Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukubali Mialiko ya Yehova Huthawabisha

Kukubali Mialiko ya Yehova Huthawabisha

Simulizi la Maisha

Kukubali Mialiko ya Yehova Huthawabisha

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA MARIA DO CÉU ZANARDI

“Yehova anajua anachofanya. Ikiwa amekupatia mwaliko huu, unapaswa kuukubali kwa unyenyekevu.” Maneno hayo yaliyosemwa na babangu miaka 45 hivi iliyopita, yalinisaidia kukubali mwaliko wa kwanza niliopokea kutoka kwa tengenezo la Yehova wa kutumikia nikiwa mhudumu wa wakati wote. Leo, ningali ninashukuru kwa ushauri wa baba kwa sababu kukubali mialiko hiyo kumenithawabisha sana.

KATIKA mwaka wa 1928, Baba aliandikisha gazeti la Mnara wa Mlinzi na akaanza kupendezwa na Biblia. Kwa kuwa alikuwa akiishi katikati mwa Ureno angeweza tu kuwasiliana na kutaniko la Mungu kupitia vichapo alivyopokea kwa njia ya posta na kupitia Biblia iliyokuwa ya babu na nyanya yangu. Katika mwaka wa 1949, nilipokuwa na umri wa miaka 13, familia yetu ilihamia kwenye vitongoji vya Rio de Janeiro, Brazili, nchi alikozaliwa Mama.

Majirani wetu wapya walitualika twende kwenye kanisa lao, nasi tukaenda mara chache. Baba alipenda kuwauliza maswali kuhusu moto wa mateso, nafsi, na kuhusu hali ya baadaye ya dunia, lakini hawakuweza kumjibu. “Itatubidi tungojee tu wanafunzi wa kweli wa Biblia,” Baba alikuwa akisema.

Siku moja, mwanamume mmoja asiyeweza kuona alitutembelea nyumbani akatupatia magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Baba alimwuliza maswali yaleyale, naye akamjibu vizuri akitumia Biblia. Juma lililofuata tulitembelewa na Shahidi mwingine wa Yehova. Baada ya kujibu maswali zaidi, aliomba radhi na kusema kwamba ilimbidi aende “shambani.” Kwa kuwa Baba hakuelewa alichomaanisha, Shahidi huyo alimsomea Mathayo 13:38: “Shamba ndio ulimwengu.” Ndipo Baba akauliza: “Ninaweza kwenda pia?” “Ndiyo,” akajibiwa. Tulifurahi sana kupata kweli ya Biblia tena! Baba alibatizwa kwenye mkusanyiko uliofuata, nami nikabatizwa muda mfupi baadaye, katika Novemba 1955.

Kukubali Mwaliko Wangu wa Kwanza

Mwaka mmoja na nusu baadaye, nilipokea bahasha kubwa ya rangi ya kahawia kutoka ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Rio de Janeiro iliyokuwa na mwaliko wa kujiunga na kazi ya kuhubiri wakati wote. Afya ya Mama ilikuwa mbaya sana wakati huo, hivyo nikamwomba baba ushauri. “Yehova anajua anachofanya,” akasema kwa mkazo. “Ikiwa amekupatia mwaliko huu, unapaswa kuukubali kwa unyenyekevu.” Maneno hayo yalinitia moyo, nikajaza fomu ya maombi na kujiunga na utumishi wa wakati wote Julai 1, 1957. Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa katika mji wa Três Rios, katika Jimbo la Rio de Janeiro.

Mwanzoni, wakazi wa Três Rios hawakutaka kusikiliza ujumbe wetu kwa sababu hatukuwa tukitumia tafsiri ya Biblia ya Katoliki. Tulipata msaada tulipoanza kujifunza Biblia na Geraldo Ramalho, mfuasi wa dini ya Katoliki. Alinisaidia kupata Biblia iliyokuwa na sahihi ya kasisi wa huko. Kuanzia wakati huo na kuendelea, nilikuwa nikimnyamazisha yeyote aliyetokeza upingamizi kwa kumwonyesha sahihi ya kasisi. Geraldo alibatizwa baadaye.

Nilifurahi sana wakati kusanyiko la mzunguko lilipofanywa katikati mwa mji wa Três Rios mwaka wa 1959. Mkuu wa polisi, aliyekuwa anajifunza Biblia wakati huo, hata alipanga kuweka mabango yaliyotangaza programu ya kusanyiko hilo kotekote mjini. Baada ya kufanya kazi kwa miaka mitatu huko Três Rios, nilipewa mgawo mpya wa kwenda mji wa Itu, umbali wa kilometa 110 hivi magharibi ya São Paulo.

Vitabu Vyenye Rangi Nyekundu, Bluu na Manjano

Baada ya kutafuta nyumba kwa muda, mimi na painia mwenzangu tulipangishwa nyumba nzuri katikati mwa mji na mjane mwenye huruma aitwaye Maria. Maria alitutendea kama binti zake. Hata hivyo, baada ya muda mfupi askofu wa Kanisa Katoliki la Itu alimtembelea na kumwambia atufukuze, lakini akakataa na kusema: “Mume wangu alipokufa, hamkunifariji hata kidogo. Mashahidi hawa wa Yehova wamenisaidia hata ingawa mimi si mfuasi wa dini yao.”

Yapata wakati huohuo, mwanamke mmoja alituambia kwamba makasisi Wakatoliki wa Itu walikuwa wamewakataza waumini wao wasichukue “kile kitabu chekundu kuhusu Ibilisi.” Walimaanisha kitabu, “Let God Be True”, kichapo kinachotegemea Biblia ambacho tulikuwa tukitolea watu juma hilo. Kwa kuwa kitabu hicho chekundu “kilipigwa marufuku” na makasisi, tulijitayarisha kutoa kitabu cha bluu (“New Heavens and a New Earth”). Baadaye, makasisi waliposikia kuhusu kitabu hiki cha bluu, tulianza kutumia kitabu cha manjano (What Has Religion Done for Mankind?), na vitabu vinginevyo. Ilifaa kama nini kwamba tulikuwa na vitabu mbalimbali vyenye majalada ya rangi tofauti-tofauti!

Baada ya kukaa Itu kwa mwaka mmoja hivi, nilipokea mwaliko kupitia telegramu wa kwenda kufanya kazi kwa muda kwenye Betheli, ambayo ni ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Rio de Janeiro. Kazi hiyo ilihusiana na matayarisho ya kusanyiko la kitaifa. Nilikubali mwaliko huo kwa furaha.

Migawo Zaidi na Magumu Mengi Zaidi

Kulikuwa na kazi ya kutosha Betheli, na nilifurahia kusaidia kwa njia yoyote ile. Ilithawabisha kama nini kuhudhuria mazungumzo ya andiko la kila siku na Funzo la Mnara wa Mlinzi kila Jumatatu jioni! Niliguswa moyo sana na sala za kutoka moyoni za Otto Estelmann na washiriki wengine wenye uzoefu wa familia ya Betheli.

Baada ya kusanyiko la kitaifa, nilifunganya virago kurudi Itu, lakini nilishangaa wakati mtumishi wa ofisi ya tawi, Grant Miller, aliponipa barua ya kunialika niwe mshiriki wa kudumu wa familia ya Betheli. Nilikaa chumba kimoja na Dada Hosa Yazedjian, ambaye angali anatumikia katika Betheli ya Brazili. Siku hizo Wanabetheli walikuwa wachache—tulikuwa 28 tu—na sote tulikuwa marafiki sana.

Katika mwaka wa 1964, João Zanardi, mhudumu wa wakati wote aliyekuwa kijana, alikuja Betheli kuzoezwa. Kisha akapewa mgawo wa kuwa mtumishi wa mzunguko au mwangalizi asafiriye katika eneo lililokuwa karibu. Tulikutana mara kwa mara alipokuja Betheli kutoa ripoti zake. Mtumishi wa Betheli alimruhusu João awe anahudhuria funzo la familia ya Betheli Jumatatu jioni, hivyo tuliweza kuwa na wakati mwingi pamoja. Mimi na João tulioana Agosti 1965. Nilifurahi kujiunga na mume wangu katika kazi ya kuzunguka.

Wakati huo ilihitaji ujasiri kufanya kazi ya kuzunguka katika maeneo ya ndanindani ya Brazili. Sitasahau ziara tulizofanya kwa kikundi cha wahubiri huko Aranha, Jimbo la Minas Gerais. Ilitubidi tusafiri kwa gari-moshi kisha kutembea kwa miguu sehemu iliyobaki ya safari hiyo, huku tukiwa tumebeba masanduku, mashine ya chapa, mashine ya kuonyeshea slaidi, mikoba ya mahubiri, na vichapo. Kila mara tulifurahi sana kumkuta Lourival Chantal, ndugu mzeemzee, ambaye alikuja kutulaki kwenye kituo cha gari-moshi ili kutusaidia kubeba mizigo.

Mikutano huko Aranha ilifanywa katika nyumba ya kupangisha. Tulilala katika chumba kidogo nyuma ya nyumba hiyo. Chumba hicho kilikuwa na mahali pa kuwashia moto wa kuni tuliotumia kupikia na kupashia moto maji ambayo akina ndugu walituletea kwa ndoo. Choo chetu kilikuwa shimo lililokuwa katikati ya shamba la mianzi. Tulilala taa yetu ya koroboi ikiwa imewaka ili kufukuza mbawakavu—mdudu aina ya mende ambaye anaweza kuambukiza maradhi ya Chagas. Kila asubuhi mapua yetu yalikuwa meusi kwa sababu ya moshi. Hiyo kwa kweli ilikuwa hali isiyo ya kawaida.

Tulipokuwa tukifanya kazi ya kuzunguka katika Jimbo la Paraná, tulipokea tena bahasha kubwa ya rangi ya kahawia kutoka ofisi ya tawi. Naam, mgawo mwingine kutoka kwa tengenezo la Yehova wa kwenda Ureno! Barua hiyo ilitushauri tufikirie kanuni ya andiko la Luka 14:28 kisha tuhesabu gharama kabla ya kukubali mgawo huo kwa sababu kazi yetu ya Kikristo ilikuwa imepigwa marufuku huko, nao ndugu wengi walikuwa wamekamatwa na serikali ya Ureno.

Je, tungeenda katika nchi ambako tungepata mnyanyaso kama huo? “Iwapo ndugu zetu Wareno wanaweza kuishi huko na kumtumikia Yehova kwa uaminifu, mbona sisi tushindwe?” João akasema. Nilikumbuka maneno yenye kutia moyo ya babangu na kusema hivi: “Ikiwa Yehova ametupatia mwaliko huu, tunapaswa kuukubali na kumtumaini.” Muda mfupi baadaye, tulienda kwenye Betheli huko São Paulo ili kupata maagizo zaidi na kutayarisha hati za kusafiria.

João Maria na Maria João

Meli yetu iitwayo, Eugênio C, ilianza safari yake kutoka bandari ya Santos, Jimbo la São Paulo, Septemba 6, 1969. Tulifika Ureno baada ya kusafiri baharini kwa siku tisa. Mwanzoni, tulihubiri kwa miezi kadhaa na ndugu wenye uzoefu katika barabara nyembamba za Alfama na Mouraria, katika wilaya ya zamani ya Lisbon. Walituzoeza kuwa waangalifu ili tusikamatwe kwa urahisi na polisi.

Mikutano ya kutaniko ilifanywa katika nyumba za Mashahidi. Tulipoona kwamba majirani walikuwa wanaanza kushuku, tulibadili upesi mahali pa kufanyia mikutano ili tusivamiwe au ndugu wasikamatwe. Makusanyiko yetu yaliyojulikana kama tafrija yalifanyiwa katika bustani ya Monsanto Park, kwenye vitongoji vya Lisbon, na Costa da Caparica, eneo la pwani lililokuwa na msitu. Tulivalia nguo za kawaida wakati huo, nao wakaribishaji walisimama chonjo sehemu mbalimbali. Ikiwa mtu yeyote waliyemshuku angetokea, tungekuwa na wakati wa kutosha kuanza mchezo fulani, kuandaa viburudisho, au kuanza kuimba wimbo fulani wa kitamaduni.

Tuliepuka kutumia majina yetu halisi ili polisi wasiweze kututambua kwa urahisi. Akina ndugu walituita tu João Maria na Maria João. Majina yetu hayakutumiwa kwenye barua au rekodi zozote. Badala yake, tulipewa namba. Niliamua kimakusudi kutoweka akilini anwani za akina ndugu. Kwa njia hiyo, singeweza kuwasaliti iwapo ningekamatwa.

Licha ya vizuizi, mimi na João tuliazimia kutumia kila nafasi kutoa ushahidi kwa kuwa tulijua kwamba tungeweza kupoteza uhuru wetu wakati wowote. Tulijifunza kumtegemea Baba yetu wa mbinguni, Yehova. Yeye ndiye aliyekuwa Mlinzi wetu na alitumia malaika zake hivi kwamba tulihisi tulikuwa ‘tunamwona Yeye asiyeonekana.’—Waebrania 11:27.

Pindi moja tulipokuwa tukihubiri nyumba kwa nyumba huko Porto, tulikutana na mtu aliyesisitiza twende kwake. Dada niliyekuwa nikihubiri naye alikubali mara moja, nami sikuwa na lingine ila kuandamana naye. Nilishtuka kuona picha ya mtu aliyevalia mavazi ya kijeshi ukutani. Tutafanya nini sasa? Mtu huyo alituomba tuketi chini, kisha akaniuliza: “Je, ungemruhusu mwanao ajiunge na jeshi kama angetakiwa kufanya hivyo?” Halikuwa swali rahisi. Baada ya kusali kimyakimya, nilimjibu kwa utulivu hivi: “Sina watoto wowote, na nina hakika kwamba kama ningekuuliza swali kama hilo kuhusu mambo ya kuwaziwa tu, ungenijibu vivyo hivyo.” Akanyamaza. Kisha nikaendelea kusema: “Kama ungeniuliza jinsi mtu anavyohisi anapofiwa na ndugu au baba, ningeweza kukujibu kwa kuwa ndugu yangu na babangu wamekufa.” Macho yangu yalilengalenga machozi nilipozungumza, nami niliona kwamba hata yeye pia alikuwa karibu kulia. Alinieleza kwamba mke wake alikuwa amekufa karibuni. Alisikiliza kwa makini nilipomweleza kuhusu ufufuo. Kisha tukaagana kwa upole na kuondoka salama, tukiacha mambo mikononi mwa Yehova.

Licha ya marufuku hayo, watu wenye mioyo minyofu walisaidiwa kupata ujuzi wa ile kweli. Huko Porto, mume wangu alianza kujifunza na Horácio, mfanya-biashara aliyefanya maendeleo haraka sana. Baadaye, mwanawe Emílio, aliyekuwa daktari mzuri, pia aliamua kumtumikia Yehova na akabatizwa. Kwa kweli, hakuna kinachoweza kuizuia roho takatifu ya Yehova.

“Hamjui Yehova Ataruhusu Nini”

Katika mwaka wa 1973, mimi na João tulialikwa kuhudhuria Mkusanyiko wa Kimataifa wa “Ushindi wa Kimungu” huko Brussels, Ubelgiji. Kulikuwa na ndugu wengi kutoka Hispania na Ubelgiji, na pia wajumbe kutoka Msumbiji, Angola, Cape Verde, Madeira, na Azores. Katika maelezo yake ya kumalizia, Ndugu Knorr, kutoka makao makuu huko New York, alituhimiza hivi: “Endeleeni kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Hamjui Yehova ataruhusu nini. Kwani, huenda mkahudhuria mkusanyiko wa kimataifa hapa Ureno!”

Mwaka uliofuata kazi yetu ya kuhubiri ilitambuliwa kisheria nchini Ureno. Maneno ya Ndugu Knorr yalithibitika kuwa kweli kwa kuwa Aprili 25, 1978, tulifanya mkusanyiko wetu wa kwanza wa kimataifa huko Lisbon. Lilikuwa pendeleo lililoje kutembea katika barabara za Lisbon, huku tukitoa ushahidi kwa mabango na magazeti, na pia kualika watu kwenye hotuba ya watu wote! Ilikuwa kama ndoto iliyotimia.

Tuliwapenda sana ndugu zetu Wareno ambao wengi wao walifungwa na kupigwa kwa kudumisha msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote kisiasa. Tulitaka kuendelea kutumikia huko Ureno. Hata hivyo, haikuwezekana. Katika mwaka wa 1982, João alipatwa na ugonjwa mbaya wa moyo, na ofisi ya tawi ikapendekeza turudi Brazili.

Wakati Mgumu

Ndugu katika ofisi ya tawi ya Brazili walikuwa wenye fadhili sana nao walitupatia mgawo wa kutumikia katika Kutaniko la Quiririm huko Taubaté, Jimbo la São Paulo. Afya ya João ilidhoofika haraka, na muda si muda akawa hawezi kutoka nyumbani. Watu wenye kupendezwa walikuja nyumbani kwetu kujifunza Biblia. Funzo la kitabu la kila juma na mikutano ya utumishi wa shambani ya kila siku ilifanyiwa nyumbani kwetu pia. Mipango hiyo ilitusaidia kudumisha hali nzuri ya kiroho.

João aliendelea kufanya yale aliyoweza katika utumishi wa Yehova hadi alipokufa Oktoba 1, 1985. Nilihuzunika na kushuka moyo kwa kiasi fulani, lakini niliazimia kuendelea na mgawo wangu. Kipingamizi kingine kilitokea Aprili 1986 wakati wezi walipovunja nyumba yangu na kuiba karibu kila kitu. Kwa mara ya kwanza maishani mwangu, nilihisi mpweke na mwenye woga. Wenzi fulani wa ndoa walinialika kwa upendo nikae pamoja nao kwa muda, nami nilishukuru sana kwa jambo hilo.

Kifo cha João na wizi huo ziliathiri pia utumishi wangu kwa Yehova. Sikuhisi nikiwa na uhakika katika huduma. Baada ya kuiandikia ofisi ya tawi kuhusu tatizo hilo, nilialikwa kukaa Betheli kwa muda fulani ili niweze kupata utulivu. Nilitiwa nguvu kama nini wakati huo!

Mara tu nilipopata nafuu kidogo, nilikubali mgawo wa kutumikia huko Ipuã, mji ulio katika jimbo la São Paulo. Nilikuwa na shughuli nyingi za kuhubiri, lakini kuna nyakati nilipohisi nimevunjika moyo. Nikihisi hivyo nilikuwa nikiwapigia simu ndugu wa Quiririm, kisha familia fulani ilinitembelea kwa siku kadhaa. Ziara hizo zilinitia moyo kwelikweli! Mwaka wangu wa kwanza huko Ipuã, ndugu na dada mbalimbali 38 walifunga safari ndefu kuja kuniona.

Katika mwaka 1992, miaka sita baada ya João kufa, nilipata mwaliko mwingine kutoka kwa tengenezo la Yehova wa kwenda Franca, Jimbo la São Paulo, ambako ningali ninatumikia nikiwa mhudumu wa wakati wote. Eneo hili lina matokeo sana. Katika mwaka wa 1994, nilianza kujifunza Biblia na meya mmoja. Wakati huo, alikuwa akigombea kiti katika bunge la Brazili, na ingawa alikuwa na shughuli nyingi, tulijifunza kila Jumatatu alasiri. Alikuwa akizima simu yake ili tusisumbuliwe. Nilifurahi sana kuona akiacha siasa polepole na, kwa msaada wa ile kweli akaboresha ndoa yake! Yeye na mkewe walibatizwa mwaka wa 1998.

Ninapokumbuka yaliyopita, ninaweza kusema kwamba nimebarikiwa sana na kupata mapendeleo mengi sana ya kumtumikia Yehova nikiwa mhudumu wa wakati wote. Kukubali mialiko ambayo Yehova amenipatia kupitia tengenezo lake, kumenithawabisha kwelikweli. Mimi niko tayari kabisa kukubali mialiko yoyote ninayoweza kupata wakati ujao.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mwaka wa 1957, nilipoanza utumishi wa wakati wote, na leo

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na familia ya Betheli ya Brazili mwaka wa 1963

[Picha katika ukurasa wa 27]

Arusi yetu mnamo Agosti 1965

[Picha katika ukurasa wa 27]

Kusanyiko huko Ureno wakati kazi yetu ilipokuwa imepigwa marufuku

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kutoa ushahidi barabarani huko Lisbon wakati wa Mkusanyiko wa Kimataifa wa “Imani Yenye Ushindi” mwaka wa 1978