Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Enoki Alitembea Pamoja na Mungu Katika Ulimwengu Wenye Dhambi

Enoki Alitembea Pamoja na Mungu Katika Ulimwengu Wenye Dhambi

Enoki Alitembea Pamoja na Mungu Katika Ulimwengu Wenye Dhambi

IBILISI anadai kwamba anaweza kufanya watu wote wamwache Mungu, na nyakati nyingine imeonekana kana kwamba amefaulu. Kwa karibu miaka 500 baada ya kifo cha Abeli, hakukuwa na yeyote aliyejidhihirisha kuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova. Badala yake, mwenendo mbaya wenye dhambi ulikuwa jambo la kawaida.

Enoki aliishi wakati huo wenye upotovu wa kiroho. Matukio ya Biblia yanaonyesha kwamba alizaliwa mwaka wa 3404 K.W.K. Enoki alikuwa tofauti na marika wake, alipata kibali cha Mungu. Mtume Paulo alionyesha kwamba Enoki alikuwa mmojawapo wa watumishi wa Yehova wenye imani inayostahili kuigwa na Wakristo. Enoki alikuwa nani? Alikabili magumu gani? Aliyashindaje? Na uaminifu wake unatuhusuje?

Katika siku za Enoshi, karibu miaka 400 kabla ya siku za Enoki, “watu wa[li]anza kuliita Jina la BWANA [“Yehova,” NW].” (Mwanzo 4:26) Jina la Mungu lilikuwa limetumiwa tangu kuumbwa kwa mwanadamu. Kwa hiyo, watu hawakuanza kumwita Yehova kwa imani na katika ibada safi katika siku za Enoshi. Wasomi fulani wa Kiebrania wanasisitiza kwamba andiko la Mwanzo 4:26 linapasa kusema “walianza kukufuru” au “ndipo kukufuru kulipoanza.” Huenda watu walijiita Yehova au kuwaita watu wengine jina hilo, wakisingizia kuwa wanamwabudu Mungu kupitia watu hao. Au huenda waliziita sanamu kwa jina la Mungu.

‘Enoki Alitembea Pamoja na Mungu wa Kweli’

Ijapokuwa dhambi ilienea kila mahali, Enoki “a[li]enda [“alitembea,” NW] pamoja na Mungu” wa kweli, Yehova. Biblia haisemi kwamba wazao wake—Sethi, Enoshi, Kenani, Mahalaleli, na Yaredi—walitembea pamoja na Mungu. Angalau hawakufanya hivyo kwa kadiri ambavyo Enoki alifanya. Yamkini mwenendo wake ulikuwa tofauti sana na wao.—Mwanzo 5:3-27.

Kutembea pamoja na Yehova kulidokeza kwamba Enoki alikuwa na urafiki pamoja na Mungu. Aliweza kuwa na urafiki huo tu kwa sababu aliishi kupatana na mapenzi ya Mungu. Yehova alikubali ibada ya Enoki. Tafsiri ya Kigiriki inayoitwa Septuagint inasema kwamba “Enoki alimpendeza [Mungu] vyema,” jambo ambalo hata mtume Paulo alitaja.—Mwanzo 5:22, NW, kielezi-chini; Waebrania 11:5.

Enoki aliweza kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova kwa sababu ya imani yake. Bila shaka aliamini ile ahadi kuhusu “mbegu” ya “mwanamke” wa Mungu. Ikiwa Enoki alifahamiana vizuri na Adamu, angeweza kupata habari fulani kuhusu jinsi ambavyo Mungu alishughulika na wanadamu wa kwanza wawili huko Edeni. Ujuzi aliokuwa nao juu ya Mungu ulimsukuma Enoki ‘amtafute kwa bidii.’—Mwanzo 3:15, NW; Waebrania 11:6, 13.

Sote, kama Enoki, tunahitaji kufanya mengi zaidi kuliko kujifunza tu juu ya Mungu, ikiwa tunataka kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova. Tukithamini sana urafiki wetu na mtu fulani, si kweli kwamba tunapatanisha mawazo na matendo yetu na maoni yake? Tunaepuka maneno na matendo yanayoweza kuvunja urafiki huo. Na tukinuia kufanya mabadiliko maishani mwetu, je, hatufikirii jinsi ambavyo mabadiliko hayo yataathiri uhusiano huo.

Mwenendo wetu unahusika vilevile tukitaka kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Kwanza tunahitaji kujua kwa usahihi kile ambacho Mungu anakubali na kile ambacho hakubali. Kisha tunapaswa kuongozwa na ujuzi huo, tukijitahidi kumpendeza kwa mawazo na matendo.

Naam, ili tutembee pamoja na Mungu, lazima tumpendeze. Ndivyo alivyofanya Enoki kwa miaka mingi. Kwa kweli, kitenzi cha Kiebrania kinachoonyesha kwamba Enoki “alitembea” pamoja na Mungu, kinaonyesha tendo linalofanywa kwa kuendelea na kwa kurudiwa-rudiwa. Noa pia alikuwa mtu mwaminifu ‘aliyetembea pamoja na Mungu.’—Mwanzo 6:9, NW.

Enoki alikuwa na mke na “wana, waume na wake,” waliomtegemea. Methusela alikuwa mmoja wa wana wake. (Mwanzo 5:21, 22) Bila shaka Enoki alijitahidi sana kusimamia jamaa yake kwa njia bora. Hata hivyo, haikuwa rahisi kwake kumtumikia Mungu kwa sababu ya dhambi iliyoenea kotekote. Huenda Lameki aliyekuwa baba ya Noa, ndiye pekee aliyemwamini Yehova miongoni mwa marika wa Enoki. (Mwanzo 5:28, 29) Hata hivyo, Enoki aliendelea kwa ujasiri kumwabudu Yehova.

Ni nini kilichomsaidia Enoki kudumisha uaminifu wake kwa Mungu? Bila shaka aliepuka kushirikiana na wale waliokufuru jina la Yehova au wengine ambao hawakuwa washiriki wafaao kwa mwabudu wa Mungu. Bila shaka, Enoki alimwomba Yehova msaada ili aweze kushikilia uamuzi wake wa kutofanya chochote kisichompendeza Muumba wake.

Unabii Dhidi ya Watu Wenye Dhambi

Kudumisha maadili mazuri katikati ya watu wenye dhambi si jambo rahisi. Lakini Enoki aliwatolea waovu ujumbe wa hukumu usioweza kubadilishwa. Enoki alitoa unabii huu akiongozwa na roho ya Mungu: “Tazama! Yehova alikuja na makumi ya maelfu yake watakatifu, kutekeleza hukumu dhidi ya wote, na kuwathibitisha ni wenye hatia wote wasiomwogopa Mungu kuhusu vitendo vyao vyote vya kutomwogopa Mungu ambavyo walitenda kwa njia ya kutomwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kushtua ambayo watenda-dhambi wasiomwogopa Mungu walisema dhidi yake.”—Yuda 14, 15.

Ujumbe huo ungewaathirije watu wasioamini waliopotoka? Yamkini maneno hayo yenye kuchoma yalifanya watu wamchukie Enoki, na huenda walimdhihaki na kumfanyia mzaha na kumtisha. Bila shaka baadhi yao walitaka kumwua. Hata hivyo, Enoki hakuogopa. Alijua kile kilichompata Abeli mwadilifu, na kama vile yeye, Enoki aliazimia kumtumikia Mungu katika hali zote.

“Mungu Alimtwaa”

Yaelekea maisha ya Enoki yalikuwa hatarini ‘Mungu alipomtwaa.’ (Mwanzo 5:24) Yehova hakuruhusu nabii wake mwaminifu kuteseka mikononi mwa maadui wakatili. Kulingana na mtume Paulo, “Enoki alihamishwa ili asione kifo.” (Waebrania 11:5) Wengi husema kwamba Enoki hakufa, bali Mungu alimpeleka mbinguni, na aliendelea kuishi huko. Hata hivyo, Yesu alisema hivi kinaganaga: “Hakuna mtu ambaye amepaa kuingia mbinguni ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, Mwana wa binadamu.” Yesu alikuwa “mtangulizi” wa wote watakaoenda mbinguni.—Yohana 3:13; Waebrania 6:19, 20.

Kwa hiyo, ni nini kilichompata Enoki? Enoki ‘alipohamishwa ili asione kifo,’ huenda alipata njozi ya kiunabii kutoka kwa Mungu, kisha Mungu akaondoa uhai wake alipokuwa akiona njozi hiyo. Enoki hakupatwa na maumivu ya kifo alipokufa kwa njia hiyo. Naye “akatoweka,” yamkini kwa sababu Yehova aliondoa mwili wake, kama ambavyo aliondoa mwili wa Musa.—Kumbukumbu la Torati 34:5, 6.

Enoki aliishi kwa muda wa miaka 365—muda mfupi sana ukilinganishwa na muda ambao wengi wa marika yake waliishi. Lakini jambo muhimu kwa wale wanaompenda Yehova ni kumtumikia kwa uaminifu hadi mwisho wa maisha yao. Tunajua kwamba Enoki alifanya hivyo kwa kuwa “kabla ya uhamisho wake alikuwa na ushahidi kwamba alikuwa amempendeza Mungu vema.” Maandiko hayasemi jinsi Yehova alivyomwambia Enoki jambo hilo. Hata hivyo, kabla ya kifo chake, Enoki alihakikishiwa kwamba alikuwa na kibali cha Mungu, na tuna uhakika kwamba Yehova atamkumbuka katika ufufuo.

Iga Imani ya Enoki

Kwa kufaa, tunaweza kuiga imani ya watu wanaomcha Mungu. (Waebrania 13:7) Enoki, nabii mwaminifu wa kwanza, alimtumikia Mungu kwa imani. Ulimwengu wa siku za Enoki ulikuwa kama wetu—wenye ujeuri, wenye kukufuru, na wenye dhambi. Lakini Enoki alikuwa tofauti. Alikuwa na imani thabiti na alijitoa kikamili katika ibada ya Mungu. Naam, Yehova alimpa ujumbe muhimu wa hukumu, na vilevile nguvu ya kuutangaza. Enoki alitangaza ujumbe wake kwa ujasiri, na Mungu alimlinda alipokabili upinzani kutoka kwa maadui.

Tukiwa na imani kama ya Enoki, Yehova atatuimarisha tuutangaze ujumbe wake katika siku hizi za mwisho. Mungu atatusaidia kukabili upinzani kwa ujasiri, na ujitoaji wetu kwake utafanya tuwe tofauti sana na watu wenye dhambi. Imani itatuwezesha kutembea pamoja na Mungu kwa njia inayofurahisha moyo wake. (Mithali 27:11) Kwa imani, Enoki alifaulu kutembea pamoja na Yehova katika ulimwengu wenye dhambi, na tunaweza kufaulu vilevile.

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

Je, Biblia Inanukuu Kutoka Kitabu cha Enoki?

Kitabu cha Enoki si sehemu ya Maandiko Matakatifu, na kimepewa jina la Enoki kimakosa. Yamkini kiliandikwa katika karne ya kwanza na ya pili K.W.K., nacho ni mkusanyo wa hekaya za Wayahudi zilizotiwa chumvi na zisizopatana na historia. Yaelekea kiliandikwa kwa kusudi la kueleza na kuchambua habari ya Enoki inayopatikana katika kitabu cha Mwanzo. Jambo hilo linafanya watu wanaopenda Neno la Mungu wakipuuze.

Kitabu cha Biblia cha Yuda ndicho pekee hutaja maneno haya ya unabii ya Enoki: “Tazama! Yehova alikuja na makumi ya maelfu yake watakatifu, kutekeleza hukumu dhidi ya wote, na kuwathibitisha ni wenye hatia wote wasiomwogopa Mungu kuhusu vitendo vyao vyote vya kutomwogopa Mungu ambavyo walitenda kwa njia ya kutomwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kushtua ambayo watenda-dhambi wasiomwogopa Mungu walisema dhidi yake.” (Yuda 14, 15) Wasomi wengi husisitiza kwamba unabii wa Enoki dhidi ya watu wenye dhambi wa kizazi chake umenukuliwa moja kwa moja kutoka katika Kitabu cha Enoki. Je, inawezekana kwamba Yuda alitoa habari zake kutokana na kitabu kisicho cha kweli na kisicho sehemu ya Maandiko Matakatifu?

Maandiko hayasemi jinsi Yuda alivyojua unabii wa Enoki. Huenda alinukuu mapokeo ya kale yaliyoaminika. Yaelekea Paulo alifanya hivyo alipotaja majina ya Yanesi na Yambresi, wachawi wawili waliomtumikia Farao na kumpinga Musa, ambao hawakujulikana kwa majina mbeleni. Ikiwa mwandishi wa Kitabu cha Enoki aliweza kutoa habari katika mapokeo kama hayo, kwa nini Yuda hangaliweza kufanya hivyo? *Kutoka 7:11, 22; 2 Timotheo 3:8.

Jinsi Yuda alivyopata habari kuhusu ujumbe ambao Enoki aliwatangazia watu wenye dhambi si jambo muhimu. Tunajua kwamba habari hiyo ni ya kweli kwa kuwa Yuda aliongozwa na roho ya Mungu alipoiandika. (2 Timotheo 3:16) Roho takatifu ya Mungu ilimzuia asiandike chochote kisichokuwa cha kweli.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 28 Mwanafunzi Stefano pia alitueleza habari ambazo hazipatikani katika kitabu kingine cha Biblia. Habari hizo zilieleza jinsi Musa alivyoelimishwa huko Misri, kwamba alikuwa na umri wa miaka 40 alipokimbia Misri, kwamba alikaa huko Midiani kwa miaka 40, na kwamba alipewa Sheria na malaika.—Matendo 7:22, 23, 30, 38.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Enoki alitangaza ujumbe wa Yehova kwa ujasiri