.

[Picha zimeaandaliwa na]

Cortesia da Biblioteca da Igreja de Santa Catarina (Igreja dos Paulistas)

[Ramani katika ukurasa wa 18]

 

BAHARI YA ATLANTIKI

URENO

Lisbon

Torre de Tavares

[Picha katika ukurasa wa 18]

Batavia katika karne ya 17

[Hisani]

From Oud en Nieuw Oost-Indiën, Franciscus Valentijn, 1724

[Picha katika ukurasa wa 18, 19]

Ukurasa wa kwanza wa tafsiri ya kwanza ya Kireno ya Agano Jipya, iliyochapishwa mwaka wa 1681

[Hisani]

Courtesy Biblioteca Nacional, Portugal