Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza Kupanuka Katika Upendo?

Je, Unaweza Kupanuka Katika Upendo?

Je, Unaweza Kupanuka Katika Upendo?

NI LAZIMA mnyororo unaoshikilia nanga ya meli ustahimili upepo mkali ili kuizuia meli isipeperushwe. Hata hivyo, hilo linawezekana tu ikiwa visehemu vya mnyororo ni salama na vyenye nguvu. Kama sivyo, mnyororo utakatika.

Ndivyo ilivyo na kutaniko la Kikristo. Ili kutaniko liwe lenye nguvu na hali nzuri, washiriki mmoja-mmoja wanahitaji kuunganishwa pamoja kwa umoja. Ni nini kinachowaunganisha? Upendo, ambao ni kifungo chenye nguvu zaidi cha umoja. Si ajabu kwamba Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” Bila shaka, Wakristo wa kweli wana upendo kati yao ambao unahusisha mengi zaidi ya kuwa tu marafiki na kuheshimiana. Wanasitawisha upendo wa kujidhabihu.—Yohana 13:34, 35.

Kuwathamini Waamini Wenzetu

Makutaniko mengi yana watu wa umri, makabila, mataifa, tamaduni, lugha, na malezi mbalimbali. Kila mshiriki ana mambo anayopenda na asiyopenda, yale anayotumaini na yale anayoogopa, na kwa kawaida kila mmoja ana mzigo wake ambao labda ni ugonjwa au matatizo ya kifedha. Tofauti hizo zinaweza kuhatarisha umoja wa Kikristo. Basi, ni nini kinachoweza kutusaidia tupanuke katika upendo na kudumisha umoja tujapokabili hali hizo ngumu? Kuwathamini kikweli washiriki wote wa kutaniko kutatusaidia kuwapenda zaidi wenzetu.

Hata hivyo, kumthamini mtu kunamaanisha nini? Kulingana na Kamusi ya Tuki, neno “thamini” linamaanisha ‘kufahamu, kutambua vyema, kufurahia, kupendezwa na.’ Ikiwa tunawathamini waamini wenzetu, tutajali mahitaji yao, tutawaheshimu sana, tutatambua sifa zao nzuri, na tutashukuru kwamba wanashirikiana nasi katika ibada. Kwa hiyo, upendo wetu kwao unazidi kukua. Kuchunguza kwa ufupi yale ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wa karne ya kwanza huko Korintho kutatusaidia tuone jinsi tunavyoweza kuonyesha upendo wa Kikristo kwa ukamili zaidi.

Wakorintho ‘Walisongwa Wakakosa Nafasi’

Paulo aliandika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho katika mwaka wa 55 W.K. na barua ya pili kabla ya mwaka huo kwisha. Maelezo yake yanaonyesha kwamba watu fulani katika kutaniko la Korintho hawakuwathamini waamini wenzao. Paulo alisema hivi kuhusu hali hiyo: “Kinywa chetu kimefunguliwa kwenu, enyi Wakorintho, moyo wetu umepanuka. Ninyi hamjasongwa mkakosa nafasi ndani yetu, lakini mmesongwa mkakosa nafasi katika upendo wenu mwororo.” (2 Wakorintho 6:11, 12) Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba walikuwa ‘wamesongwa wakakosa nafasi’?

Alimaanisha kwamba hawakupanuka na hawakuwa na moyo wa ukarimu. Msomi mmoja wa Biblia anasema kwamba upendo wa Wakorintho kwa Paulo “ulizuiwa na hali ngumu kwa sababu ya mashaka yasiyo na msingi . . . na kiburi cha kwamba wametendewa isivyo haki.”

Ona shauri hili ambalo Paulo alitoa: “Yakiwa kama malipo—mimi nasema kana kwamba ni kwa watoto—ninyi, pia, panukeni.” (2 Wakorintho 6:13) Paulo aliwatia moyo Wakorintho wapanuke katika upendo wao kwa waamini wenzao. Hilo lingemaanisha kwamba wangechochewa na mtazamo unaofaa na moyo wa ukarimu badala ya mashaka na matatizo madogo-madogo.

Kupanuka Katika Upendo Wetu Leo

Inatia moyo kuona jinsi waabudu wa kweli wa Mungu leo wanavyojitahidi sana kupanuka katika upendo kwa waabudu wenzao. Ni kweli kwamba kupanuka kunahitaji jitihada. Haitoshi tu kujua kwamba tunapaswa kupanuka. Kupanuka kunamaanisha tujiendeshe kwa njia tofauti na watu ambao hawaishi kupatana na viwango vya Biblia. Mara nyingi, watu hao hawawathamini wengine. Wanaweza kuwa wasiojali, wasio na heshima, na wenye dhihaka. Hivyo basi, tusikubali kamwe kuiga mitazamo hiyo. Ingesikitisha sana ikiwa upendo wetu ungezuiwa na mashaka yetu kuwaelekea wengine, kama wale Wakorintho. Hilo linaweza kutukia leo ikiwa sisi ni wepesi kuona makosa ya ndugu yetu Mkristo, lakini hatuwi wepesi kuona sifa zake nzuri. Hilo pia linaweza kutukia ikiwa tumesongwa na kushindwa kumpenda mtu fulani kwa sababu ni wa jamii tofauti.

Tofauti na hilo, mtumishi wa Mungu ambaye anapanuka katika upendo anawathamini kikweli waamini wenzake. Anawaheshimu sana, anatambua sifa zao nzuri, naye anajali mahitaji yao. Hata anapokuwa na sababu nzuri ya kulalamika, yuko tayari kusamehe naye anakataa kuweka kinyongo. Badala yake, anaamini kwamba waamini wenzake hawana nia mbaya. Moyo wa ukarimu unamsaidia kuonyesha upendo ambao Yesu alizungumzia alipotabiri hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—Yohana 13:35.

Tafuta na Ufanye Marafiki Wapya

Upendo kutoka moyoni utatuwezesha kutafuta marafiki wapya na kujitahidi kushirikiana na wale ambao kwa kawaida hatuna uhusiano wa karibu nao kutanikoni. Wanaweza kuwa akina nani? Kuna ndugu na dada zetu wengine ambao wanaona haya, au wana marafiki wachache kwa sababu fulani. Huenda mwanzoni tukahisi kwamba tuna mapendezi tofauti na watu hao ingawa tunashirikiana katika ibada. Lakini je, si ni kweli kwamba watu fulani waliokuwa marafiki wakubwa katika Biblia walikuwa watu ambao walionekana kuwa na mapendezi tofauti?

Kwa mfano, Ruthu na Naomi walikuwa na umri tofauti kabisa, walitoka katika mataifa na tamaduni tofauti, na hata walizungumza lugha tofauti. Hata hivyo, urafiki wao haukuharibiwa na tofauti hizo. Yonathani alilelewa akiwa mwana wa mfalme, naye Daudi alikuwa mchungaji. Umri wao ulitofautiana sana. Hata hivyo, urafiki wao ni mojawapo ya mahusiano ya karibu zaidi yanayotajwa katika Maandiko Matakatifu. Marafiki hao waliotajwa walileteana furaha na kutegemezana kiroho.—Ruthu 1:16; 4:15; 1 Samweli 18:3; 2 Samweli 1:26.

Hata leo, urafiki wa karibu unasitawi kati ya Wakristo wenye umri unaotofautiana sana au wale ambao hali zao za maisha ni tofauti kabisa. Kwa mfano, Regina ni mama asiye na mwenzi wa ndoa na ana watoto wawili matineja. * Ana ratiba yenye shughuli nyingi na hana wakati mwingi kuwa pamoja na marafiki. Harald na Ute ni wenzi wa ndoa waliostaafu na hawana watoto. Huenda ikaonekana kwamba familia hizo mbili zinatofautiana kabisa. Lakini Harald na Ute walifuata shauri la Biblia la kupanuka. Walimkaribisha Regina na watoto wake katika shughuli zao, walihubiri pamoja, na kufurahia tafrija pamoja nao.

Je, tunaweza kupanuka na kutafuta marafiki wengine wapya? Kwa nini usitafute marafiki wa karibu kati ya waamini wenzako wa mataifa, tamaduni, au umri tofauti na wako?

Kujali Mahitaji ya Wengine

Moyo wa ukarimu utatuchochea kujali mahitaji ya wengine. Mahitaji ya aina gani? Watazame washiriki wa kutaniko la Kikristo. Vijana wanahitaji mwongozo, wazee wanahitaji kutiwa moyo, wahudumu wa wakati wote wanahitaji kupongezwa na kutegemezwa, na waamini wenzetu walioshuka moyo wanahitaji mtu atakayewasikiliza. Kila mtu ana mahitaji. Tunataka kutosheleza mahitaji hayo kadiri ya uwezo wetu.

Pia, kupanuka kunamaanisha kuwafikiria wale walio na mahitaji ya pekee. Je, unamjua mtu fulani aliye na ugonjwa usiopona au aliye na tatizo lingine maishani? Kupanuka katika upendo na kusitawisha moyo wa ukarimu kutakusaidia kuwafikiria na kuwategemeza wenye uhitaji.

Unabii wa Biblia kuhusu wakati ujao unapotimia, vifungo vyenye nguvu vya umoja katika kutaniko vitakuwa na thamani zaidi kuliko vitu vya kimwili, uwezo, au mafanikio. (1 Petro 4:7, 8) Kila mmoja wetu anaweza kusaidia kuimarisha vifungo vya umoja katika kutaniko lake kwa kupanuka katika upendo kuelekea waamini wenzake. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatubariki tukitenda kupatana na maneno haya yaliyosemwa na Mwana wake, Yesu Kristo: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda ninyi.”—Yohana 15:12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 10]

Kuwathamini ndugu na dada zetu kunamaanisha tunawaheshimu sana wote, tunatambua sifa zao nzuri, na tunajali mahitaji yao