Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Elimu ya Biblia Inajenga Imani

Elimu ya Biblia Inajenga Imani

Elimu ya Biblia Inajenga Imani

“LIMEKUWA pendeleo kubwa kama nini kutumia miezi mitano ambayo imepita kuchunguza mawazo ya Muumba wetu na kujifunza kuona mambo jinsi anavyoyaona!” akasema mwakilishi mmoja wa darasa la 122 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) katika siku ya kuhitimu. Machi 10, 2007 (10/3/2007), ni siku ambayo wanafunzi 56 wa darasa hilo watakumbuka kwa muda mrefu sana. Wanafunzi hao walikuwa tayari kuanza migawo yao ya utumishi wa umishonari katika nchi 26.

Baada ya kuwakaribisha kwa uchangamfu watu 6,205 waliohudhuria, Theodore Jaracz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alisema hivi: “Tuna hakika kwamba ninyi mtaimarishwa kiroho na kujengwa katika imani kwa sababu ya kuhudhuria programu hii ya kuhitimu.” Aliwataja wasemaji wanne ambao wangewapa wanafunzi mashauri na himizo la wakati unaofaa kutoka katika Biblia ili kuwasaidia wafanikiwe katika migawo yao ya umishonari.

Kuwatia Moyo Wanafunzi Wawasaidie Wengine Kujenga Imani

Leon Weaver, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani, alitoa hotuba yenye kichwa, “Endelea Kufanya Yaliyo Mema.” Aliwakumbusha wanafunzi kwamba tayari kwa wastani kila mmoja wao ametumia miaka 13 katika utumishi wa wakati wote, akiendeleza elimu ya Biblia inayojenga imani. Alisema: “Hiyo ni kazi njema kwa sababu inahusisha kuokoa maisha ya watu, na la maana zaidi, hiyo ni kazi njema kwa sababu inamtukuza Baba yetu wa mbinguni, Yehova.” Kisha Ndugu Weaver akawatia moyo wanafunzi waendelee ‘kupanda kwa roho’ na ‘wasife moyo katika kufanya yaliyo mema.’—Wagalatia 6:8, 9.

David Splane, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa vikumbusho vinavyofaa katika hotuba yake yenye kichwa “Hakikisheni Kwamba Mnaanza Vizuri.” Ndugu Splane aliwatia moyo wamishonari wapya waanze migawo yao mipya vizuri kwa kufanya mambo yafuatayo: “Kudumisha mtazamo unaofaa. Kutokata kauli haraka-haraka. Kutabasamu. Kutochambua. Kuwa wanyenyekevu, na kuwaheshimu ndugu wenyeji.” Kisha akaongezea: “Mnaposhuka kutoka kwenye ndege, anzeni vizuri, na Yehova abariki miguu yenu mizuri inapowaletea watu ‘habari njema za jambo bora.’—Isaya 52:7.

“Urithi Usiokuwa na Shaka Lolote” ndicho kilichokuwa kichwa cha hotuba ya mwalimu wa Shule ya Gileadi Lawrence Bowen. Ndugu Bowen aliwakumbusha wanafunzi kwamba Shule ya Gileadi ilianzishwa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu kwa sababu ya kuwa na uhakika kabisa kwamba Neno la Yehova la kinabii litatimia. (Waebrania 11:1; Ufunuo 17:8) Tangu hapo, Shule ya Gileadi imewawezesha wanafunzi kuimarisha imani yao. Imani yenye nguvu inawachochea wanafunzi kusonga mbele na kutangaza kweli kwa bidii.

Mark Noumair, mwalimu mwingine wa Shule ya Gileadi, alitoa hotuba yenye kusisimua iliyokuwa na kichwa, “Mnanikumbusha Mtu Fulani.” Alizungumzia mfano wa nabii Elisha, ambaye alionyesha imani na ujasiri katika mgawo wake. Akitumia 1 Wafalme 19:21, Ndugu Noumair alisema: “Elisha alikuwa tayari kufanya mabadiliko maishani, kuweka mapendezi yake ya kibinafsi mahali pa pili, na kutetea kusudi la Yehova.” Aliwapongeza wahitimu kwa kuonyesha roho kama hiyo na akawatia moyo waendelee kufanya hivyo katika migawo yao mipya.

Imani Inatokeza Uhuru wa Usemi

Wanafunzi hao waliotarajia kuwa wamishonari walipokuwa wakijenga imani yao shuleni, walitumia siku za mwisho wa juma kuwahubiria wengine habari njema. Kwa sababu hiyo walipata mambo yaliyoonwa ambayo yalisimuliwa ama kuigizwa wakati wa sehemu ya programu iliyoongozwa na Wallace Liverance, mwalimu mwingine wa Shule ya Gileadi. Kichwa cha sehemu hiyo kilikuwa, “Tunaonyesha Imani na kwa Hiyo Tunasema,” na ilikazia maneno ya mtume Paulo katika 2 Wakorintho 4:13.

Baada ya sehemu hiyo, Daniel Barnes na Charles Woody, washiriki wa familia ya Betheli, waliwahoji ndugu fulani wamishonari na wengine waliowahi kutumika kama wamishonari. Mahojiano hayo yalikazia jinsi Yehova anavyowatunza na kuwabariki wale wanaomtumikia kwa uaminifu. (Methali 10:22; 1 Petro 5:7) Mmishonari mmoja alisema: “Bila shaka Yehova alinitunza mimi na mke wangu kupitia elimu tuliyopokea katika Shule ya Gileadi. Kwa kweli iliimarisha imani yetu. Imani ni ya maana kwa sababu watumishi wote wa Mungu, kutia ndani wamishonari, watapata majaribu, matatizo, na mahangaiko.”

Endeleza Elimu ya Biblia Inayojenga Imani

Samuel Herd, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alifikisha programu hiyo kwenye kilele kizuri alipotoa hotuba yenye kichwa “Endelea Kuwajenga Ndugu Zako.” Ni nini kusudi la elimu ambayo wanafunzi walipokea? “Kusudi lake ni kuwafunza jinsi ya kutumia ulimi wenu kumsifu Yehova, kufundisha kweli zake katika maeneo mapya ambako mmetumwa, na kujengana katika imani,” akasema Ndugu Herd. Hata hivyo, aliwakumbusha wanafunzi kwamba ulimi unaweza pia kusema mambo yasiyojenga. (Methali 18:21; Yakobo 3:8-10) Aliwahimiza wanafunzi waige mfano wa Yesu wanapotumia ulimi wao. Pindi moja, baada ya kumsikiliza Yesu, wanafunzi wake walisema: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka . . . alipokuwa akitufungulia Maandiko?” (Luka 24:32) Ndugu Herd akasema hivi: “Maneno yenu yakiwa yenye kujenga, yatagusa mioyo ya ndugu na dada zenu katika migawo yenu.”

Kisha, wahitimu wakapokea diploma zao. Halafu barua ya shukrani za wanafunzi hao ilisomwa. Ilisema hivi: “Tunahisi kwamba tuna wajibu mzito wa kutumia mambo tuliyojifunza katika kutimiza kwa uaminifu migawo yetu tukiwa wamishonari. Tuko tayari kwenda mpaka sehemu za mwisho za dunia na tunasali ili jitihada zetu zimletee sifa kubwa Mfundishaji wetu Mkuu, Yehova Mungu.” Wasikilizaji waliitikia kwa kupiga makofi kwa shangwe. Bila shaka, programu hiyo ya kuhitimu ilijenga imani ya wahudhuriaji wote.

[Blabu katika ukurasa wa 17]

“Maneno yenu yakiwa yenye kujenga, yatagusa mioyo ya ndugu na dada zenu katika migawo yenu”

[Sanduku katika ukurasa wa 15]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi ambazo zimewakilishwa: 9

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 26

Idadi ya wanafunzi: 56

Wastani wa umri: 33.4

Wastani wa miaka katika kweli: 16.8

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13

[Picha katika ukurasa wa 16]

Darasa la 122 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Howitt, R.; Smith, P.; Martinez, A.; Pozzobon, S.; Kitamura, Y.; Laud, C. (2) Fiedler, I.; Beasley, K.; Matkovich, C.; Bell, D.; Lippincott, W. (3) Sites, W.; Andersen, A.; Toevs, L.; Fusano, G.; Rodríguez, C.; Yoo, J. (4) Sobomehin, M.; Thomas, L.; Gasson, S.; Dauba, V.; Bertaud, A.; Winn, C.; Dobrowolski, M. (5) Yoo, J.; Dauba, J.; Mixer, H.; Newton, M.; Rodríguez, F.; Mixer, N. (6) Laud, M.; Lippincott, K.; Martinez, R.; Haub, A.; Schamp, R.; Pozzobon, L.; Toevs, S. (7) Howitt, S.; Kitamura, U.; Newton, D.; Haub, J.; Sites, J.; Thomas, D. (8) Sobomehin, L.; Matkovich, J.; Fusano, B.; Winn, J.; Schamp, J.; Andersen, D.; Dobrowolski, J. (9) Fiedler, P.; Bell, E.; Beasley, B.; Smith, B.; Bertaud, P.; Gasson, M.