Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ibada ya Kweli Huunganisha Watu

Ibada ya Kweli Huunganisha Watu

Ibada ya Kweli Huunganisha Watu

INGAWA kwa ujumla dini huelekea kugawanya watu, ibada ya Mungu wa pekee wa kweli ina nguvu za kuunganisha watu. Waisraeli walipokuwa taifa teule la Mungu, watu wengi wasio Wayahudi waliokuwa wanyofu, walivutiwa na ibada ya kweli. Kwa mfano, Ruthu aliacha miungu ya nchi ya kwao ya Moabu na kumwambia Naomi hivi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Ruthu 1:16) Kufikia karne ya kwanza W.K., watu wengi wasio Wayahudi walikuwa waabudu wa Mungu wa kweli. (Matendo 13:48; 17:4) Baadaye, wakati mitume wa Yesu walipoanza kupeleka habari njema katika maeneo ya mbali, watu wengine wanyofu walijiunga na ibada ya Mungu wa kweli. ‘Mlimgeukia Mungu kutoka kwenye sanamu zenu ili mtumikie kama watumwa Mungu aliye hai na wa kweli,’ akaandika mtume Paulo. (1 Wathesalonike 1:9) Je, ibada ya Mungu wa kweli ina nguvu za wa kuunganisha watu hivyo hata leo?

Watu wenye kutilia shaka husisitiza kwamba ni kosa kuzungumza juu ya “waabudu wa kweli” au “Mungu wa kweli.” Huenda wakahisi hivyo kwa sababu hawajui ni wapi wanapoweza kupata kweli. Lakini watu wanaotafuta kweli kutoka malezi mbalimbali wanatambua kwamba ibada haitegemei uchaguzi wa kibinafsi tu. Muumba wa vitu vyote, Yehova Mungu, ndiye pekee anayestahili ibada yetu. (Ufunuo 4:11) Yeye ndiye Mungu wa kweli, na ana haki ya kuamua jinsi anavyopaswa kuabudiwa.

Ili kutusaidia kuelewa matakwa yake, Yehova amewasiliana nasi kupitia Neno lake, Biblia. Karibu kila mtu duniani leo anaweza kupata Biblia nzima au sehemu fulani za Biblia. Isitoshe, Mwana wa Mungu alisema: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika neno langu, . . . mtajua kweli.” (Yohana 8:31, 32) Kwa hiyo, watu wanaweza kujua kweli. Mamilioni ya watu wenye mioyo minyofu kutoka dini mbalimbali wanaendelea kukubali kweli hiyo kwa ujasiri na kuunganishwa katika ibada ya kweli.—Mathayo 28:19, 20; Ufunuo 7:9, 10.

Muungano wa Ulimwenguni Pote Katika Wakati Wetu!

Unabii wenye kutokeza katika kitabu cha Biblia cha Sefania unasema kuhusu kuunganishwa pamoja kwa watu wa malezi mbalimbali. Unasema hivi: “Maana hapo ndipo [mimi Yehova Mungu] nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la BWANA, wamtumikie kwa nia moja.” (Sefania 3:9) Ni jambo lenye kupendeza kama nini kuona watu waliobadilika wakimtumikia Mungu kwa muungano!

Jambo hilo lingetukia wakati gani? Andiko la Sefania 3:8 lasema: “Ningojeni, asema BWANA, hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.” Naam, wakati Yehova anapokusanya mataifa na kabla hajawamwagia ghadhabu yake, anawapa wapole wa dunia lugha safi. Wakati huo umeshafika, kwa kuwa tayari mataifa yote yameanza kukusanywa kwa ajili ya vita ile kuu ya Mungu Mweza Yote, Har-Magedoni.—Ufunuo 16:14, 16.

Ili kuunganisha watu wake, Yehova amewapa lugha safi. Lugha hiyo mpya yatia ndani kuelewa ifaavyo kweli ya Biblia kuhusu Mungu na makusudi yake. Kuzungumza lugha safi kwahusisha kuiamini kweli, kuwafundisha wengine, na kuishi kupatana na sheria na kanuni za Mungu. Kwataka tuepuke siasa zenye kugawanya na kung’oa kabisa kutoka mioyoni mwetu mitazamo ya ubinafsi, kama vile ubaguzi wa rangi na mambo ya kizalendo ya ulimwengu huu. (Yohana 17:14; Matendo 10:34, 35) Watu wote wenye mioyo minyofu ambao wanapenda kweli wanaweza kujifunza lugha hiyo. Fikiria wale watu watano waliotajwa katika makala iliyotangulia—ambao awali walifuata dini mbalimbali—lakini sasa wameungana katika kumwabudu Mungu mmoja tu na wa pekee, Yehova.

Wameungana Katika Ibada ya Kweli

Wakati Fidelia, Mkatoliki mwaminifu alipomnunulia binti yake Biblia ya kutumia shuleni alimwuliza kasisi amweleze akitumia Biblia, ni nini kilichowapata watoto wake watano waliokufa. “Jibu lake lilinivunja moyo kama nini!” asema. Kwa hiyo Mashahidi wa Yehova walipomtembelea, aliwauliza swali hilohilo. Aliposoma katika Biblia yake mwenyewe ukweli kuhusu hali ya wafu, alitambua jinsi alivyokuwa amedanganywa na kanisa. Alifahamu kwamba wafu hawajui jambo lolote na kwa hiyo hawateseki katika Ahera au mahali kwingineko. (Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5) Fidelia alitupa sanamu zake zote za kidini, akaacha kwenda kwenye kanisa hilo, na kuanza kujifunza Biblia. (1 Yohana 5:21) Kwa muda wa miaka kumi ambayo imepita, amefurahia kuwafundisha wengine kweli za Kimaandiko.

Tara anayetoka Kathmandu alihamia nchi fulani iliyokuwa na mahekalu machache ya Wahindu. Kwa hiyo alizuru kanisa la Kimethodisti akiwa na tumaini la kutosheleza mahitaji yake ya kiroho. Lakini hakupata jibu lolote kuhusu sababu inayofanya wanadamu wateseke. Kisha Mashahidi wa Yehova wakamtembelea na kujitolea kujifunza Biblia pamoja naye. Tara asema: “Niling’amua kwamba Mungu mwenye upendo hawezi kuwa anasababisha mateso yote ulimwenguni . . . Nilifurahishwa sana na taraja la ulimwengu mpya wenye amani na upatano.” (Ufunuo 21:3, 4) Tara alitupa sanamu zake za Kihindu, akaacha kufuata desturi za kidini za nchi yake, na akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alifurahia sana kuwasaidia wengine watosheleze mahitaji yao ya kiroho.

Panya, mfuasi wa Buddha, alikuwa mpiga ramli wakati Mashahidi wa Yehova walipomtembelea kwa mara ya kwanza huko Bangkok. Kwa hiyo alipendezwa sana na unabii mbalimbali wa Biblia. Panya alisema: “Nilipojua ni kwa nini hali za sasa ni tofauti na jinsi Muumba alivyokusudia hapo awali na jinsi anavyopanga kuondoa madhara yanayosababishwa na wale wanaomkataa na kukataa enzi kuu yake, nilihisi kana kwamba nimefunguliwa macho. Ujumbe wote wa Biblia ulipatana sana. Nilipata kumpenda na kumwona Yehova kuwa mtu halisi; na jambo hilo lilinichochea kufanya mambo niliyojua kuwa ni sawa. Nilikuwa na hamu ya kuwasaidia wengine waone tofauti iliyopo kati ya hekima ya kibinadamu na hekima ya Mungu. Hekima ya kweli imebadili maisha yangu kwelikweli.”

Baada ya muda, Virgil alianza kushuku sana imani yake ya kidini. Badala ya kusali kwamba Mungu awasaidie watu weusi au lile aliloliona kuwa shirika la ubaguzi wa rangi lililochochea chuki dhidi ya wazungu, alisali apate kweli, mahali popote ambapo ingepatikana. “Nilipoamka siku iliyofuata baada ya kusali kwa Mungu kwa bidii,” asema Virgil, “nilipata gazeti Mnara wa Mlinzi ndani ya nyumba. . . . Lazima liwe lilipitishwa chini ya mlango.” Punde si punde akaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova kwa bidii. Aendelea kusema: “Kwa mara ya kwanza maishani, nilihisi nimeridhika. . . . Nikaanza kuwa na tumaini.” Punde si punde Virgil aliungana na watu ambao huwapa wengine tumaini pekee la kweli kama lipatikanavyo katika Neno la Mungu, Biblia.

Charo anayeishi Amerika Kusini alifurahi wakati Shahidi mmoja anayeitwa Gladys alipoona kwamba alikuwa anasumbuliwa na watoto wake wadogo na akamsaidia kwa kumpeleka sokoni. Baada ya muda, Charo alikubali kujifunza Biblia na Gladys. Charo alishangaa sana alipojifunza katika Biblia yake kwamba si watu wote wazuri watakaoenda mbinguni, bali Yehova atawabariki wanadamu wengine kwa kuwapa uhai udumuo milele duniani. (Zaburi 37:11, 29) Charo amekuwa akiwaeleza wengine tumaini hilo kwa miaka 15.

Hebu wazia dunia nzima ikiwa imejaa watu wanyofu walioungana katika kumwabudu Yehova, Mungu wa pekee wa kweli! Hiyo si ndoto tu. Ndivyo Yehova ameahidi. Kupitia nabii wake Sefania, Mungu alisema hivi: “Nitasaza ndani yako watu walioonewa na maskini, nao watalitumainia jina la BWANA. . . . Hawatatenda uovu, wala kusema uongo; wala ulimi wa hadaa hautaonekana kinywani mwao; . . . wala hapana mtu atakayewaogofya.” (Sefania 3:12, 13) Ikiwa unavutiwa na ahadi hiyo, zingatia himizo hili la Biblia: “Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.”—Sefania 2:3.